Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wanazi Hawakufaulu Kunibadili

Wanazi Hawakufaulu Kunibadili

Wanazi Hawakufaulu Kunibadili

Limesimuliwa na Hermine Liska

AMANI na utulivu nilioufurahia nikiwa mtoto ulikatizwa ghafula katika mwaka wa 1938 wakati Adolf Hitler na chama chake cha Nazi kilipochukua mamlaka Austria, nchi ya nyumbani kwetu. Punde si punde mimi na wanafunzi wenzangu tuliamuriwa tutoe salamu ya “Heil Hitler,” kuimba nyimbo za Nazi, na kujiunga na Kikundi cha Vijana cha Hitler. Nilikataa katakata kufanya mambo hayo. Hebu nieleze kwa nini nilikataa.

Mimi na kaka zangu wanne tulilelewa kwenye shamba moja huko St. Walburgen katika jimbo la Carinthia, Austria. Wazazi wangu waliitwa Johann na Elisabeth Obweger. Katika mwaka wa 1925, Baba akawa Bibelforscher, au Mwanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo. Mama alibatizwa mwaka wa 1937. Tangu nilipokuwa mtoto, walinifundisha kanuni za Biblia na kunisaidia nimpende Mungu na uumbaji wake. Kwa mfano, walinifundisha ni kosa kumwabudu mwanadamu yeyote. Yesu Kristo alisema: “Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu, na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.”—Luka 4:8.

Mama na Baba walipenda sana kuwakaribisha wageni. Tulitembelewa na wageni wengi na baadhi ya wale waliofanya kazi katika shamba letu waliishi na familia yetu ya watu saba. Tuliimba mara nyingi—zoea ambalo bado linapendwa sana katika jimbo la Carinthia—na mara nyingi sana tulikuwa na mazungumzo yenye kupendeza ya Biblia. Bado ninakumbuka funzo la Biblia ambalo familia yetu ilikuwa nalo kila Jumapili (Siku ya Yenga) asubuhi sebuleni.

Tunaacha Kuwa Huru Tunaanza Kuishi kwa Woga

Ujerumani ilitwaa Austria nilipokuwa na umri wa miaka minane hivi. Tangu wakati huo na kuendelea, watu walilazimishwa kufuata sera za chama cha Nazi, na punde si punde raia wote waliamuriwa watoe salamu za “Heil Hitler.” Nilikataa kufanya hivyo kwa sababu neno “heil” katika Kijerumani linamaanisha “wokovu,” na singeweza kusema kwamba Hilter ndiye mwokozi wangu! Nilijua kwamba Yesu Kristo ndiye Mwokozi wangu. (Matendo 4:12) Kwa sababu ya msimamo wangu, nilidhihakiwa mara nyingi na walimu na wanafunzi wenzangu. Nilipokuwa na umri wa miaka 11, mwalimu mkuu wa shule ya msingi niliyohudhuria aliniambia: “Hermine, nitakurudisha hadi darasa la kwanza. Siwezi kuvumilia mtoto mkaidi kama wewe katika darasa langu!”

Kwa sababu mimi na ndugu zangu tulikataa kabisa kutoa salamu ya heil Hitler, Baba aliagizwa afike kortini. Aliambiwa atie sahihi hati fulani kuonyesha kwamba ameikana imani yake. Hati hiyo pia ilimwagiza awalee watoto wake kulingana na sera za Nazi. Kwa sababu alikataa kutia sahihi hati hiyo, yeye na Mama walinyang’anywa watoto wao, nami nikatumwa katika kituo kimoja cha kuelimisha watu upya kilichokuwa kilomita 40 hivi kutoka nyumbani.

Nilitamani sana kurudi nyumbani na nililia sana. Nikiwa huko, yule aliyekuwa akitutunza alijaribu kunilazimisha nijiunge na Kikundi cha Vijana cha Hitler, lakini nikakataa. Wasichana wengine walijaribu kuinua mkono wangu wa kulia ili niisalimu bendera ya Nazi, lakini hawakufaulu. Nilihisi kama watumishi wa Mungu wa kale waliosema: “Ni jambo lisilowaziwa, kwa upande wetu, kumwacha Yehova ili kuitumikia miungu mingine.”—Yoshua 24:16.

Wazazi wangu walizuiwa wasinitembelee. Hata hivyo, tulikutana kisiri nilipokuwa nikienda shuleni na pia nilipokuwa shuleni. Pindi hizo zilinitia moyo sana niendelee kuwa mwaminifu kwa Yehova. Pindi moja tulipokutana, Baba alinipa Biblia ndogo, nami nikaificha vizuri kitandani mwangu. Nilifurahia sana kuisoma, ingawa nilifanya hivyo kisiri. Siku moja, karibu nipatikane nikisoma Biblia hiyo, lakini niliificha haraka chini ya blanketi.

Napelekwa Kwenye Makao ya Watawa

Kwa kuwa jitihada zote za kunielimisha upya hazikufua dafu, wenye mamlaka walishuku kwamba bado nilikuwa nikiwasiliana na wazazi wangu. Hivyo, mnamo Septemba (Mwezi wa 9) 1942, nilisafirishwa kwa gari-moshi hadi Munich, Ujerumani, na nikatiwa katika shule ya Wakatoliki iliyoitwa Adelgunden, ambayo pia ilikuwa makao ya watawa wa kike. Nilipokuwa nikipelekwa huko, watawa waliiona Biblia yangu na wakaichukua.

Hata hivyo, nilikuwa nimeazimia kuendelea kushikilia imani yangu kwa hivyo nilikataa kuhudhuria ibada kanisani. Nilipomwambia mmoja wa watawa kwamba wazazi wangu walikuwa na zoea la kunisomea Biblia kila Jumapili, alifanya jambo lililonishangaza. Alinirudishia Biblia yangu! Inaonekana kwamba yale niliyomwambia yalimgusa moyo. Hata aliniruhusu nimsomee Biblia hiyo.

Pindi moja, mwalimu fulani aliniambia hivi: “Hermine, una nywele zenye rangi ya dhahabu, na macho ya bluu. Kwa hiyo, wewe ni Mjerumani, si Myahudi. Yehova ni Mungu wa Wayahudi.”

Nilimjibu: “Lakini Yehova ndiye aliyefanya kila kitu. Yeye ndiye Muumba wa kila mtu!”

Mwalimu mkuu pia alijaribu kunishinikiza. Wakati mmoja, aliniambia: “Hermine, mmoja wa ndugu zako amejiunga na jeshi. Unapaswa kufuata mfano wake mzuri!” Nilijua kwamba mmoja wa ndugu zangu alikuwa amejiunga na jeshi, lakini sikuwa na nia yoyote ya kufuata mfano wake.

“Mimi si mfuasi wa ndugu yangu,” nilimwambia. “Mimi ni mfuasi wa Yesu Kristo.” Mwalimu huyo mkuu alitisha kunipeleka kwenye hospitali ya watu walio na matatizo ya akili, hata akamwagiza muuguzi ajitayarishe kunipeleka. Hata hivyo, hakufanya hivyo.

Katika majira ya kiangazi ya mwaka wa 1943, Munich ilishambuliwa kwa mabomu, na watoto kutoka shule ya Adelgunden wakahamishwa hadi sehemu za mashambani. Wakati wa kipindi hicho, mara nyingi nilitafakari maneno ya Mama: “Iwapo siku moja tutatenganishwa na hutapokea barua zozote kutoka kwangu, kumbuka kwamba Yehova na Yesu wako pamoja nawe. Hawatakuacha kamwe. Kwa hiyo, endelea kusali.”

Naruhusiwa Kurudi Nyumbani

Mnamo Machi (Mwezi wa 3) 1944, nilirudishwa Adelgunden, ambako mara nyingi, iwe mchana au usiku tulijificha mahali fulani kwa sababu mji wa Munich ulikuwa ukishambuliwa sana kwa mabomu yaliyorushwa kutoka angani. Wazazi wangu waliomba mara nyingi kwamba nirudishwe nyumbani. Mwishowe ombi lao lilikubaliwa, na niliwasili nyumbani mwishoni mwa Aprili (Mwezi wa 4) 1944.

Nilipoenda kumuaga mwalimu mkuu, aliniambia hivi: “Hermine, tuandikie barua utakapofika nyumbani. Na udumishe msimamo wako.” Mtazamo wa mwalimu huyo ulikuwa umebadilika kama nini! Nilipata habari kwamba punde tu nilipoondoka, wasichana tisa na watawa watatu waliuawa wakati wa shambulizi la bomu. Vita ni kitu kiovu sana!

Kwa upande mwingine, nilifurahi sana kuungana tena na familia yetu. Mei (Mwezi wa 5) 1944, vita vikiwa bado vinaendelea, nilibatizwa kwenye beseni kubwa ya kuogea, na hivyo kuonyesha wakfu wangu kwa Yehova. Vita vilipokwisha mwaka wa 1945, nilianza utumishi wa wakati wote, nikiwa na hamu ya kuwaambia wengine habari njema za Ufalme wa Mungu ambao ndio tumaini pekee kwa wanadamu la kuleta amani na usalama.—Mathayo 6:9, 10.

Katika mwaka wa 1950, nilikutana na Erich Liska, mhudumu anayesafiri wa Mashahidi wa Yehova kutoka Vienna, Austria. Tulifunga ndoa mwaka wa 1952, na kwa muda mfupi, niliandamana na Erich alipotembelea makutaniko ili kuyaimarisha kiroho.

Mtoto wetu wa kwanza alizaliwa mwaka wa 1953, na baadaye tukapata watoto wengine wawili. Kwa sababu majukumu yetu yaliongezeka, tuliacha utumishi wa wakati wote ili tuweze kuwalea watoto wetu. Nimejifunza kwamba ukishikamana na Mungu, hatawahi kukukatisha tamaa, bali atakupa nguvu. Hajawahi kunikatisha tamaa. Hasa baada ya mume wangu mpendwa kufa mwaka wa 2002, Yehova amenifariji na kunitia nguvu.

Ninapotafakari maisha yangu, ninawashukuru sana wazazi wangu kwa kukazia katika moyo wangu mchanga tamaa ya kumpenda Mungu na Neno lake lililoandikwa, ambalo ndilo chanzo cha hekima ya kweli. (2 Timotheo 3:16, 17) Lakini zaidi ya hayo, ninamshukuru sana Yehova ambaye anaendelea kunipa nguvu za kuvumilia majaribu maishani.

[Blabu katika ukurasa wa 19]

“Mimi si mfuasi wa ndugu yangu . . . Mimi ni mfuasi wa Yesu Kristo”

[Picha katika ukurasa wa 19]

Nikiwa na familia yetu kwenye shamba letu huko St. Walburgen

[Picha katika ukurasa wa 19]

Wazazi wangu, Elisabeth na Johann Obweger

[Hisani]

Both photos: Foto Hammerschlag

[Picha katika ukurasa wa 20]

Mimi na mume wangu, Erich