Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka Kwa Wasomaji Wetu

Kutoka Kwa Wasomaji Wetu

Kutoka Kwa Wasomaji Wetu

Vijana Huuliza . . . Ninaweza Kufanya Nini ili Nifurahie Kusoma Biblia? (Aprili 2009) Nina umri wa miaka 24, nimeolewa na nina watoto, na sikuzote imekuwa vigumu kwangu kusoma Biblia. Nilifuata madokezo katika makala hiyo, na ninatumia vizuri sanduku linaloweza kukatwa kwenye gazeti hilo. Sasa, mimi hutazamia kwa hamu usomaji wangu wa Biblia. Ninaweza kuona jinsi ambavyo vitabu vya Biblia vinapatana. Ninafurahia sana usomaji wa Biblia kuliko wakati mwingine wowote. Asanteni sana!

K. T., Marekani

Kitabu Kinachotegemeka—Sehemu ya 6 (Aprili 2011) Makala yenye kichwa “Roma na Historia ya Biblia” ilisema: “Jiji la Yerusalemu lilipatwa na nini? Majeshi ya Roma yalirudi, yakiongozwa na Vespasiani na mwana wake Tito—wakati huu majeshi hayo yalikuwa na askari-jeshi 60,000.” Kusema hivyo kunamaanisha kwamba Vespasiani na Tito waliongoza majeshi wakati Yerusalemu liliposhambuliwa. Hata hivyo, vitabu vya kihistoria vinaonyesha kwamba Vespasiani alikuwa Roma wakati huo.

J. O., Australia

“Amkeni!” lajibu: Kulingana na kitabu “Josephus—The Essential Writings,” kilichoandikwa na Paul L. Maier, “Tito aliwasili upesi kutoka Aleksandria, akiwa na kikosi cha Kumi na Tano, na akaungana na baba yake huko Tolemai, ambako Vespasiani alikuwa akimsubiri pamoja na Kikosi cha Tano na cha Kumi.” Kwa kuongezea, kitabu “Encyclopedia of the Roman Empire,” cha Matthew Bunson, kinasema mambo yafuatayo kumhusu Vespasiani: “Akiwa pamoja na mwana wake Tito, alivunjavunja uasi wa Wayahudi na alikuwa akijitayarisha kulizingira hekalu la Yerusalemu mwaka wa 68 wakati alipopata habari kwamba Nero amekufa na mahali pake pakachukuliwa na Galba. . . . Alifika Roma wakati wa majira ya kupukutika ya mwaka wa 70.” Kwa hiyo, inaonekana kwamba mwanzoni Vespasiani na Tito walikuwa pamoja wakati wa uvamizi wa Yerusalemu. Hata hivyo, baadaye Vespasiani alirudi Roma na akamwacha Tito akiongoza jeshi.

Je, Una Miradi Inayopatana na Akili? (Februari 2011) Makala hiyo ilipokuwa ikitoa mifano ya miradi isiyopatana na akili, iliorodhesha “umashuhuri, utajiri, mwenzi bora kabisa wa ndoa, au afya kamilifu.” Kwa nini ilitaja “mwenzi bora kabisa wa ndoa”? Kwa nini wazo la kupata mwenzi wa ndoa wa kudumu si jambo “linalopatana na akili”?

S. K., Marekani

“Amkeni!” lajibu: Makala hiyo haikusema kwamba ndoa yenyewe ni mradi usiopatana na akili. Badala yake, iliongea kuhusu jitihada za kutafuta “mwenzi bora kabisa wa ndoa.” Katika muktadha wa makala hiyo, mwenzi “bora kabisa” wa ndoa ni yule ambaye hana kasoro yoyote, ambaye hafanyi makosa. Kutafuta mwenzi wa namna hiyo ni ubatili kwa sababu mbili hivi: Kwanza, hakuna mtu kama huyo. (Waroma 3:23) Pili, jitihada za kutafuta mwenzi wa namna hiyo hukazia kile ambacho mtu atapata katika ndoa badala ya kile ambacho mtu atatoa katika ndoa. Kuhusiana na hilo, hata baadhi ya wenzi wa ndoa huwa na matarajio yasiyopatana na akili kwamba wanaweza kumgeuza mwenzi wao apatane na vile wanavyofikiri mwenzi “bora kabisa” anapaswa kuwa. Kinyume na hilo, ndoa imara hufanyizwa na watu wawili ambao wanakubali kwamba kila mmoja wao si mkamilifu lakini wanaweza ‘kuendelea kuvumiliana na kusameheana kwa hiari.’—Wakolosai 3:13.