Hamia kwenye habari

SEPTEMBA 25, 2014
MAREKANI

Ripoti ya Makusanyiko ya Kimataifa: Mashahidi Wafanya Makusanyiko ya Kihistoria Kwenye Uwanja wa MetLife

Ripoti ya Makusanyiko ya Kimataifa: Mashahidi Wafanya Makusanyiko ya Kihistoria Kwenye Uwanja wa MetLife

NEW YORK—Juni 20-22 na Juni 27-29, 2014, Mashahidi wa Yehova walifurika kwenye Uwanja wa MetLife, East Rutherford, New Jersey, kwa ajili ya mfululizo wa Makusanyiko ya Kimataifa yenye kichwa “Endeleeni Kuutafuta Kwanza Ufalme wa Mungu!” yaliyofanywa katika Kiingereza na Kihispania.

Miisho-juma yote miwili ilikuwa na jumla ya wahudhuriaji zaidi ya 118,000. Muda mrefu sana umepita tangu Mashahidi wa Yehova walipokuwa na makusanyiko yenye idadi kubwa hivyo ya wahudhuriaji katika eneo la jiji la New York. Wahudhuriaji wengine zaidi ya 407,000 katika majiji mengine waliunganishwa kupitia video ili kusikiliza sehemu fulani za programu hiyo, na basi jumla ya wahudhuriaji ilikuwa zaidi ya 525,500.

Sehemu nyingi za programu hiyo zilikuwa na maonyesho na video zilizoonyesha jinsi ya kutumia vizuri kanuni za Biblia. Kila siku, makusanyiko hayo yalimalizika kwa hotuba zilizotolewa na washiriki wa Baraza Linaloongooza la Mashahidi wa Yehova. David Splane alikuwa msemaji kwenye makusanyiko yaliyofanywa Juni 20-22; na Geoffrey Jackson alikuwepo kwenye makusanyiko ya Juni 27-29.

Watu walibatizwa pia katika makusanyiko hayo. Watu 1,255 walibatizwa katika uwanja huo, na wengine 2,930 walibatizwa katika hayo maeneo mengine yaliyounganishwa kwa video, na hivyo jumla ya waliobatizwa ilikuwa watu 4,185.

Waliohudhuria walitia ndani wajumbe au wageni walioalikwa kutoka Argentina, Australia, Belize, Chile, Costa Rica, El Salvador, Guatemala, Hispania, Honduras, Italia, Malasia, Mexico, Nikaragua, Panama, Peru, Ugiriki, Uingereza, Ujerumani, na Venezuela.

J. R. Brown, msemaji wa Mashahidi wa Yehova alisema hivi: “Tukio hilo lilikumbusha wengi wetu kuhusu kusanyiko la kihistoria lililofanywa jijini New York katika mwaka wa 1958. Watu zaidi ya 253,000 walihudhuria tukio hilo katika Uwanja wa Yankee na wengine walisikiliza wakiwa kwenye ule uliokuwa Uwanja wa Polo. Bila shaka, makusanyiko yaliyofanywa kwenye Uwanja wa MetLife mwaka huu yatakumbukwa kati ya makusanyiko muhimu katika historia ya Mashahidi wa Yehova.”

Wanahabari Wanaweza Kuwasiliana na:

J. R. Brown, Ofisi ya Habari za Umma, simu +1 718 560 5000