Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wote Wanakaribishwa Kwenye Majumba ya Ufalme

Wote Wanakaribishwa Kwenye Majumba ya Ufalme

Ripoti ya Watangazaji wa Ufalme

Wote Wanakaribishwa Kwenye Majumba ya Ufalme

ALIPOKUWA anawazoeza wanafunzi wake kwa ajili ya kazi ya kuhubiri hadharani, Yesu Kristo aliwatia moyo ‘wahubiri kutoka paa za nyumba.’ (Mathayo 10:27) Naam, walipaswa kufanya huduma yao ya Kikristo hadharani, mbele ya watu wote. Kwa kufuata kanuni ya ushauri huo, Mashahidi wa Yehova pia hufanya kazi yao hadharani. Kwa sababu hiyo Mashahidi wameweza kushinda upinzani na kutambuliwa kwa njia ifaayo.

Ingawa watu wote wanakaribishwa kwenye mikutano ya kutaniko ya Mashahidi wa Yehova, wengine husita kuingia kwenye Jumba la Ufalme kwa sababu ya maoni yasiyofaa. Ndivyo ilivyo nchini Finland. Watu wengine huogopa kuingia mahali wasipopajua. Jumba jipya la Ufalme linapojengwa au la zamani linaporekebishwa, kwa kawaida kunakuwa na mpango wa kuwaalika watu waje kutembezwa na kufurahia viburudisho. Huenda jitihada ya pekee ikafanywa kuwaalika majirani watembelee Jumba la Ufalme ili wapate kujua kazi ya Mashahidi wa Yehova.

Katika eneo moja Mashahidi walipanga wawe na kampeni ya kuwaachia watu magazeti siku ileile ambayo walikuwa wamepanga kuwaalika watu kwenye Jumba lao jipya la Ufalme. Mashahidi wawili walikutana na mzee mmoja aliyesema kwamba alifurahia sana kusoma magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Ndugu walimweleza juu ya mpango huo nao wakajitolea kumpeleka kwenye Jumba la Ufalme. Mzee huyo alisema angefurahia kwenda. Mke wake aliyekuwa akisikiliza mazungumzo hayo, alisema kwa sauti, “Msiniache!”

Walipofika kwenye Jumba la Ufalme, mzee huyo alitazama hapa na pale kisha akasema: “Jumba hili si jeusi hata kidogo. Limepakwa rangi nyangavu yenye kupendeza. Niliambiwa Jumba la Ufalme limepakwa rangi nyeusi!” Mzee huyo na mke wake walikaa kidogo kisha wakaomba wapewe baadhi ya vichapo vilivyokuwa vimewekwa juu ya meza ya vitabu.

Kutaniko moja lilitaka kutangaza kwenye gazeti moja la kwao kwamba watu wamealikwa kutembezwa na kufurahia viburudisho kwenye Jumba la Ufalme wakati wa kuwekwa wakfu. Baada ya kupata habari hizo, mhariri mkuu wa gazeti hilo alipendekeza kwamba makala moja iandikwe kuhusu tukio hilo. Ndugu walikubali, na muda si muda, makala nzuri iliyochukua nusu ya ukurasa mmoja ikachapwa kwenye gazeti hilo, ikizungumzia tukio hilo na kueleza kazi inayofanywa na kutaniko la hapo la Mashahidi wa Yehova.

Baada ya makala hiyo kuchapishwa, Shahidi mmoja mzee alikutana na jirani na kumwambia: “Kuna makala nzuri kuhusu Mashahidi wa Yehova katika gazeti leo!” Dada huyo alimtolea ushahidi na baadaye akamwachia broshua Mashahidi wa Yehova Katika Karne ya 20.

Mbali na kufafanua mambo fulani yasiyoeleweka vizuri kuhusu Mashahidi wa Yehova, mipango kama hiyo ya kuwaalika watu watembelee Majumba ya Ufalme mapya au waje wakati wa kuwekwa wakfu kwa Majumba hayo, kumewachochea sana wahubiri kualika watu wengi zaidi wahudhurie mikutano. Naam, katika nchi nyingi, kutia ndani Finland, watu wamejua kwamba wote wanakaribishwa kwenye Majumba ya Ufalme ya Mashahidi wa Yehova.