Hamia kwenye habari

APRILI 25, 2024
PARAGUAI

Mashahidi Waonyesha Neno la Mungu Kwenye Maonyesho ya Vitabu Nchini Paraguai

Mashahidi Waonyesha Neno la Mungu Kwenye Maonyesho ya Vitabu Nchini Paraguai

Kuanzia Februari 28 hadi Machi 10, 2024, maonyesho ya vitabu ya kila mwaka yanayojulikana kama Libroferia Capel yalifanyika Asunción, nchini Paraguai. Watu wapatao 10,000 hivi wa umri mbalimbali huhudhuria maonyesho hayo kila mwaka. Zaidi ya ndugu na dada 160 walijitolea kutoa ushahidi kwenye banda letu la machapisho na wengi walivutiwa sana na Neno la Mungu na walipata msaada wa jinsi ya kujifunza Biblia kwenye jw.org. Nakala za kielektroni na zilizochapishwa za machapisho yetu zilipatikana katika Kiguarani, Lugha ya Ishara ya Paraguai, na Kihispania.

Mwanamume mmoja alikaribia banda letu la machapisho baada ya kuona tangazo la funzo la Biblia bila malipo. Ndugu zetu walimfafanulia jinsi funzo la Biblia linavyoongozwa na wakamwonyesha mwanamume huyo broshua Furahia Maisha Milele! Baada ya kusoma yaliyomo mwanamume huyo alisema hivi: “Sikujua kwamba Biblia inaweza kujibu maswali haya yote!” Pia, alifurahi sana kujifunza jina la Mungu la kibinafsi, Yehova. Mipango ilifanywa ili kuwasiliana naye na kuanzisha funzo la Biblia.

Katika pindi nyingine, mwanamume mwingine alianza kuzungumza na dada zetu waliokuwa kwenye banda letu la machapisho. Alieleza jinsi alivyofurahi kuona habari mbalimbali zilizokuwa zikipatikana kwenye tovuti yetu katika lugha ya Kiguarani, Kiguarani (Mbyá), na lugha ya Nivaclé. Aliwapongeza Mashahidi wa Yehova kwa jitihada walizofanya ili kutafsiri machapisho yanayotegemea Biblia katika lugha mbalimbali za wenyeji.

Baadhi ya wajitoleaji ambao walishiriki katika jitihada za kutoa ushahidi

Ndugu Daniele Sarcone, ambaye alisaidia kuwapanga wajitoleaji alisema: “Tulifurahi sana kuwa na mazungumzo mazuri pamoja na wale waliopendezwa na kujifunza mambo mengi kuhusu Biblia.” Katika muda wote wa tukio hilo, angalau watu 13 waliomba habari kuhusu jinsi wanavyoweza kujifunza Biblia kibinafsi.

Tunafurahi kwamba ushahidi mzuri unaendelea kutolewa nchini Paraguai na hivyo watu wengi wanaweza kujifunza kuhusu Biblia na Yehova.​—Zaburi 119:160.