Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ushikamanifu ni kama nanga ambayo huifanya ndoa ibaki imara wakati wa misukosuko

KWA WENZI WA NDOA

1: Ushikamanifu

1: Ushikamanifu

MAANA YAKE

Waume na wake ambao wameazimia kushikamana na ndoa zao huuona muungano huo kuwa wa kudumu, na mtazamo huo hufanya wahisi wakiwa salama. Kila mmoja wao ana uhakika kwamba mwenzi wake hatamwacha hata hali ziwe ngumu.

Baadhi ya watu hubaki kwenye ndoa kwa kuwa wanahisi jamii au familia itawashangaa wakitalikiana. Hata hivyo, mnapaswa kuchochewa kushikamana na ndoa yenu kwa sababu mnapendana na kuheshimiana.

KANUNI YA BIBLIA: “Mume hapaswi kumwacha mke wake.”—1 Wakorintho 7:11.

“Ikiwa umeazimia kushikamana na ndoa yako, hutakuwa mwepesi wa kukasirika. Utakuwa mwepesi wa kusamehe na kuomba msamaha. Utaona matatizo kuwa changamoto za kawaida, na si msingi wa kuvunja ndoa.”—Micah.

KWA NINI NI MUHIMU

Matatizo yanapotokea, wenzi wa ndoa ambao hawajaazimia kushikamana na ndoa yao, hukimbilia kusema, ‘Inaonekana hatufaani.’ Kisha wanatafuta njia za kuachana.

“Watu wengi hufunga ndoa wakiwa na wazo la kwamba, ikiwa mambo hayataenda vizuri, watatalikiana. Mtu anapofunga ndoa akiwa na wazo la talaka, maana yake ni kwamba tangu mwanzo hajaazimia kushikamana na ndoa yake.”—Jean.

MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

JICHUNGUZE

Mnapokuwa mmekosana . . .

  • Je, wewe hujutia kufunga ndoa na mwenzi uliye naye?

  • Je, wewe hujiwazia ukiwa na mwenzi mwingine?

  • Je, wewe husema maneno kama vile “Ninakuacha” au “Nitatafuta mtu anayeona umuhimu wangu”?

Ikiwa umejibu ndiyo kwa lolote kati ya maswali hayo, huu ndio wakati wa kuimarisha azimio lako la kushikamana na ndoa yako.

ZUNGUMZA NA MWENZI WAKO

  • Je, kiwango cha ushikamanifu katika ndoa yetu kimeshuka? Ikiwa ndiyo, kwa nini?

  • Tufanye nini ili tuimarishe ushikamanifu katika ndoa yetu?

MAPENDEKEZO

  • Uwe ukimwandikia mwenzi wako ujumbe wa mapenzi bila yeye kutarajia

  • Onyesha umeazimia kushikamana na ndoa yako kwa kuweka picha za mwenzi wako mahali unapofanyia kazi

  • Mpigie simu mwenzi wako kila siku unapokuwa kazini au wakati haupo pamoja naye

KANUNI YA BIBLIA: “Kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.” —Mathayo 19:6.