Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Mtendee Mwenzi Wako wa Ndoa kwa Heshima

Mtendee Mwenzi Wako wa Ndoa kwa Heshima

Siri ya Furaha ya Familia

Mtendee Mwenzi Wako wa Ndoa kwa Heshima

Will * anasema: “Rachel anapokasirika, yeye hulia kwa muda mrefu. Tunapoketi chini kuzungumzia jambo hilo, yeye huzidi kuudhika na kuamua kunyamaza. Hakuna mbinu inayofaulu. Ninahisi kwamba nimekata tamaa.”

Rachel anasema: “Will alipokuja nyumbani nilikuwa nikilia. Nilijaribu kumweleza kwa nini nilikuwa ninalia, lakini hakuacha nimalize. Aliniambia kwamba hilo ni jambo dogo na hivyo nilipaswa kuliacha tu. Hilo liliniudhi hata zaidi.”

JE, NYAKATI nyingine wewe huhisi kama Will na Rachel? Wote wawili wanataka kuelezana hisia zao, lakini mara nyingi wao hukasirika. Kwa nini?

Wanaume na wanawake hueleza hisia zao kwa njia tofauti. Mara nyingi, mwanamke anaweza kutamani kueleza waziwazi hisia zake. Wanaume nao, hujaribu kudumisha amani kwa kusuluhisha matatizo mara moja na kuepuka masuala yaliyo magumu. Unawezaje kushinda matatizo hayo na kuwasiliana na mume au mke wako? Kwa kumtendea mume au mke wako kwa heshima.

Mtu mwenye heshima anawathamini wengine na kujaribu kuelewa hisia zao. Tangu utotoni, huenda ulijifunza kuwaheshimu zaidi watu walio na mamlaka au ujuzi mwingi kuliko wako. Hata hivyo, katika ndoa, tatizo ni kumwonyesha heshima mtu ambaye unahisi kana kwamba uko sawa naye, yaani, mwenzi wako. “Ninajua kwamba Phil angemsikiliza kwa makini mtu yeyote yule ambaye angeongea naye,” anasema Linda, ambaye alifunga ndoa miaka minane iliyopita. “Ninataka awe mwenye huruma kwangu pia.” Yaelekea unawasikiliza marafiki na watu wengine kwa makini na kuzungumza nao kwa heshima. Lakini je, unamtendea mke au mume wako vivyo hivyo?

Ukosefu wa heshima unaleta hali ya wasiwasi nyumbani na mwishowe kusababisha ugomvi. Mtawala mmoja mwenye hekima alisema: “Afadhali mkate mkavu kwa amani, kuliko karamu katika nyumba ya ugomvi.” (Methali 17:1, Biblia Habari Njema) Biblia inamshauri mume amtendee mke wake kwa heshima. (1 Petro 3:7) Pia, “mke anapaswa kumheshimu sana mume wake.”—Waefeso 5:33.

Mtafanya nini ili mweze kuwasiliana kwa heshima? Fikiria mifano ifuatayo kutoka katika Biblia.

Mume au Mke Wako Anapokuwa na Jambo la Kusema

Tatizo: Watu wengi wanapenda kuongea zaidi kuliko kusikiliza. Je, wewe ni mmoja wao? Biblia inasema kwamba mtu ‘anayejibu jambo kabla ya kulisikia’ ni mpumbavu. (Methali 18:13) Kwa hiyo, sikiliza kwanza kabla ya kusema. Kwa nini? “Mimi ninafurahi mume wangu asipojaribu kutatua matatizo yangu mara moja,” anasema Kara ambaye alifunga ndoa miaka 26 iliyopita. “Sihitaji akubali au ajaribu kuelewa chanzo cha tatizo langu. Ninataka tu anisikilize na atambue kwamba hisia zangu ni za kweli.”

Kwa upande mwingine, wanaume na wanawake fulani husita kujieleza na hawajihisi huru ikiwa mwenzi wao atajaribu kuwalazimisha waeleze jinsi wanavyohisi. Lorrie, ambaye aliolewa hivi karibuni, ametambua kwamba inamchukua mume wake muda mrefu kueleza hisia zake. Anasema: “Ninahitaji kuwa na subira na kumngoja aeleze hisia zake.”

Suluhisho: Ikiwa wewe na mwenzi wako wa ndoa mnahitaji kuzungumza kuhusu jambo fulani linaloweza kuleta ugomvi, lizungumzieni wakati ambapo nyote wawili mmetulia. Namna gani ikiwa mwenzi wako anasita kuzungumzia hisia zake? Tambua kwamba “shauri moyoni mwa mtu ni kama kilindi cha maji, lakini mtu mwenye utambuzi ataliteka.” (Methali 20:5) Ikiwa utaivuta ndoo iliyojaa maji kutoka katika kisima haraka-haraka, basi maji mengi yatamwagika. Vivyo hivyo, ikiwa utazungumza na mume au mke wako kwa ukali, ataudhika na hutaweza kujua yaliyo moyoni mwake. Badala yake, uliza maswali kwa upole na heshima, na uwe na subira ikiwa mwenzi wako hataki kueleza hisia zake mara moja.

Mwenzi wako anapozungumza, uwe “mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema, si mwepesi wa ghadhabu.” (Yakobo 1:19) Msikilizaji mzuri hasikilizi tu maneno yanayosemwa, bali pia hujaribu kuelewa hisia zilizofanya maneno hayo yasemwe. Mume au mke wako anapozungumza, jaribu kuelewa hisia zake. Mwenzi wako atatambua kama unamheshimu au humheshimu kutokana na jinsi unavyomsikiliza.

Yesu alifundisha jinsi ya kusikiliza. Kwa mfano, wakati mwanamume fulani mgonjwa alipomwomba amponye, Yesu hakufanya hivyo mara moja. Kwanza, alisikiliza maneno ya kusihi ya mgonjwa huyo. Kisha, maneno hayo yakamsukuma kumsikitikia sana na mwishowe akamponya. (Marko 1:40-42) Iga mfano wa Yesu mwenzi wako anapozungumza. Kumbuka kwamba, anataka mtu wa kumsikitikia kutoka moyoni, na si kumpa suluhisho la mara moja. Hivyo, msikilize kwa makini. Jaribu kujiweka katika hali yake. Baada ya kufanya hayo, ndipo unapoweza kuanza kushughulikia mahitaji yake. Ukifanya hivyo, utaonyesha kwamba unamheshimu mke au mume wako.

JARIBU KUFANYA HIVI: Mume au mke wako anapoanza kuzungumza nawe, jizuie usimjibu mara moja. Subiri hadi amalize kuzungumza na uhakikishe umeelewa yale anayosema. Baadaye, unaweza kumuuliza, “Je, unahisi kwamba nilikusikiliza kwa makini?”

Unapotaka Kusema Jambo Fulani

Tatizo: “Vipindi vya vichekesho kwenye televisheni, vimefanya ionekane kuwa ni jambo la kawaida kuongea vibaya kumhusu mwenzi wako na hata kumtukana na kumdhihaki,” anasema Linda, aliyetajwa hapo awali. Watu wengine wamelelewa katika familia ambazo kuongea bila heshima ni jambo la kawaida. Baadaye wanapofunga ndoa, inakuwa vigumu kwao kuwaheshimu watu wa familia zao. Ivy anayeishi Kanada, anasema: “Nililelewa katika familia ambapo dhihaka, kupiga kelele, na matusi yalikuwa mambo ya kawaida.”

Suluhisho: Unapozungumza na watu wengine kumhusu mwenzi wako waeleze “neno lolote ambalo ni jema kwa ajili ya kujenga kulingana na uhitaji, ili liwape wasikiaji lile linalofaa.” (Waefeso 4:29) Ongea kumhusu mume au mke wako kwa njia ambayo itawafanya wengine wamheshimu.

Hata mnapokuwa peke yenu, epuka dhihaka na matusi. Katika Israeli la kale, Mikali alimkasirikia mume wake, Mfalme Daudi. Aliongea kwa dhihaka akisema kwamba Daudi alijiendesha “kama vile mmoja wa watu wapumbavu.” Maneno yake yalimuumiza Daudi na kumchukiza Mungu pia. (2 Samweli 6:20-23) Tunajifunza nini? Unapozungumza na mume au mke wako, chagua maneno ya kusema. (Wakolosai 4:6) Phil, ambaye amekuwa katika kifungo cha ndoa kwa miaka minane, anasema bado kuna mambo ambayo yeye na mke wake hawakubaliani. Ametambua kwamba nyakati nyingine mambo anayosema hufanya hali iwe mbaya hata zaidi. “Nimetambua kwamba ‘kushinda’ mabishano kunaweza kuharibu uhusiano kati ya mume na mke. Hivyo, ninaona inafaa na inaridhisha kuimarisha uhusiano huo.”

Mjane mmoja mzee katika nyakati za kale, aliwaambia wake za watoto wake watafute “mahali pa kupumzika kila mmoja katika nyumba ya mume wake.” (Ruthu 1:9) Mume na mke wanapoheshimiana, wanafanya nyumba yao iwe “mahali pa kupumzika.”

JARIBU KUFANYA HIVI: Tenga wakati ambao wewe na mwenzi wako mnaweza kutumia kuzungumzia mambo ambayo yamedokezwa chini ya kichwa hiki kidogo. Muulize hivi: “Ninapoongea kukuhusu mbele ya watu, je, unahisi nimekuheshimu au kukuaibisha? Ninaweza kufanya marekebisho gani ili kuboresha hali hiyo?” Sikiliza kwa makini mwenzi wako anapoeleza hisia zake. Jaribu kufanya marekebisho anayopendekeza.

Tambua Kwamba Wewe na Mwenzi Wako Mna Maoni Tofauti

Tatizo: Wenzi fulani wapya wa ndoa wamefikiri kimakosa kwamba Biblia inaposema “mwili mmoja” inamaanisha kwamba wanapaswa kuwa na maoni au sifa zilezile. (Mathayo 19:5) Hata hivyo, wanatambua upesi kwamba hivyo si ndivyo ilivyo. Baada ya muda fulani, mara nyingi tofauti zao zinafanya waanze kubishana. Linda anasema: “Tofauti moja kubwa kati yangu na Phil ni kwamba yeye hahangaishwi sana na mambo kama mimi. Nyakati nyingine anaweza kutulia tu huku nikihangaishwa na jambo fulani, hivyo mwishowe ninakasirika kwa kuwa anaonekana kama hajali kuhusu jambo hilo.”

Suluhisho: Mthamini mwenzi wako jinsi alivyo, na uheshimu maoni yake ambayo yanaweza kuwa tofauti na yako. Kwa mfano: Macho na masikio yako yanafanya kazi kwa njia tofauti, lakini yanashirikiana na ndiyo maana unaweza kuvuka barabara bila kugongwa na gari. Adrienne ambaye alifunga ndoa miaka 30 hivi iliyopita, anasema: “Mimi na mume wangu tunaweza kuwa na maoni tofauti bora tu yasipingane na Neno la Mungu. Kwani, hata kama tumeoana sisi ni watu wawili walio tofauti.”

Mwenzi wako anapokuwa na maoni au hisia tofauti na zako, usikazie fikira mapendezi yako tu. Fikiria hisia zake. (Wafilipi 2:4) Kyle, mume wa Adrienne, anasema: “Si wakati wote ninaelewa au kukubaliana na maoni ya mke wangu. Lakini ninajikumbusha kwamba ninampenda zaidi ya jinsi ninavyopenda maoni yangu. Anapokuwa na furaha, hata mimi ninakuwa na furaha.”

JARIBU KUFANYA HIVI: Andika mambo yanayoonyesha kwamba maoni au njia ya mwenzi wako ya kufanya mambo ni bora kuliko yako.—Wafilipi 2:3.

Heshima ni mojawapo ya siri ya kuwa na ndoa yenye furaha. “Heshima huleta uradhi na usalama katika ndoa,” anasema Linda. “Bila shaka, ni sifa inayofaa kukuzwa.”

[Maelezo ya Chini]

^ Majina yamebadilishwa.

JIULIZE . . .

▪ Tofauti zetu zimeimarishaje familia yetu?

▪ Kwa nini inafaa kukubaliana na mapendezi ya mume au mke wangu ikiwa hakuna kanuni za Biblia zinazovunjwa?