Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Baba Ambaye Watoto Wanahitaji

Baba Ambaye Watoto Wanahitaji

Baba Ambaye Watoto Wanahitaji

WATOTO wanahitaji baba ambaye anawapenda, aliye tayari kuwategemeza, na anayefanya kila anachoweza kuwasaidia kuwa watu wazima wanaotegemeka na kutumainika. Lakini watu wengi hawatambui kwamba watoto wanahitaji baba wa aina hiyo.

Ni kweli kwamba akina mama ndio wanaowazaa watoto, na mama mwenye upendo hutimiza daraka muhimu. Likionyesha kwamba baba pia ana daraka muhimu, jarida The Wilson Quarterly lilisema: “Kushindwa kwa akina baba kutimiza madaraka yao ndicho kisababishi kikuu cha matatizo mengi makubwa yanayoikumba jamii ya Marekani”—na tunaweza kuongezea kwamba ndicho kisababishi kikuu cha matatizo yanayokumba ulimwengu wote.

Gazeti la Brazili Jornal da Tarde linaripoti kuhusu uchunguzi ulioonyesha kwamba mara nyingi matatizo mengi ya kitabia ya vijana, kama vile kuwa wenye jeuri, kuwa watundu, kutofanya vizuri shuleni, na kutojali “husababishwa na kukosekana kwa akina baba.” Na kitabu cha Kiitaliano Gli imperfetti genitori (Wazazi Wasiokamilika) cha Marcello Bernardi kinakazia kwamba watoto wanahitaji kuwa na wazazi wawili ili wakue vizuri.

Maisha ya Familia Yanaweza Kuboreshwa

Hata ikiwa baba anayepuuza madaraka yake amechangia au kusababisha kwa kadiri kubwa matatizo katika familia, haimaanishi kwamba hali haiwezi kurekebishwa na maisha ya familia kuboreshwa. Hilo linawezekanaje? Baba anahitaji kufanya nini?

Hapana shaka kwamba watoto wanahitaji kuwa katika mpango mzuri wa familia, yaani, kuhisi kwamba mtu anayeongoza familia anawahangaikia. Uhitaji huo usipotoshelezwa, kama inavyotukia mara nyingi leo, maisha ya watoto huathiriwa sana. Hata hivyo, baba awepo au asiwepo, bado kuna tumaini. Katika Zaburi 68:5, Biblia inasema hivi: “Baba ya wavulana wasio na baba . . . ni Mungu katika makao yake matakatifu.” *

Jinsi ya Kupata Msaada

Kisa cha Lidia, yule msichana wa Poland aliyetajwa katika makala iliyotangulia, kinaonyesha kwamba msaada wa Mungu ni muhimu kwa ajili ya mafanikio na unaweza kupatikana. Maisha ya familia yao yalikuwaje? Familia hiyo ilipataje msaada wa Mungu?

Franciszek, baba ya Lidia, anakubali kwamba aliipuuza familia yake wakati watoto wake walipokuwa wachanga kama vile binti yake alivyosema. Anasema: “Sikujali kile ambacho watoto wetu walikuwa wakifanya. Sikuwaonyesha kwamba ninawapenda, na hatukuwa na uhusiano wa karibu.” Hivyo, hakujua kwamba wakati ambapo Lidia alikuwa na umri wa miaka 14, tayari yeye na ndugu na dada yake mdogo walikuwa wakienda kwenye karamu za ulevi, kuvuta sigara, kunywa pombe, na kupigana na wengine.

Hatimaye, Franciszek alitambua matatizo yaliyowakabili watoto wake, na aliudhika sana hivi kwamba akaamua kuchukua hatua. Anasema: “Nilimwomba Mungu msaada.” Inapendeza kwamba muda mfupi baadaye, Mashahidi wa Yehova waliwatembelea nyumbani, kisha yeye na mke wake wakakubali kujifunza Biblia. Muda si muda, wazazi hao wakaanza kutumia kanuni za Biblia maishani mwao. Hilo liliwasaidiaje watoto wao?

Franciszek anaeleza hivi: “Watoto wetu walianza kutambua kwamba nimeacha kunywa pombe na kuwa baba mzuri zaidi. Walitaka kuwafahamu vizuri Mashahidi wa Yehova. Walianza pia kujifunza Biblia na kuacha mashirika yao mabaya.” Rafał, mwana wake, anasema hivi kumhusu baba yake: “Nilianza kumpenda kama rafiki.” Kisha anaongeza hivi: “Sikuona tena umuhimu wa kushirikiana na genge la mitaani. Familia yetu ilijishughulisha sana na mambo ya kiroho.”

Sasa Franciszek ni mzee Mkristo katika kutaniko la Mashahidi wa Yehova, naye anaendelea kuhangaikia familia yake na maendeleo ya kiroho ya kila mmoja wao. Mke wake na Lidia ni mapainia, yaani, waeneza-injili wa wakati wote. Rafał na dada yake mdogo Sylwia hushiriki kikamili katika funzo la Biblia, kutoa maelezo katika mikutano ya Kikristo, na kuwahubiria wengine.

Alitenda Yale Aliyofundisha

Fikiria pia yaliyompata Luis, baba ya Macarena. Huyo ni yule msichana mwenye umri wa miaka 21 wa Hispania aliyenukuliwa katika makala iliyotangulia. Luis alimwiga baba yake ambaye alikuwa mlevi. Kama Macarena alivyosema, baba yake alizoea kwenda na marafiki zake na kutorudi nyumbani kwa siku kadhaa. Isitoshe, alimtendea mke wake kama mtumwa badala ya kumtendea kama mwenzi anayethaminiwa. Ndoa yao ilikuwa karibu kuvunjika, na Macarena na ndugu na dada zake wadogo walisononeka sana.

Hatimaye, Luis alikubali kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Anasema: “Nilianza kutumia wakati pamoja na mke na watoto wangu. Tulianza kuzungumza, kula, na kujifunza Biblia pamoja. Pia tulishirikiana kufanya kazi za nyumbani na kufurahia burudani pamoja.” Macarena anasema: “Nilianza kuhisi kwamba nilikuwa na baba anayejali ambaye alipendezwa kabisa na familia yake.”

Zaidi ya kutia moyo familia yake kumtumikia Mungu, Luis alitenda yale aliyofundisha. Macarena anaeleza kwamba baba yake aliacha “biashara yenye mafanikio kwa kuwa ilichukua wakati wake mwingi, naye alitaka kutumia muda mwingi zaidi kushughulikia mambo ya familia.” Matokeo yalikuwa mazuri sana. Macarena anasema: “Mfano wake umenifundisha kuwa na jicho rahisi na kutanguliza mambo ya kiroho.” Sasa anatumikia akiwa painia, na mama yake na ndugu zake wadogo ni washiriki wenye bidii wa kutaniko la Kikristo.

Uamuzi wa Ofisa wa Reli

Bila shaka, watoto wanahitaji baba anayefanya maamuzi kwa kufikiria masilahi yao. Kijana wa Takeshi Tamura, yule ofisa Mjapani aliyetajwa katika makala iliyotangulia, alikuwa na marafiki wenye mwenendo mpotovu na alikuwa karibu kutumbukia katika matatizo makubwa. Hilo lilitukia mwaka wa 1986, mwaka ambao Takeshi aliamua kuacha cheo chake kikubwa katika Shirika la Reli la Japani. Takeshi anahisije sasa kuhusu uamuzi aliofanya miaka 18 iliyopita?

Hivi karibuni, alisema: “Labda huo ndio uamuzi bora zaidi ambao nimewahi kufanya. Kutumia wakati mwingi pamoja na mwanangu na kufanya mambo pamoja, kutia ndani kujifunza Biblia, kulikuwa na matokeo mazuri sana. Hilo lilituwezesha kuwa marafiki, naye alivunja uhusiano na marafiki zake wabaya na kuacha mwenendo usiofaa.”

Mke wa Takeshi alipata kuwa Shahidi wa Yehova miaka michache iliyotangulia, na mwenendo wake mzuri ndio uliomchochea mume wake kuichunguza Biblia na kujishughulisha zaidi na familia yake. Hatimaye Takeshi, mwana wake, na binti yake wakawa Mashahidi wa Yehova. Sasa, Takeshi na mwana wake ni wazee katika makutaniko wanayoshirikiana nayo, na mke wake na binti yake ni mapainia.

Akina Baba Wanahitaji Msaada

Ingawa baba wengi hutambua kwamba wanawapuuza watoto wao, hawajui la kufanya. Gazeti La Vanguardia la Hispania lilikuwa na kichwa hiki, “Asilimia 42 ya Wazazi [wa Hispania] Wanakubali Kwamba Hawajui Jinsi ya Kuwalea Vijana Wao.” Hilo ni kweli pia kuwahusu akina baba wenye watoto walio na umri wa chini ya miaka 13 na hata walio wachanga zaidi. Tofauti na maoni ya wengi, watoto hao pia wanahitaji baba anayetumia wakati pamoja nao na kuwahangaikia.

Ni mambo gani mengine ambayo akina baba wanaweza kujifunza ili wawe baba wazuri? Ni nani walio mifano bora kwa akina baba, na akina baba wanaweza kujifunza nini kutoka kwao? Makala yetu ya mwisho itashughulikia maswali hayo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Tafadhali ona sura yenye kichwa “Familia za Mzazi Mmoja Zaweza Kufanikiwa!” katika kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Akina baba waliowapa watoto wao kile wanachohitaji

Franciszek na familia yake

Luis na familia yake

Takeshi na familia yake