Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wafuasi wa karibu dini zote kubwakubwa wanaamini kwamba wanadamu wana nafsi isiyoweza kufa

HABARI KUU | BIBLIA INASEMA NINI KUHUSU UHAI NA KIFO?

Swali Lenye Kutatanisha

Swali Lenye Kutatanisha

WATU wana maoni mbalimbali kuhusu uhai na kifo. Baadhi yao hufikiri kwamba baada ya kufa wataendelea kuishi wakiwa viumbe hai katika mwili tofauti au katika makao mengine. Wengine huhisi kuwa watazaliwa tena katika umbo lingine. Na pia wengine hufikiri kifo ndio mwisho wa mambo yote.

Huenda unaamini jambo tofauti, ikitegemea malezi au utamaduni wako. Kwa kuwa maoni kuhusu kile ambacho hutendeka tunapokufa yanatofautiana sana, je, kuna mtu yeyote au kitabu chochote kinachoweza kutupatia jibu sahihi na lenye kutegemeka la swali hilo lenye kutatanisha?

Kwa karne nyingi, viongozi wa kidini wamefundisha fundisho la kutokufa kwa nafsi. Wafuasi wa karibu dini zote kubwakubwa kama vile Wakristo, Wahindu, Wayahudi, Waislamu, na wengine wanaamini kwamba wanadamu wana nafsi isiyoweza kufa, ambayo huendelea kuishi katika ulimwengu wa roho baada ya mwili kufa. Kwa upande mwingine, Wabudha wanaamini kwamba, roho au nguvu iliyo ndani ya mtu inapozaliwa upya tena na tena inaweza kufikia makao ya raha na amani yaitwayo Nirvana.

Kwa sababu ya mafundisho kama hayo, watu wengi duniani wanaamini kifo ni njia ya kuingia ulimwengu mwingine. Wengi huona kifo kuwa hatua muhimu katika mzunguko wa maisha ya wanadamu, na wanakiona kuwa ni mapenzi ya Mungu. Hata hivyo, Biblia inasema nini kuhusu jambo hilo? Tafadhali chunguza makala inayofuata. Huenda ukashangazwa na jibu lake.