Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Yehova, Umenipata!”

“Yehova, Umenipata!”

“Yehova, Umenipata!”

Simulizi la Nelly Lenz

“Je, ninyi ni Mashahidi wa Yehova?” Hivyo ndivyo nilivyowauliza wanaume wawili waliokuja nyumbani kwetu. “Ndiyo,” wakajibu. Kisha nikawaambia, “Mimi pia!” Nilikuwa na umri wa miaka 13 tu na sikuwa nikihudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme. Wazazi wangu hawakuwa Mashahidi wa Yehova. Basi, kwa nini nilijitambulisha kuwa Shahidi wa Yehova?

KAMA si Mashahidi wa Yehova, huenda singezaliwa kamwe. Mama yangu alipata mimba alipokuwa akiishi huko Montreal, Quebec, Kanada. Alikuwa na umri wa miaka 17 tu. Familia yake ilimshurutisha atoe mimba. Naye akakubali.

Mama aliomba ruhusa kazini ili akatoe mimba. Inaonekana msimamizi wake, ambaye ni Shahidi wa Yehova, alijua kwa nini aliomba ruhusa kutoka kazini. Alimwambia Mama kwamba uhai ni zawadi yenye thamani sana. (Zaburi 139:13-16) Mama alipokuwa njiani kuelekea hospitalini, alifikiria mambo aliyokuwa ameambiwa na mwajiri wake. Aliamua kutotoa mimba. Baada ya kunizaa katika mwaka wa 1964, mama yangu alinipeleka kwenye makao ya kutunzia mayatima.

Kusikia Kuhusu Kweli ya Biblia Mara ya Kwanza

Nilipokuwa na umri wa miaka miwili hivi, mama yangu na mume wake, ambaye alikuwa amemwoa karibuni, walinitoa kwenye makao ya mayatima. Tulipokuwa tukiishi Sainte-Marguerite-du-Lac-Masson, walianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova na kuhudhuria mikutano ya kutaniko. Hata hivyo, punde baadaye tukahamia Boisbriand na wazazi wangu wakaacha kujifunza.

Miaka michache baadaye walianza tena kujifunza. Nilisikiliza kwa makini yale yaliyosemwa kuhusu tumaini linalozungumziwa katika Biblia kwamba dunia itakuwa paradiso. (Luka 23:43) Nikaanza kumpenda Yehova sana.

Hata hivyo, siku moja Mama aliniambia kwamba wameacha kujifunza na Mashahidi na kwamba hatutaenda tena kwenye Jumba la Ufalme. Mwanzoni, hilo lilinifurahisha. Nikiwa mtoto wa umri wa miaka minane, niliona kwamba mikutano inachukua muda mrefu sana. Jioni hiyo nilitaka kuongea na Yehova katika sala, lakini sikuwa na uhakika kwamba atanisikiliza.

Alasiri ya Jumapili iliyofuata, niliwaona majirani zetu waliokuwa Mashahidi wa Yehova, wakienda kwenye Jumba la Ufalme kuhudhuria mkutano. Nilianza kulia na kumuuliza Mungu, “Kwa nini watoto wao wanaenda mikutanoni nami siwezi kwenda?” Hata hivyo, maneno haya ya Zaburi 33:18 yangetimia katika maisha yangu: “Tazama! Jicho la Yehova linawaelekea wale wanaomwogopa, wale wanaozingojea fadhili zake zenye upendo.”

Kurudi Kwenye Jumba la Ufalme

Majuma matatu baadaye, niliwatembelea majirani zetu na kumwambia Lilianne, mama yao, kwamba ninataka kuhudhuria mikutano. Lilianne aliniambia kwamba haiwezekani kwa kuwa mama yangu hapendi Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, nilisisitiza. Hivyo akanipeleka nyumbani na kumwomba mama yangu ruhusa niende pamoja nao. Nilishangaa Mama alipokubali. Alisema kwamba mikutano itanifundisha maadili mazuri. Hivyo, nilihudhuria mikutano kila Jumapili.

Kwa miaka mitatu hivi, nilihudhuria mikutano ya kutaniko. Lakini nilipokuwa na umri wa miaka 11, wazazi wangu walitalikiana kisha mimi na mama yangu tukahama. Kwa mara nyingine tena singeweza kuwasiliana na Mashahidi wa Yehova.

Tukio Lisilotazamiwa

Siku moja nikiwa nimeketi kwenye ngazi za nyumba yetu, Mashahidi wawili—Eddie Besson na Don Fisher walikuja na kuniuliza ikiwa wazazi wangu wako nyumbani. Nilipowaambia kwamba hawapo, watu hao waliondoka. Lakini niliwafuata mbio, na tukawa na mazungumzo yaliyo katika utangulizi.

Inaeleweka ni kwa nini watu hao walishangaa nilipojitambulisha kuwa Shahidi wa Yehova. Niliwaeleza hali yangu na kuwasihi warudi jioni hiyo. Nilipomwambia Mama kwamba Mashahidi watatutembelea, alikasirika sana na kusema kwamba hatawakaribisha. Hata alipanga kuondoka kabla hawajawasili. Nilimsihi Mama kwa machozi asiondoke. Alipokuwa akijitayarisha kuondoka, mlango ulibishwa. Eddie Besson alikuwa amewasili. Wazia jinsi nilivyofurahi Mama alipokubali kujifunza Biblia!

Hatimaye niliweza tena kuhudhuria mikutano ya kutaniko! Hata hivyo, kabla ya mwaka mmoja kwisha, mama yangu aliacha tena kujifunza. Wakati huo, alinikataza nisishirikiane na Mashahidi na kutupa vitabu vyote vya Mashahidi wa Yehova alivyopata. Hata hivyo niliweza kuficha Biblia, kitabu cha nyimbo, mabuku mawili ya Mnara wa Mlinzi, Vitabu vya Mwaka vya Mashahidi wa Yehova viwili, na kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele. * Katika funzo langu la mwisho, nilimuuliza Eddie Besson yale ninayopaswa kufanya kwani ninampenda Yehova sana. Alinitia moyo nijifunze kibinafsi na kusali mara nyingi. Alinihakikishia kwamba Yehova atanitunza. Nilikuwa na umri wa miaka 14 hivi.

Kufanya “Mikutano” Peke Yangu

Kuanzia wakati huo, kila Jumapili niliingia chumbani mwangu na kuwazia kwamba nilikuwa kwenye mikutano. Niliimba wimbo “Kazia Zawadi Macho Yako!” nilipoanza na nilipomaliza kwa kuwa huo ndio wimbo wa Ufalme niliokumbuka. Mpaka leo, mimi hutokwa machozi ninapoimba wimbo huo. Pia nilisoma makala ya Mnara wa Mlinzi kwenye yale mabuku niliyokuwa nayo. Nilimaliza “mkutano” wangu kwa sala. Hivyo, ingawa sikushirikiana na Mashahidi, nilihisi kwamba Yehova alikuwa karibu nami.

Nilipokuwa na umri wa miaka 17, mimi na Mama tulihamia Montreal. Miaka hiyo ilikuwa na magumu mengi kwani familia yetu haikuwa na upendo.

Ninapatikana!

Siku moja Mama alipokea kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani kutoka kwa Mashahidi wa Yehova. Nilipofika nyumbani, nilikiona kitabu hicho mezani nami nikaanza kukitazama. Nilipoona kwamba kina jina la Mungu, Yehova, nilianza kulia na kusali hivi kimyakimya, “Yehova, umenipata!”

Nilitaka kuwasiliana na ndugu na dada zangu Wakristo. Lakini ningewezaje? Mama aliniambia kwamba huenda jirani yetu mmoja ni Shahidi wa Yehova. Hivyo, nilipokuwa nikienda kazini nilipitia kwake na kubisha mlango. Mwanamume mmoja aliyekuwa na usingizi alifungua mlango. Alishangaa sana nilipomwambia kwamba mimi ni Shahidi wa Yehova na ninataka kubatizwa! Alipanga ili dada mmoja Mkristo anayeitwa Josée Miron anifundishe Biblia. Lakini Mama alianza tena kunipinga nisijifunze Biblia. Aliniambia kwamba ninapaswa kungoja hadi nifike umri wa miaka 18 kabla ya kuwa Shahidi.

Je, Nimwache Yehova Ili Nipate Familia?

Mwajiri wangu alitambua kwamba mambo yalikuwa yakizidi kuwa mabaya nyumbani. Mara nyingi alinikaribisha tufanye mambo pamoja naye na mke wake mwishoni mwa juma. Kwa kuwa ninapenda farasi, mara nyingi tuliendesha farasi pamoja. Niliwaona kuwa wazazi wangu.

Siku moja mwajiri wangu aliniambia kwamba yeye na mke wake wananipenda sana na hivyo wanataka niishi nao. Alikuwa akiniahidi kitu ambacho nilikuwa nimetamani sana sikuzote, yaani, familia yenye upendo. Lakini kulikuwa na sharti moja—niache kushirikiana na Mashahidi wa Yehova. Walinipa juma moja nifikirie jambo hilo, lakini sikuhitaji hata siku moja. Niliwajibu papo hapo. Yehova hajawahi kuniacha kamwe, nami siwezi kumwacha kamwe.

Kumtumikia Mungu

Kwa sababu ya matatizo niliyopata nyumbani, nilienda kuishi na baba yangu wa kambo. Alinitia moyo niendelee kujifunza, nami nikabatizwa Desemba 17, 1983, nikiwa na umri wa miaka 19. Nilifurahi sana kumwona Eddie Besson siku hiyo ya ubatizo. Sasa hakuwa na shaka lolote kwamba mimi ni Shahidi wa Yehova!

Hata hivyo, maoni ya baba yangu wa kambo yalibadilika baada ya ubatizo wangu. Wakati wowote niliposali, alizungumza kwa sauti kubwa na hata kunitupia vitu! Pia alisisitiza kwamba niendeleze masomo yangu, na hilo lingeathiri mradi wangu wa kuwa painia, yaani, mhubiri wa wakati wote. Hatimaye alinifukuza nyumbani. Alinipa hundi ya dola 100 na kuniambia kwamba wakati nitakapoipeleka benki ili kupata pesa taslimu, nitajua kwamba Yehova hanijali.

Nilianza upainia Septemba 1, 1986, na bado nina hundi hiyo! Nyakati nyingine ilikuwa vigumu kuhubiri maeneo ya mashambani bila gari. Lakini washiriki wa kutaniko letu walinitegemeza na kunisaidia sana.

Muda si muda, nilikutana na mwanamume Mkristo mwenye fadhili anayeitwa Ruben Lenz. Tulifunga ndoa mwaka wa 1989. Kwa sasa, Ruben ni mzee wa kutaniko huku Milton, Ontario, Kanada, ambapo tumeishi tangu mwaka wa 2002. Ndoa yetu ni mojawapo ya baraka kubwa zaidi ambazo Yehova amenipa. Niliendelea kuhubiri wakati wote, hadi tulipopata mtoto wetu wa kwanza, Erika, mwaka wa 1993. Miaka mitatu hivi baadaye, tulimpata mwana anayeitwa Mika. Baada ya miaka mingi ya upweke, Yehova Mungu amenibariki sana kwa kunipa familia inayompenda kama ninavyompenda.

Ingawa nyakati nyingine nilitenganishwa na watu wa Yehova nilipokuwa nikikua, sikuacha kamwe kumtumaini Mungu na kushikilia tumaini la uzima wa milele katika Paradiso. (Yohana 3:36) Ninafurahi sana kwamba Yehova “alinipata”!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 17 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Nikiendesha farasi wa mwajiri wangu

[Picha katika ukurasa wa 15]

Nelly Lenz akiwa na mume wake, Ruben, na watoto wake, Erika na Mika