Hamia kwenye habari

Ofisi mpya ya utafsiri ya lugha ya Wayuunaiki iliyo Riohacha, Kolombia, ambayo iliwekwa wakfu hivi karibuni

MEI 30, 2023
KOLOMBIA

Kuhamishwa kwa Ofisi ya Utafsiri ya Lugha ya Wayuunaiki Nchini Kolombia

Kuhamishwa kwa Ofisi ya Utafsiri ya Lugha ya Wayuunaiki Nchini Kolombia

Machi 18, 2023, ofisi mpya ya utafsiri (RTO) ya lugha ya Wayuunaiki iliyo Riohacha, Kolombia, iliwekwa wakfu. Lugha ya Wayuunaiki ndio lugha ya asili inayozungumzwa na watu wengi zaidi nchini Kolombia na Venezuela. Inazungumzwa na watu 700,000 hivi.

Hapo awali, watafsiri wa Wayuunaiki walifanya kazi katika nyumba mbili za kukodi ambazo hazikuwa na nafasi ya kutosha na umeme ulikatika-katika, isitoshe, huduma za simu na Intaneti hazikutegemeka. Ofisi ya tawi ya Kolombia ilinunua nyumba sita kwenye eneo la makazi na kuzirekebisha, na ofisi ya utafsiri ikahamishiwa hapo. Majengo hayo yanatumika yakiwa makao na pia ofisi kwa ajili ya watafsiri. Mradi huo uliidhinishwa Oktoba 2022 na kukamilishwa Januari 2023.

Ndugu Juan Felipe Rodríguez, mshiriki wa Idara ya Usanifu-Majengo na Ujenzi, alisema hivi kuhusu manufaa ya majengo hayo mpya: “Sasa tuna chumba kidogo cha kurekodia cha kisasa, nafasi ya kutosha kwa ajili ya watafsiri kufanya kazi pamoja, pia huduma za Intaneti ni bora zaidi, na kuna jenereta linalosaidia umeme unapokatika.”

Watafsiri watatu wa lugha ya Wayuunaiki wakifanya kazi kwenye ofisi mpya ya lugha ya utafsiri

Machapisho yanayotegemea Biblia yalianza kutafsiriwa katika lugha ya Wayuunaiki mwaka wa 1998. Kwa sasa, kuna ndugu na dada 14 wanaofanya kazi ya utafsiri. Kuna wahubiri 400 hivi katika makutaniko 20 ya lugha ya Wayuunaiki.

Tunapata shangwe nyingi tunapoona jinsi tengenezo la Yehova linavyoendelea kuwasaidia watu wa lugha zote ‘kumkaribia Mungu.’​—Yakobo 4:8.