Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Mungu wa Faraja Yote”

“Mungu wa Faraja Yote”

Mkaribie Mungu

“Mungu wa Faraja Yote”

2 Wakorintho 1:3, 4

MAMBO mengi maishani kama vile, kuteseka, kuvunjika moyo, au upweke, yanaweza kumfanya mtu ahuzunike au hata atamauke. Nyakati kama hizo unaweza kujiuliza, ‘Nitapata wapi msaada?’ Maneno ya mtume Paulo yanayopatikana kwenye 2 Wakorintho 1:3, 4 yanaonyesha chanzo cha faraja isiyokoma, yaani, Yehova Mungu.

Katika mstari wa 3, Mungu anaitwa “Baba ya rehema nyororo.” Maneno hayo yanamaanisha nini? Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “rehema nyororo” linaweza kuwa na wazo la kuhisi huruma kwa ajili ya kuteseka kwa wengine. * Kitabu kimoja cha marejeo ya Biblia kinasema kwamba neno hilo linaweza kutafsiriwa “anahisi sikitiko” au “anajali sana.” “Rehema nyororo” za Mungu zinamchochea kutenda. Kujua sifa hiyo ya utu wa Mungu kunatufanya tutake kumkaribia, sivyo?

Pia, Paulo anamrejelea Yehova kama “Mungu wa faraja yote.” Hapo Paulo anatumia neno linalosemekana kutia ndani “wazo la kumliwaza mtu aliye na matatizo au huzuni na la kumsaidia au kumtia moyo.” Kitabu fulani kuhusu Biblia (The Interpreter’s Bible) kinaeleza hivi: “Tunamfariji mtu anayeteseka tunapompa ujasiri wa kuvumilia maumivu yake.”

Huenda ukauliza, ‘Mungu anatufariji jinsi gani na kutupa ujasiri wa kuvumilia maumivu?’ Anafanya hivyo hasa kupitia Neno lake, Biblia, na kupitia zawadi ya sala. Paulo anatuambia kwamba kwa upendo Mungu anatupa Neno Lake ili “kupitia faraja kutokana na Maandiko tuwe na tumaini.” Isitoshe, kupitia sala za kutoka moyoni, tunaweza kuwa na “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote.”—Waroma 15:4; Wafilipi 4:7.

Yehova anawafariji watu wake kwa kadiri gani? Paulo anasema kwamba Mungu “hutufariji katika dhiki yetu yote.” (2 Wakorintho 1:4) Hata tukipatwa na mkazo, maumivu makali, au kuteseka kokote, Mungu anaweza kutupa ujasiri na nguvu tunazohitaji ili kuvumilia hali hizo. Je, hatufarijiwi kujua hilo?

Faraja ambayo Mungu anatoa haimfaidi tu yule anayeipokea. Paulo anaendelea kusema kwamba Mungu anatufariji ili “tuweze kuwafariji wale walio katika namna yoyote ya dhiki kupitia faraja ambayo sisi wenyewe tunafarijiwa na Mungu.” Baada ya kufarijiwa katika dhiki yetu, tunasaidiwa kuwa na hisia-mwenzi kuelekea wengine na tunachochewa kuwasaidia wale walio na uhitaji.

Akiwa “Mungu wa faraja yote,” Yehova haondoi matatizo au maumivu yetu. Hata hivyo, tunaweza kuwa na uhakika wa jambo hili: Tukimwendea ili atufariji, anaweza kutuimarisha tukabiliane na huzuni au matatizo yoyote yanayoweza kutokea maishani. Kwa kweli, Mungu mwenye huruma hivyo anastahili ibada na sifa yetu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Mungu anaitwa “Baba [au, chanzo] ya rehema nyororo” kwa sababu huruma inatoka kwake na ni sehemu ya utu wake.