Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Siku Yenye Furaha na Matazamio Makubwa

Siku Yenye Furaha na Matazamio Makubwa

Kuhitimu kwa Darasa la 130 la Gileadi

Siku Yenye Furaha na Matazamio Makubwa

BILA shaka, kuhitimu kwa darasa la 130 la Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead) kulichochea matumaini na matazamio ya wengi. Siku ya Jumamosi (Siku ya Posho), Machi 12, 2011 (12/3/2011), zaidi ya watu 8,500 walihudhuria sherehe hiyo ya kuhitimu, kutia ndani wanafunzi na watu wao wa familia na marafiki. Matarajio yalikuwa mengi, si kuhusu tu programu ya siku hiyo, bali pia kuhusu wakati ujao wa wamishonari hao waliozoezwa vizuri ambao walikuwa karibu kutumwa sehemu mbalimbali duniani ili kuwafundisha watu kweli za Biblia.

“Wenye Furaha Ni Wale Wote Wanaoendelea Kumtarajia” Yehova

Wazo hilo lenye kutia moyo linalotoka katika andiko la Isaya 30:18, ndilo kichwa cha hotuba iliyotolewa na Geoffrey Jackson, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, ambaye ndiye aliyekuwa mwenyekiti wa programu hiyo. Kwa uchangamfu na ucheshi kidogo, aliwapongeza wanafunzi wote kwa kumaliza masomo yao magumu na akawahakikishia kwamba hata siku hiyo ya kuhitimu itaisha pia licha ya wasiwasi waliokuwa nao. Wanafunzi wangekuwa na matazamio gani yanayofaa kuhusu wakati ujao? Alizungumzia hoja tatu zinazoweza kuwasaidia zinazotajwa katika andiko la Isaya 30:18-21.

Kwanza, Ndugu Jackson alisema, “Mnaweza kutarajia kwamba Yehova atasikia sala zenu.” Alitaja uhakikisho unaotolewa kwenye mstari wa 19: “Hakika [Mungu] atakuonyesha kibali unapotoa sauti ya kilio chako.” Katika Kiebrania, neno “atakuonyesha” linalotumiwa katika mstari huo liko katika umoja na si wingi, hivyo Ndugu Jackson akaonyesha kwamba Yehova anasikiliza sala za mtu mmojammoja. “Kama Baba, Yehova haulizi, ‘Kwa nini usiwe jasiri kama yule mtu mwingine?’ Badala yake, anamsikiliza kila mtu kwa makini, na kumjibu.”

Pili, msemaji alitaja kwamba tunaweza kutazamia matatizo. “Yehova hatuahidi kwamba maisha yatakuwa rahisi, bali anaahidi kutusaidia.” Kama mstari wa 20 unavyoonyesha, Mungu alitabiri kwamba wakati ambapo Waisraeli wangezingirwa, wangefahamu minyanyaso na ukandamizaji kama wanavyofahamu mkate na maji. Na bado Yehova sikuzote angekuwa tayari kuwaokoa watu wake. Pia, wanafunzi wa Gileadi watakabili matatizo mbalimbali, ingawa huenda yasiwe yale wanayotazamia! Ndugu Jackson aliongeza kusema, “Lakini unaweza kutazamia kwamba Yehova atakuwa tayari kukusaidia ukabiliane na kila tatizo.”

Tatu, Ndugu Jackson aliwakumbusha wanafunzi kwamba kama inavyoonyeshwa na mstari 20 na 21, “mnaweza kutazamia mwongozo, hivyo, utafuteni!” Ndugu Jackson alisema kwamba leo, kila Mkristo anahitaji kusikiliza kwa makini Yehova anapozungumza kupitia Biblia na machapisho yanayotegemea Biblia. Kwa uchangamfu, aliwahimiza wanafunzi waendelee kusoma Biblia kila siku, kwa sababu jambo hilo linamaanisha uhai.

“Hofu ya Yehova na Iwe Juu Yenu”

Anthony Morris, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alieleza maana ya usemi wa Biblia, “hofu ya Yehova.” (2 Mambo ya Nyakati 19:7) Hofu ya Yehova si aina fulani ya woga usiofaa, bali, ni tamaa kubwa ya kufanya yaliyo sawa, na heshima kubwa ya kutoka moyoni ambayo inaweza kumfanya mtu atetemeke. “Iweni na hofu hiyo mnapoenda kwenye mgawo wenu wa umishonari,” Ndugu Morris akawahimiza wanafunzi. Ni kwa njia gani wanafunzi wanaweza kumwonyesha Yehova heshima hiyo kubwa? Msemaji alikazia njia mbili muhimu za kufanya hivyo.

Kwanza, Ndugu Morris aliwahimiza wanafunzi watii shauri kwenye Yakobo 1:19: ‘Uwe mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema.’ Alitaja kwamba wanafunzi wamejifunza mambo mengi katika muda wa miezi mitano ya masomo yao, lakini wanapaswa kuwa waangalifu wasijigambe kuhusu mambo waliyojifunza watakapokuwa kwenye migawo yao. “Unapaswa kusikiliza kwanza,” akasema. “Wasikilize akina ndugu katika kutaniko utakaloshirikiana nalo na wale wanaongoza katika nchi utakayotumwa; sikiliza yale wanayosema kuhusu nchi hiyo na utamaduni wake. Usisite kusema, ‘Sijui.’ Ikiwa umefaidika na masomo yako, basi kadiri utakavyoendelea kujifunza, ndivyo utakavyozidi kutambua kuwa unafahamu mambo machache.”

Pili, Ndugu Morris alisoma Methali 27:21: “Chungu cha kusafishia ni kwa ajili ya fedha, na tanuru ni kwa ajili ya dhahabu; na mtu hulingana na sifa yake.” Alieleza kuwa kama dhahabu na fedha zinavyohitaji kusafishwa, ndivyo sisi tunavyoweza kusafishwa na sifa tunazopewa. Jinsi gani? Kusifiwa kunaweza kututia katika jaribu. Kunaweza kufanya tuwe na kiburi na kupoteza uhusiano wetu na Yehova, au tuone kama tunadaiwa na Yehova na hivyo kuazimia kabisa tusimkosee. Hivyo, Ndugu Morris akawahimiza wanafunzi wawe na mtazamo unaofaa wanaposifiwa, yaani, watumie nafasi hiyo kuthibitisha kwamba ‘wana hofu inayofaa kumwelekea Yehova.’

“Thamini Mgawo Wako wa Umishonari”

Guy Pierce, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alitoa hotuba ya msingi katika programu hiyo. Alizungumzia kichwa ambacho kimetajwa hapo juu, akieleza maana ya neno “mmishonari” kuwa “mtu aliyetumwa kutimiza mgawo au kazi fulani.” Pia, alieleza kuwa si ajabu kwamba kuna mashirika mbalimbali yanayotuma wamishonari ili watimize kazi au migawo mbalimbali. Wengi wao hukazia fikira matibabu ya kimwili na kutafuta suluhisho la kisiasa kwa matatizo ya ulimwengu. “Nyinyi ni tofauti,” akasema. Jinsi gani?

Katika masomo yao yaliyotegemea Biblia, wanafunzi walizungumzia mambo mengi kuhusu uponyaji wa kimwili. Yesu alipomfufua msichana mdogo, wazazi wake ‘walikuwa na shangwe kubwa.’ (Marko 5:42) Vivyo hivyo, vipofu walipoponywa kimuujiza, walifurahi sana. Sababu moja ya miujiza hiyo ni kutuonyesha yale ambayo Kristo atatimiza katika ulimwengu mpya unaokuja wakati ambapo “umati mkubwa” wa wanadamu waadilifu ambao wataokoka mwisho wa ulimwengu huu mwovu, wataponywa magonjwa yao yote. (Ufunuo 7:9, 14) Wapendwa wao waliokufa, ambao watawakaribisha wakati wa ufufuo, pia watakuwa na afya nzuri. Itakuwa furaha iliyoje!

Hata hivyo, kama Ndugu Pierce alivyoeleza, uponyaji utakaokuwa muhimu zaidi si wa kimwili. Wagonjwa walioponywa na Yesu walipatwa na ugonjwa tena baadaye. Wafu aliowafufua walikufa tena baadaye. Hata vipofu aliowaponya walikuwa vipofu tena katika kifo. Uponyaji uliokuwa muhimu zaidi ambao Yesu alifanya ni ule wa kiroho—kuwasaidia watu wamrudie Mungu na kuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye. Wamishonari wa Gileadi wana mgawo wa kuwaponya watu kiroho. Wanawasaidia watu wamrudie Baba yetu wa mbinguni ili wawe hai kiroho. Wale ambao wameponywa kiroho ndio tu watakaopata uzima wa milele. “Uponyaji huo wa kiroho,” akasema Ndugu Pierce, “ndilo jambo linalomletea Mungu sifa. Linafanya ufanikiwe katika utumishi wako.”

Mambo Mengine Matatu Makuu Katika Programu

“Je, Hii Itakuwa Siku Nzuri?” Robert Rains, mshiriki wa Halmashauri ya Ofisi ya Tawi ya Marekani, alizungumzia swali hilo. Aliwahimiza wanafunzi wahakikishe kuwa kila siku katika mgawo wao wa umishonari ni siku nzuri, kwa kutumia wakati wao kwa hekima, kwa kuchunguza Neno la Mungu wanapokuwa na mahangaiko, na kwa kumtegemea Yehova kupitia sala.

“Je, Utafanya Mambo ya Zamani Kuwa Mapya?” Mark Noumair, mwalimu wa shule ya Gileadi, alianza hotuba yake kwa kuuliza swali hilo. Alizungumzia andiko la 1 Yohana 2:7, 8, ambapo mtume Yohana anataja “amri ya zamani” ambayo pia ni “amri mpya.” Amri hizo mbili zinarejelea agizo lilelile—kwamba wafuasi wa Kristo wapendane bila ubinafsi, wakiwa na roho ya kujitolea. (Yohana 13:34, 35) Sheria hii ilikuwa ya zamani kwa kuwa Kristo alikuwa amewapa wafuasi wake miaka mingi iliyokuwa imepita; hata hivyo, ilikuwa mpya pia kwa kuwa Wakristo walikuwa wanakabili matatizo mengine mapya na walihitaji kuuonyesha upendo kwa njia nyingine mpya na kwa ukamili zaidi. Wamishonari pia wanakabili hali mpya na wanahitaji kujifunza kuonyesha upendo kulingana na hali hizo. Siri ya kufanya hivyo ni nini?

“Usiwe kile unachochukia,” Ndugu Noumair akawahimiza. Alionya kwamba ikiwa mtu atatutendea jambo fulani tunalochukia, kisha sisi tumtendee vivyo hivyo, basi tutakuwa kile tunachochukia, na kufanya hivyo ni kujiangamiza wenyewe. Kwa upande mwingine, ikiwa badala ya kufanya hivyo tutatafuta njia nyingine za kuwaonyesha upendo watu kama hao, tutaangaza “nuru ya kweli” na kufukuza giza la kiroho.

“Beba Mzigo.” Michael Burnett, mwalimu mwingine wa shule ya Gileadi, alizungumzia kichwa hiki kinachofaa. Alieleza kuhusu baadhi ya watu barani Afrika ambao wanabeba mizigo kichwani. Wanatumia kata, kipande cha kitambaa kilichoviringwa na kuwekwa kichwani ili mzigo usiyumbeyumbe wala kumuumiza anayeubeba. Pia, kubeba mzigo kwa njia hiyo humfanya mbebaji atembee vizuri. Wamishonari wa Gileadi watahitaji kubeba mzigo mzito wa majukumu katika nchi watakazotumwa, lakini wamepewa kitu kinachoweza kulinganishwa na kata: mazoezi mengi yanayotegemea Biblia. Wanapoendelea kufuata mambo waliyojifunza, wataweza kubeba mzigo wao kwa usawaziko na kutembea vizuri.

Mambo Yaliyoonwa na Mahojiano

Mazoezi ya Gileadi yanatia ndani kuhubiri pamoja na makutaniko ya Mashahidi wa Yehova yaliyo karibu. William Samuelson, mwangalizi wa Idara ya Shule za Kitheokrasi, alizungumzia mambo ambayo wanafunzi waliona walipokuwa wakihubiri. Hotuba yake ilikuwa na kichwa, “Usiache Mkono Wako Upumzike.” (Mhubiri 11:6) Kwa kuigiza mambo waliyoona, wanafunzi walioonyesha jinsi walivyohubiri habari njema kwa bidii, wakitafuta nafasi za kuzungumza na watu kwenye ndege, katika mikahawa, na hata vituo vya mafuta. Kando na kuhubiri nyumba kwa nyumba, walizungumza na watu mahali pengine popote walipopatikana, na pia wakahubiri kupitia barua. Kwa kweli, hawakuacha mikono yao ipumzike, na matokeo yalikuwa mazuri sana.

Kisha, Kenneth Stovall, mfanyakazi katika idara inayosimamia Shule ya Gileadi, akawahoji ndugu watatu waliotumika wakiwa wamishonari kwa muda mrefu. Nao ni Barry Hill aliyetumika nchini Ekuado na Jamhuri ya Dominika, Eddie Mobley aliyetumika nchini Côte d’Ivoire, na Tab Honsberger aliyetumika nchini Senegal, Benin, na Haiti. Hotuba hiyo ya mahojiano ilikuwa na kichwa “Mjaribu Yehova na Uvune Baraka.” (Malaki 3:10) Kwa mfano Ndugu Hill alieleza jinsi yeye na mke wake walivyohitaji kuzoea mabadiliko ya hali ya hewa nchini Ekuado. Nyakati nyingine kunakuwa na joto na vumbi, na nyakati nyingine joto na matope. Anakumbuka kwamba kwa miaka miwili na nusu, walioga kwa kutumia ndoo. Lakini hawakufikiria kuacha mgawo wao; waliuona kuwa baraka kutoka kwa Yehova. “Tulihisi kuwa hali hizo ni sehemu ya maisha yetu,” akasema.

Mwishoni mwa programu, mmoja wa wanafunzi alisoma barua yenye kugusa moyo kutoka kwa wanafunzi wenzake. Katika barua hiyo walitoa shukrani zao za kutoka moyoni kwa ajili ya mambo waliyojifunza. “Imani yetu imeimarishwa sana,” barua hiyo ikaeleza, “na bado tunajua kuwa tunahitaji kuendelea kufanya maendeleo.” Wanafunzi wote walipewa diploma zao na migawo ya kwenda nchi mbalimbali. Ndugu Jackson alimalizia programu kwa kuwahakikishia wanafunzi kwamba wanaweza kutazamia msaada wa Yehova katika maisha yao, hasa wanapokabili hali ngumu. Wote waliokuwepo waliondoka wakiwa na matumaini na matazamio makubwa zaidi. Bila shaka, Yehova atawatumia wamishonari hao wapya kutimiza mambo mengi mazuri.

[Chati/​Ramani katika ukurasa wa 31]

TAKWIMU ZA DARASA

9 nchi zilizowakilishwa

34.0 wastani wa umri

18.6 wastani wa miaka tangu kubatizwa

13.1 wastani wa miaka katika huduma ya wakati wote

[Ramani]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Wahitimu walitumwa katika nchi zilizoonyeshwa hapa chini

MIGAWO YA WAMISHONARI

ARGENTINA

ARMENIA

BURKINA FASO

BURUNDI

KONGO (KINSHASA)

JAMHURI YA CHEKI

HAITI

HONG KONG

INDONESIA

KENYA

LITHUANIA

MALASIA

MSUMBIJI

NEPAL

PAPUA NEW GUINEA

RUMANIA

SENEGAL

TANZANIA

UGANDA

ZIMBABWE

[Picha katika ukurasa wa 31]

Darasa la 130 Lililohitimu la Shule ya Gileadi

Katika orodha iliyo chini, nambari za safu zinaanza mbele kwenda nyuma, na majina yameorodheshwa kuanzia kushoto kwenda kulia katika kila safu.

(1) Molina, Z.; Bassolino, S.; Alatsis, C.; Arroyo, A.; Niño, L.; Merkling, S.; Clark, M.

(2) Little, C.; Tibaudo, S.; Jakobsson, S.; Moreno, J.; Rodriguez, A.; Lee, K.; Cárdenas, H.; Aguilar, L.

(3) Clairbush, A.; Polley, A.; Caldwell, S.; Adame, J.; Hildebrandt, S.; Shoemaker, I.; Grohman, N.; Galvez, G.

(4) Clark, J.; Bassolino, A.; Packham, K.; Adame, J.; Knaus, M.; Niño, M.; Moreno, R.; Galvez, J.

(5) Rodriguez, D.; Geynes, M.; Molina, J.; Aguilar, A.; Alatsis, I.; Manno, A.; Grohman, R.; Packham, J.

(6) Geynes, S.; Cárdenas, M.; Arroyo, C.; Manno, C.; Merkling, J.; Lee, H.; Clairbush, X.; Jakobsson, P.

(7) Little, J.; Hildebrandt, B.; Shoemaker, M.; Knaus, K.; Caldwell, J.; Tibaudo, F.; Polley, C.