Hosea 2:1-23
2 “Waambieni ndugu zenu, ‘Watu wangu!’+ na dada zenu, ‘Ee mwanamke uliyeonyeshwa rehema!’+
2 Fanyeni kesi na mama yenu;+ fanyeni kesi, kwa maana yeye si mke wangu+ nami si mume wake.+ Naye anapaswa kuondolea mbali uasherati wake kutoka mbele yake na matendo yake ya uzinzi kutoka katikati ya maziwa yake,+
3 ili nisimvue nguo awe uchi+ na kumtendea kama katika siku ya kuzaliwa kwake,+ na kwa kweli kumfanya kama nyika+ na kumfanya kama nchi isiyo na maji+ na kumuua kwa kiu.+
4 Nami sitawaonyesha wanawe rehema,+ kwa maana wao ni wana wa uasherati.+
5 Kwa maana mama yao amefanya uasherati.+ Yeye mwenye kuwachukua mimba ametenda kwa njia ya aibu,+ kwa maana amesema, ‘Nataka kuwafuata wale wanaonipenda kwa tamaa nyingi,+ wale wanaonipa mkate na maji, sufu na kitani, mafuta na kinywaji.’+
6 “Kwa sababu hiyo ninazungushia njia yako ukuta wa miiba; nami nitasimamisha ukuta wa mawe juu yake,+ ili asipate kuona barabara zake.+
7 Naye kwa kweli atawafuata wale wanaompenda kwa tamaa nyingi, lakini hatawafikia;+ naye hakika atawatafuta, lakini hatawapata. Naye atasema, ‘Nataka kwenda, nirudi kwa mume wangu,+ yule wa kwanza,+ kwa maana hali ilikuwa nzuri zaidi kwangu wakati huo kuliko ilivyo sasa.’+
8 Lakini yeye mwenyewe hakutambua+ kwamba mimi ndiye niliyempa nafaka+ na divai tamu na mafuta, na kwamba nilimfanya awe na fedha nyingi, na dhahabu, ambayo waliitumia kwa Baali.+
9 “ ‘Kwa sababu hiyo nitarudi na kuondolea mbali nafaka yangu wakati wake na divai yangu tamu katika majira yake,+ nami nitanyakua sufu yangu na kitani changu vinavyofunika uchi wake.+
10 Na sasa nitazifunua sehemu zake za siri zionekane na macho ya wale wanaompenda kwa tamaa nyingi,+ na hakuna mwanamume atakayemnyakua mkononi mwangu.+
11 Nami hakika nitakomesha furaha+ yake yote, sherehe+ yake, mwezi wake mpya+ na sabato yake na majira yake yote ya sherehe.
12 Nami nitaufanya kuwa ukiwa mzabibu+ wake na mtini+ wake, ambao amesema hivi kuuhusu: “Hizo ni zawadi zangu nilizopewa, ambazo wale wanaonipenda kwa tamaa nyingi wamenipa”; nami nitazifanya kuwa msitu,+ na mnyama wa mwituni atazila.
13 Nami nitamtoza hesabu+ kwa ajili ya siku za sanamu za Baali+ alizokuwa akifukizia moshi,+ wakati alipokuwa akijipamba kwa pete yake na pambo+ lake na kuwafuata wale wanaompenda kwa tamaa nyingi,+ naye alinisahau+ mimi,’ asema Yehova.
14 “ ‘Kwa sababu hiyo ninamshawishi mwanamke huyu, nami nitamfanya aende nyikani,+ na nitasema kwa kufikia moyo wake.+
15 Nami nitampa mashamba yake ya mizabibu kuanzia wakati huo+ na kuendelea, na nchi tambarare ya chini ya Akori+ kama lango la tumaini; naye hakika atajibu hapo kama katika siku za ujana wake+ na kama katika siku ya kutoka kwake katika nchi ya Misri.+
16 Na itakuwa katika siku hiyo,’ asema Yehova, ‘kwamba utaniita mimi Mume wangu, nawe hutaniita tena Mmiliki wangu.’+
17 “ ‘Nami nitaondoa majina ya sanamu za Baali kutoka katika kinywa chake,+ nazo hazitakumbukwa tena kwa majina yake.+
18 Na kwa ajili yao hakika nitafanya agano siku hiyo na mnyama wa mwituni+ na kiumbe kinachoruka cha mbinguni na kitu kinachotambaa cha nchi, nami nitavunja kutoka katika nchi upinde na upanga na vita,+ nami nitawafanya walale salama salimini.+
19 Nami nitakuchumbia mpaka wakati usio na kipimo,+ nitakuchumbia uwe wangu katika uadilifu na katika haki na katika fadhili zenye upendo na katika rehema.+
20 Nami nitakuchumbia uwe wangu katika uaminifu; nawe hakika utamjua Yehova.’+
21 “ ‘Na itakuwa katika siku hiyo kwamba mimi nitajibu,’ asema Yehova, ‘nitazijibu mbingu, mbingu nazo zitaijibu dunia;+
22 dunia nayo itaijibu nafaka+ na divai tamu na mafuta; vitu hivyo navyo vitajibu Yezreeli [‘Mungu atapanda mbegu’].+
23 Nami hakika nitampanda yeye duniani kama mbegu kwa ajili yangu,+ nami nitamwonyesha rehema yeye ambaye hakuonyeshwa rehema,+ nami nitawaambia wale ambao si watu wangu: “Ninyi ni watu wangu”;+ wao nao watasema: “Wewe ni Mungu wangu.” ’ ”+

