Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Shauri Zuri Linahitajiwa?

Je, Shauri Zuri Linahitajiwa?

Je, Shauri Zuri Linahitajiwa?

LEO, wengi wanaamini kwamba wanaweza kutofautisha mema na mabaya, na kwamba wana haki ya kufanya watakalo. Wengine husema kwamba jambo lolote linakubalika mradi tu linawafurahisha. Ndoa na maisha ya familia, ambayo kwa muda mrefu yameonekana kuwa nguzo muhimu za jamii, yameathiriwa sana.—Mwanzo 3:5.

Fikiria Verónica, * ambaye anaishi Mexico. Anasema: “Punde tu kabla ya kusherehekea mwaka wa 15 wa ndoa yetu, mume wangu aliniambia kwamba ana uhusiano na mwanamke mwingine. Alisema kwamba hangemwacha mwanamke huyo kwa sababu alikuwa mwenye umri mdogo na alimfanya afurahi zaidi. Nilishtuka kujua kwamba sitaweza kufurahia ushirika wa rafiki yangu wa karibu zaidi. Nilikuwa nikifikiri kwamba kifo cha wapendwa wetu ndicho kingemfanya mtu aumie zaidi. Lakini mimi niliumizwa hata zaidi na uzinzi kwa sababu nilimpoteza mtu niliyempenda sana, naye aliendelea kufanya mambo yaliyoniumiza.”

Kisha kuna kisa cha mwanamume mwenye umri wa miaka 22 ambaye tayari ametalikiwa na ambaye ana mtoto wa kiume, lakini hataki kukubali jukumu lake akiwa baba. Anatarajia mama yake amtunze na atunze mtoto wake. Mama yake anapokataa kufanya yale anayotaka afanyiwe, yeye hukasirika na kumtusi kama anavyofanya mtoto mtundu. Mama yake hushindwa la kufanya kuhusiana na tabia hiyo yenye kuudhi.

Hivyo ni visa vya kawaida. Kutengana kisheria na talaka ni mambo yanayoongezeka kila mahali. Watoto wengi wameona mmoja wa wazazi wao akiondoka nyumbani na kuanza maisha mapya. Vijana fulani hawawaheshimu wengine hata kidogo, kutia ndani wazazi wao, nao hujiendesha kwa njia ambayo haingewaziwa hapo zamani. Majaribio ya kingono, matumizi ya dawa za kulevya, mashambulizi ya vijana, na mauaji ya walimu au wazazi yanayofanywa na watoto yamekuwa mambo ya kawaida katika nchi nyingi. Na huenda umeona kwamba katika ulimwengu wa sasa kuna hali nyingine maishani ambazo hutokeza magumu mbali na kulea watoto na ndoa.

Tunapoona mambo hayo huenda tukajiuliza jamii imepatwa na nini. Ikiwa kwa kweli watu wanaweza kutofautisha mema na mabaya, kwa nini kuna matatizo mengi ambayo hayajatatuliwa? Je, kuna uhitaji wa shauri zuri? Je, kuna chanzo cha shauri hilo lenye kunufaisha, ambalo limekuwa lenye kutegemeka? Ingawa wengi wanadai kwamba wanamwamini Mungu na Neno lake lililoandikwa, wao hawazingatii jambo hilo wanapofanya maamuzi. Lakini tunaweza kupata manufaa gani tunapotafuta na kupata shauri kutoka kwa Mungu? Na tuzungumzie jambo hilo katika makala inayofuata.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Jina limebadilishwa.