Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unakumbuka?

Je, Unakumbuka?

Je, umesoma kwa makini makala za hivi karibuni za Mnara wa Mlinzi? Angalia ikiwa unaweza kujibu maswali yafuatayo:

Tunawezaje kuuzima moto wa usemi usiodhibitiwa?

Tunapaswa kuuchunguza moyo wetu. Badala ya kumchambua-chambua ndugu, kwa nini tusichunguze kwa nini tuna mtazamo huo? Je, labda tunamchambua ili tuonekane kuwa bora zaidi? Isitoshe, kuwachambua-chambua wengine kunaweza kufanya tu hali ya kukosana iwe mbaya zaidi.—8/15, ukurasa wa 21.

Sheria ilionyeshaje maoni ya Mungu kuhusu wanawake?

Wanawake Waisraeli walifurahia uhuru mwingi, na waliruhusiwa kupata elimu. Waliheshimiwa na kustahiwa, na haki zao zililindwa.—9/1, ukurasa wa 5-7.

Ni matukio gani yatakayotukia hivi karibuni siku ya Yehova inapozidi kukaribia?

Tangazo la “amani na usalama!” litatolewa. Mataifa yatamshambulia na kumharibu Babiloni Mkubwa. Watu wa Mungu watashambuliwa. Vita vya Har–Magedoni vitatokea, kisha Shetani na roho wake waovu watatupwa ndani ya abiso.—9/15, ukurasa wa 4.

Tunafaidikaje kwa kutojua mwisho utakuja lini?

Kutojua ile siku au saa hususa kunatupatia nafasi ya kufunua mambo yaliyo moyoni mwetu. Kunatupatia fursa ya kuufurahisha moyo wa Mungu. Kunatuchochea kufuatia maisha ya kujidhabihu na kutusaidia kumtegemea Mungu kikamili zaidi na kufuata kwa bidii Neno lake. Zaidi ya hayo, hilo linaruhusu matatizo tunayokabili yatusafishe ili tuwe Wakristo bora zaidi.—9/15, ukurasa wa 24-25.

Tunawezaje kutumia andiko la Mwanzo 3:19 kumsadikisha mtu anayeamini moto wa mateso?

Andiko hilo linasema kwamba baada ya Adamu kufa angerudi mavumbini, halisemi kwamba angeenda katika moto wa mateso.—10/1, ukurasa wa 13.

Ni nani wanaofananishwa na “nyota saba” zinazotajwa katika Ufunuo 1:16 na 20 ambazo ziko katika mkono wa kuume wa Yesu?

Zinafananisha waangalizi wa makutaniko waliotiwa mafuta kwa roho, na kwa maana kubwa zaidi, waangalizi wote.—10/15, ukurasa wa 14.

Familia inaweza kukabilianaje na madeni?

Wenzi wa ndoa wanapaswa kuzungumza waziwazi na kwa utulivu kuhusu madeni yao. Itakuwa vizuri wakichanganua bajeti yao ya sasa. Je, wanaweza kuongeza mapato yao au kupunguza gharama za familia? Wanapaswa kuamua njia watakayotumia kulipa madeni yao, labda kwa kuzungumza na wakopeshaji. Lakini wanapaswa kuona mambo kihalisi na kuwa na maoni yanayofaa kuhusu pesa. (1 Tim. 6:8)—11/1, ukurasa wa 19-21.

Yesu alionyeshaje mtazamo wa unyenyekevu unaorejelewa katika Isaya 50:4, 5?

Mistari hiyo inasema kwamba mtu mwenye “ulimi wa waliofundishwa” hawezi ‘kugeuka upande ulio kinyume.’ Yesu alionyesha mtazamo wa unyenyekevu kwa kusikiliza kwa makini mambo aliyofundishwa na Baba yake. Yesu alitamani na alikuwa tayari kujifunza kutoka kwa Yehova, alitazama kwa makini mfano wa unyenyekevu ambao Mungu aliweka alipowaonyesha rehema wanadamu wenye dhambi.—11/15, ukurasa wa 11.

Stempu ya kumbukumbu nchini Estonia ilithibitishaje utimilifu wa Mashahidi wa Yehova?

Mwaka wa 2007 Ofisi ya Posta ya Kitaifa ilitoa stempu iliyoonyesha mauaji ya jamii nzima za Waestonia wakati wa utawala wa Stalin. Stempu hiyo ilikuwa na namba 382, ambayo ni idadi ya Mashahidi na watoto wao waliohamishwa mwaka wa 1951 na kupelekwa kwenye kambi za kazi ngumu katika maeneo ya mbali nchini Urusi.—12/1, ukurasa wa 27-28.