Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Maadili Yanazorota?

Je, Maadili Yanazorota?

Je, Maadili Yanazorota?

ZAWADI kubwa sana ambayo wazazi wanaweza kuwapatia watoto wao ni upendo wa kweli na maadili ambayo wanayafuata wala si kuyafundisha tu.

Bila maadili, maisha hayana maana. Maadili hufanya maisha yaridhishe. Yanafanya mtu ajue mambo yanayopasa kutangulizwa, yale anayopaswa kufanya na yale asiyopaswa kufanya.

Hata hivyo, maadili mengi ya kale yanabadilika haraka sana. Kwa mfano, Profesa Ronald Inglehart anasema kwamba “siku hizi jamii inaendelea kuwaruhusu watu watosheleze tamaa yao ya ngono jinsi wapendavyo na kuwapa uhuru wa kusema.” Katika mwaka wa 1997, kura ya maoni ya Gallup iliyohusisha nchi 16, iliwahoji watu kuhusu wanawake wanaopata watoto nje ya ndoa. Ripoti ya Gallup inasema: “Tabia hiyo inakubalika kwa kiwango cha kuanzia asilimia 90 au zaidi huko Ulaya Magharibi hadi chini ya asilimia 15 nchini Singapore na India.”

Watu wengine wameisifu tabia hiyo iliyopotoka. Hata hivyo, kitabu The Rise of Government and the Decline of Morality, cha James A. Dorn kinasema kwamba “ongezeko la watoto wanaozaliwa nje ya ndoa” na “kuvunjika kwa familia,” ni “mambo yanayoonyesha wazi kwamba maadili yamepotoka.”

Maadili Mengine Yanayozorota

Maadili mengine ambayo yamekuwapo kwa miaka mingi yanazorota pia. Uchunguzi wa Maadili Ulimwenguni, ulioongozwa na Profesa Inglehart, unaonyesha kwamba katika nchi zilizoendelea watu “wanazidi kudharau mamlaka.”

Tangu jadi watu wamekuwa na maadili ya kuwajibika kazini. Lakini kuna uthibitisho kwamba maadili hayo pia yanazorota. Huko Marekani, Shirika la Kitaifa la Wafanyabiashara wa Kujitegemea liliwachunguza waajiri zaidi ya nusu milioni. “Asilimia 31 walisema kwamba ni vigumu kujaza nafasi za kazi zilizo wazi, na asilimia 21 walisema kwamba kwa ujumla, kazi haifanywi vizuri.” Mwajiri mmoja alisema hivi: “Inaendelea kuwa vigumu kupata wafanyakazi ambao wanataka kufanya kazi kwa zaidi ya siku moja, wanaofika kazini bila kuchelewa, na ambao hawajalewa.”

Huenda hali hiyo inaletwa na sababu za kiuchumi. Faida ya biashara inapopungua, wafanyakazi wanafutwa au wanapunguziwa marupurupu fulani. Gazeti Ethics & Behavior linasema hivi: “Wafanyakazi wenye waajiri kama hao wasio waaminifu na wasiowajibika, huanza kuwa na maoni yasiyofaa kuwaelekea. Hawawezi kufanya kazi kwa bidii kwa sababu huenda kesho wakafutwa.”

Nidhamu na adabu ni mambo mengine ambayo yamezorota sana. Uchunguzi uliofanywa nchini Australia ulifikia mkataa huu: “Zaidi ya asilimia 87.7 ya wafanyakazi walisema [kwamba] utovu wa nidhamu unapunguza bidii kazini.” Wafanyabiashara mashuhuri nchini Marekani walipohojiwa, “asilimia themanini kati yao walisema kuna ongezeko la matusi katika biashara.” Kulingana na shirika la habari la CNN, “wateja wengi hawahudumiwi vizuri na karibu nusu ya wale waliohojiwa walisema kwamba iliwabidi waondoke dukani bila kununua chochote mwaka uliopita. Nusu yao walisema kwamba wao huwaona watu wakizungumza kwa simu ya mkononi kwa sauti kubwa au kwa njia yenye kuudhi. Pia madereva sita kati ya 10 walisema kwamba wao huwaona wengine wakiendesha gari bila kujali.”

Je, Uhai wa Mwanadamu Una Thamani?

Wakati mwingine, watu husema kwamba wanafuata “maadili” fulani, lakini hawatendi kulingana na maneno yao. Kwa mfano, Taasisi ya Maadili Duniani ilifanya kura ya maoni katika nchi 40. Asilimia 40 walisema “kuheshimu uhai” ni mojawapo ya maadili matano “yaliyo muhimu zaidi.” *

Lakini mambo yakoje kihalisi? Bila shaka mataifa yaliyoendelea yana uwezo wa kukomesha mateso mengi kati ya yale yanayowapata wanadamu. Lakini katika mwaka wa 1998, kitabu kilichoandikwa na Carol Bellamy, mkurugenzi mkuu wa Hazina ya Watoto ya Umoja wa Mataifa, kilisema kwamba utapiamlo “huchangia zaidi ya nusu ya vifo vya watoto wapatao milioni 12 wenye umri wa chini ya miaka mitano kila mwaka katika nchi zinazoendelea. Idadi hiyo ya vifo ni ya juu zaidi tangu tauni ilipotokea huko Ulaya katika karne ya 14.” Taarifa kama hizo humsikitisha mtu yeyote anayethamini uhai. “Lakini,” asema Bellamy, “janga la ulimwenguni pote la utapiamlo limewagutusha watu wachache sana, licha ya kuwa sayansi imepiga hatua kubwa kuonyesha kwamba ugonjwa huo ni hatari. Watu hukazia zaidi habari za kupanda na kushuka kwa bei katika soko la hisa ulimwenguni kuliko hatari kubwa ya utapiamlo, au kuliko umuhimu wa kuwapatia watu lishe bora.”

Vilevile inaonekana wazi kuwa wataalamu wa tiba wana maoni yasiyofaa kuhusu uhai. Katika mwaka wa 1970, watoto waliozaliwa baada ya kukaa tumboni mwa mama kwa majuma 23, hawakuwa na tumaini lolote la kupona. Leo, asilimia 40 ya watoto hao wanaweza kuokoka. Kwa hiyo, ni jambo la kusikitisha sana kwamba ulimwenguni pote vijusi milioni 40 hadi 60 hufa kutokana na utoaji wa mimba kila mwaka! Vijusi vingi hutolewa majuma machache tu kabla ya kufikia umri wa watoto wale ambao madaktari hujitahidi kuokoa! Je, jambo hilo halionyeshi kwamba maadili yamezorota sana?

Mwongozo wa Maadili Unahitajika

Watu walipoulizwa, “Ni kitu gani chenye umuhimu mdogo zaidi maishani?” katika kura ya maoni ya Gallup, wengi walisema moja kati ya mambo mawili yenye umuhimu mdogo sana ni ‘kuwa mwaminifu kwa dini yao.’ Basi si ajabu kwamba watu wanaoenda kanisani wanazidi kupungua. Profesa Inglehart anasema kwamba nchi za Magharibi “zinawafanya watu wahisi wakiwa salama sana” na kwamba jambo hilo “limepunguza uhitaji wa usalama waliopata katika dini zamani.”

Kadiri watu wanavyoacha dini, ndivyo wanavyoendelea kukosa imani katika Biblia. Katika uchunguzi mmoja wa kimataifa, watu waliulizwa walipata mwongozo kutoka kwa nani au kutoka wapi walipotaka kujua mambo yanayofaa au yasiyofaa. Wengi sana walisema walitegemea ujuzi wao maishani. “Ni wachache sana waliosema kwamba walitegemea neno la Mungu,” yasema ripoti ya uchunguzi huo.

Si ajabu basi kwamba maadili yanazidi kuzorota! Kukosa mwongozo wa maadili, kukazia utafutaji wa mali, na ubinafsi umeleta pupa na kutojali hisia za wengine. Matokeo yamekuwa nini?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 12 Zaidi ya miaka 50 iliyopita, Umoja wa Mataifa ulitangaza Azimio la Haki za Binadamu. Kifungu cha 1 cha Azimio hilo kinasema hivi: “Wanadamu wote huzaliwa wakiwa huru na wakiwa na cheo na haki sawa.”

[Picha katika ukurasa wa 4, 5]

Kuvunjika kwa familia, kutowajibika kazini, na utovu wa nidhamu ni mambo yanayoletwa na kuzorota kwa maadili

[Picha katika ukurasa wa 6]

Mamilioni ya vijusi vichanga kuliko kitoto hiki hutolewa kila mwaka