Hamia kwenye habari

Kazi ya Uchapishaji ya Ulimwenguni Pote Inayowasaidia Watu Kujifunza Kumhusu Mungu

Kazi ya Uchapishaji ya Ulimwenguni Pote Inayowasaidia Watu Kujifunza Kumhusu Mungu

Ulimwenguni pote, watu husoma machapisho ya Mashahidi wa Yehova. Mamilioni ya watu husoma machapisho hayo katika mfumo wa kielektroniki kama unavyofanya sasa. Hata hivyo, huenda ukashangazwa kujua ukubwa wa kazi yetu ya uchapishaji. Kufikia mwaka wa 2013, machapisho yetu yanayotegemea Biblia yalikuwa yakipatikana katika lugha 700 na kugawanywa katika nchi 239.

Kabla ya mwaka wa 1920, machapisho yetu yalikuwa yakichapishwa na mashirika ya kibiashara. Katika mwaka huo, tulianza kuchapisha baadhi ya magazeti na vijitabu vyetu katika jengo dogo la kukodiwa huko Brooklyn, New York. Tangu mwanzo huo mdogo hadi kufika sasa tuna viwanda 15 vya uchapishaji katika bara la Afrika, Asia, Australia, Ulaya, Amerika Kaskazini, na Amerika Kusini.

Kitabu Chetu Muhimu Zaidi

Biblia ndicho kitabu muhimu zaidi tunachochapisha. Katika mwaka wa 1942, tulichapisha Biblia nzima ya kwanza ya Kiingereza ya King James Version. Tangu mwaka wa 1961, Mashahidi wa Yehova wametafsiri na kuchapisha Biblia nzima ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Kufikia mwaka wa 2013, tulikuwa tumechapisha zaidi ya nakala milioni 184 za Biblia hiyo katika lugha 121.

Tarakimu hizo hazielezi mambo yote kuihusu Biblia yenyewe. Biblia tunazochapisha ni imara sana. Karatasi zilizotumiwa kutengeneza kurasa zake hazina asidi ambayo ingeweza kuzifanya zibadilike rangi na kuwa za manjano na pia karatasi hizo zimeunganishwa pamoja vizuri. Hilo limefanya Biblia hiyo iweze kudumu kwa muda mrefu licha ya matumizi yake ya kila siku.

Machapisho Mengine

Pia, tunachapisha machapisho yanayowasaidia watu kuielewa Biblia. Ona takwimu fulani za mwaka wa 2013:

  • Mnara wa Mlinzi, jarida letu kuu, linachapishwa katika lugha zaidi ya 210 na ndilo gazeti linalosambazwa kwa wingi zaidi ulimwenguni. Nakala 45,000,000 huchapwa kwa kila toleo lenye kurasa 16.

  • Amkeni!​—gazeti la pili linalosambazwa kwa wingi zaidi duniani na ambalo hutolewa pamoja na Mnara wa Mlinzi​—linachapishwa katika lugha 99. Nakala 44,000,000 hivi huchapishwa kwa kila toleo.

  • Biblia Inafundisha Nini Hasa? ni kitabu chenye kurasa 224 kilicho na jalada jepesi na ambacho kimeandaliwa kwa kusudi hasa la kuwasaidia wasomaji waelewe mafundisho ya msingi ya Biblia. Tangu mwaka wa 2005, zaidi ya nakala milioni 214 za kitabu hicho zimechapishwa katika lugha zaidi ya 240.

  • Msikilize Mungu ni broshua yenye kurasa 32 iliyoandaliwa kwa ajili ya wale wasiojua kusoma vizuri. Broshua hiyo ina picha nzuri zenye kuvutia na maelezo mafupi kuzihusu​—mambo yanayomsaidia msomaji kuelewa kweli za Biblia kwa njia rahisi. Zaidi ya nakala milioni 42 za broshua hiyo zimechapishwa katika lugha zaidi ya 400.

Pamoja na machapisho hayo, Mashahidi wa Yehova huchapisha vitabu, broshua, na trakti mbalimbali zinazowasaidia wanafunzi wa Biblia kufanyia utafiti maswali yao yanayohusu Biblia, jinsi wanavyoweza kukabiliana na matatizo ya maisha, na jinsi ya kuwa na familia zenye furaha. Katika mwaka wa 2012 viwanda vya uchapishaji vinavyoendeshwa na Mashahidi wa Yehova vilitumiwa kutengeneza zaidi ya magazeti bilioni 1.3 na vitabu na Biblia milioni 80.

Katika mwaka wa 2012 viwanda vya uchapishaji vinavyoendeshwa na Mashahidi wa Yehova vilichapisha zaidi ya magazeti bilioni 1.3 na vitabu na Biblia milioni 80

Wageni wanaotembelea viwanda vyetu vya uchapishaji mara nyingi hushangaa kuona jinsi watu wanavyofanya kazi ya uchapishaji kwa bidii. Wanaume na wanawake hao hutoa wakati na nguvu zao. Wanapokuja Betheli, jina linalomaanisha “Nyumba ya Mungu,” wengi huwa hawana uzoefu wowote katika kazi ya uchapishaji. Hata hivyo, wao huweza kufanya kazi hiyo vizuri kwa kuwa wanazoezwa wakiwa huko na pia kwa sababu ya mazingira mazuri ya kufanyia kazi. Kwa mfano, ni jambo la kawaida kuona wanaume vijana wenye umri wa miaka 20 hivi wakiendesha mashine ya uchapishaji inayofanya kazi kwa kasi sana na ambayo ina uwezo wa kuchapisha nakala 200,000 za gazeti la kurasa 16 kwa saa moja.

Pesa Zinatoka Wapi?

Ulimwenguni pote, kazi inayofanywa na Mashahidi wa Yehova inategemezwa kwa michango ya hiari. Toleo la Agosti 1879 la gazeti la Zion’s Watch Tower, ambalo sasa linaitwa Mnara wa Mlinzi, lilisema hivi: “‘Tunaamini kwamba gazeti ‘Zion’s Watch Tower’ linategemezwa na YEHOVA, na maadamu hivyo ndivyo ilivyo halitawaomba watu wala kuwasihi kamwe walitegemeze.” Bado tunaamini hivyo.

Kwa nini tunatumia muda, pesa, na wakati mwingi katika kazi hiyo? Kwa sababu iwe unasoma mojawapo ya mamilioni ya Biblia na vitabu tunavyochapisha au unasoma machapisho hayo kwenye mtandao, tunatumaini kwamba yatakusaidia kumkaribia Mungu.