Hamia kwenye habari

Kuunganishwa kwa Ofisi za Tawi za Mashahidi wa Yehova

Kuunganishwa kwa Ofisi za Tawi za Mashahidi wa Yehova

Kuanzia Septemba 2012, usimamizi wa zaidi ya ofisi 25 za tawi za Mashahidi wa Yehova umehamishwa kwenye ofisi kubwa zaidi.

Isitoshe, ofisi mpya za tawi zimeanzishwa katika nchi ya Serbia na Makedonia. Kuna sababu mbili kuu za mabadiliko hayo.

1. Teknolojia imerahisisha kazi

Katika miaka ya karibuni, maendeleo katika teknolojia ya mawasiliano na uchapishaji yamepunguza uhitaji wa wafanyakazi katika ofisi fulani za tawi. Kwa kuna watu wachache zaidi katika ofisi kubwa za tawi, nafasi imepatikana kwa ajili ya baadhi ya wale waliokuwa wakifanya kazi katika matawi madogo zaidi katika nchi nyingine.

Sasa, katika ofisi hizo kubwa za tawi kuna idadi kubwa ya Mashahidi wenye uzoefu wanaoshughulikia kazi ya elimu ya Biblia. Kwa mfano, kazi ya kuhubiri katika nchi za El Salvador, Guatemala, Honduras, Kosta Rika, Nikaragua, na Panama inasimamiwa na ofisi ya tawi ya Mexico. Kwa sababu hiyo, ofisi za tawi katika nchi hizo sita zilifungwa.

Mashahidi 40 kutoka katika ofisi hizo 6 walipewa mgawo wa kutumika katika ofisi ya tawi ya Mexico. Wengine 95 hivi walibaki katika nchi walimozaliwa wakifanya kazi ya kuhubiri wakati wote.

Wengine katika nchi hizo za Amerika ya Kati walianza kufanya kazi katika ofisi za tafsiri chini ya usimamizi wa ofisi ya tawi ya Mexico. Kwa mfano, Mashahidi karibu 20 nchini Panama wanatafsiri machapisho ya Watchtower katika lugha za kienyeji. Katika ofisi ya tawi ya zamani nchini Guatemala, Mashahidi wapatao 16 sasa wanatafsiri machapisho katika lugha nne za kienyeji. Kwa hiyo, katika Amerika ya Kati, jitihada za kupanga kazi upya zimepunguza idadi ya wafanyakazi katika ofisi za tawi kutoka 300 hadi 75 hivi.

2. Wafanyakazi wana wakati mwingi zaidi wa kuhubiri

Kwa sababu ya kuunganishwa kwa ofisi za tawi, wahubiri wenye uzoefu waliokuwa wakitumika kwenye ofisi ndogo za tawi sasa wanaweza kukazia fikira kazi ya kuhubiri habari njema.

Shahidi mmoja barani Afrika, aliyepewa mgawo wa kuhubiri, aliandika hivi: “Katika miezi michache ya kwanza, haikuwa rahisi kubadili mtindo wangu wa maisha ili ufae hali mpya. Hata hivyo, nimepata shangwe na baraka nyingi sana kwa kushiriki katika utumishi kila siku. Kwa sasa, ninajifunza Biblia na watu 20, na baadhi yao wanahudhuria mikutano ya kutaniko.”