Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Waathiriwa Waliosahauliwa” Wakumbukwa

“Waathiriwa Waliosahauliwa” Wakumbukwa

Ripoti ya Watangazaji wa Ufalme

“Waathiriwa Waliosahauliwa” Wakumbukwa

MAPEMA mnamo 2001, Haykaz, ambaye ni Shahidi wa Yehova mwenye umri wa miaka 15, alitembelea maonyesho yaliyoitwa “Waathiriwa Waliosahauliwa,” huko Bern, Uswisi, yaliyohusu mateso ambayo Mashahidi wa Yehova walipata kutoka kwa Nazi. Mwishoni mwa ziara yake, Haykaz alisema: “Nilisikia kuhusu vitendo vya ukatili na mateso ambayo Mashahidi wa Yehova walipata chini ya utawala wa Nazi, lakini hii ilikuwa mara ya kwanza kuona hati halisi na picha za wakati huo. Maonyesho, ripoti za mashahidi waliojionea, na maelezo ya wanahistoria kwenye maonyesho hayo yalikazia sana mambo hayo katika akili na moyo wangu.”

Baadaye, Haykaz alipopewa mgawo wa kuandika ripoti kwa ajili ya wanafunzi wenzake katika shule ya sekondari, alichagua kuandika kuhusu, “Mashahidi wa Yehova—Waathiriwa Waliosahauliwa wa Utawala wa Nazi.” Mwalimu wake alikubali aandike kuhusu habari hiyo lakini akamwambia Haykaz kwamba alihitaji kutia ndani habari kutoka katika vitabu vya kilimwengu. Haykaz akakubali kwa furaha. “Niliandika maelezo mafupi ya vitabu fulani nilivyosoma kuhusu Mashahidi wa Yehova wakati wa utawala wa Nazi. Pia nilieleza maoni yangu binafsi kuhusu maonyesho, ‘Waathiriwa Waliosahauliwa.’ Ripoti hiyo ya kurasa 43 ilitia ndani mifano na picha.”

Mnamo Novemba 2002, Haykaz alitoa ripoti yake mbele ya wanafunzi wenzake, walimu, familia, na marafiki. Baadaye, kulikuwa na kipindi cha maswali na majibu, ambacho kilimpa nafasi ya kueleza imani yake inayotegemea Biblia. Msichana mmoja kati ya wasikilizaji alipomwuliza kwa nini alichagua habari hiyo, Haykaz alieleza kwamba vitabu vingi vya historia havitaji Mashahidi wa Yehova, na kwamba alipenda watu wajue jinsi Mashahidi walivyotetea imani yao ya Kikristo kwa ujasiri. Matokeo yakawaje?

“Wanafunzi wenzangu walishangaa,” akasema Haykaz. “Hawakujua kwamba Mashahidi wa Yehova waliteswa kikatili wakiwa kikundi. Pia, wengi hawakujua kwamba katika kambi za mateso za Nazi Mashahidi walivaa alama ya pekee ya rangi ya zambarau yenye pembe tatu.”

Baada ya kutoa habari yake, Haykaz alipata nafasi nyingi zaidi za kuzungumza na wanadarasa wenzake kuhusu msimamo wa Mashahidi unaotegemea Biblia kuhusiana na kutiwa damu mishipani, vileo, na maadili. “Hakuna mwanafunzi yeyote aliyenidhihaki,” akasema Haykaz. Isitoshe, ripoti yake sasa imehifadhiwa katika maktaba ya shule. Hilo litasaidia kuhakikisha kwamba msimamo wa ujasiri wa Mashahidi wa Yehova hautasahauliwa.