Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Biblia na Wakati Wako Wenye Kuja

Biblia na Wakati Wako Wenye Kuja

WAZIA kwamba uko unatembea katika njia yenye giza wakati wa usiku. Hata kama jua limekwisha kushuka tangu zamani, hauone kuwa umepotea kabisa, kwa sababu katika mukono wako uko na torche yenye kuangaza sana. Wakati unaangaza chini mara moja unaona muzuri kila kitu chenye kuwa mbele yako. Na wakati unaangaza mbele yako, mwangaza wenye nguvu wa torche hiyo unafika mbali.

Katika njia fulani, Biblia iko kama vile torche hiyo. Kama vile tuliona katika habari zenye kutangulia, Neno la Mungu linaweza kutusaidia kupambana na matatizo yenye tunakutana nayo leo, ni kusema, magumu ya kila siku yenye sisi wote tunapambana nayo katika ulimwengu huu wenye kubadilika-badilika. Lakini Biblia inafanya mengi zaidi. Inatutolea mwangaza ili tuone muzuri zaidi wakati wenye kuja, ikitusaidia kuona na kufuata njia yenye itatusaidia tukuwe wenye kutosheka na kupata furaha ya milele. (Zaburi 119:105) Namna gani?

Tuchunguze njia mbili ambamo Biblia inatutolea tumaini lenye kufaa kwa ajili ya wakati wenye kuja: 1 Inatusaidia tukuwe na maisha yenye kusudi, na 2 inatufundisha namna tunaweza kuwa na urafiki wa milele pamoja na Muumbaji wetu.

1 MAISHA YENYE KUSUDI

Biblia inatoa mashauri yenye kutumainika yenye yanaweza kutusaidia kupambana na matatizo yetu. Hata hivyo Biblia inafanya mengi zaidi ya kuwa tu kitabu cha kutumia ili kujisaidia mwenyewe. Kuliko kututia moyo kukaza tu akili juu ya mahangaiko yetu wenyewe, Biblia inatufundisha tujione kuwa tuko na sehemu ya kutimiza katika kusudi kubwa la Mungu lenye linatia ndani mambo ya maana zaidi kuliko tu tamaa zetu wenyewe na mambo yenye tunahangaikia. Ni kwa kufanya hivyo tu ndio maisha yetu yanaweza kuwa kabisa na kusudi.

Kwa mufano, fikiria kanuni hii ya Biblia: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Unakumbuka wakati wenye ulisaidia mutu mwenye kuwa na lazima ya kitu fulani? Ao pengine wakati ulijitoa ili kusikiliza rafiki fulani wakati alikuwa anakuambia mambo yenye kuwa katika moyo wake? Je, ulijisikia kuwa mwenye furaha wakati ulitolea mutu mwingine kitulizo?

Tunapata furaha kubwa wakati tunapatia wengine bila kutumainia kuwa wataturudishia. Mwandikaji mumoja aliandika hivi: “Mara nyingi unapewa zawadi nyingi zaidi kupita zile zenye unatolea wengine, na hilo linafanyika wakati unatoa bila kuwa na wazo la kupata malipo.” Lakini, wakati tuko tayari kupatia wengine, zaidi sana wale wenye hawana namna ya kuturudishia kitu fulani, tunapata kabisa malipo. Kwa kufanya hivyo, tunatimiza sehemu fulani katika kusudi la Mungu. Kwa kweli tuko tunatumika bega kwa bega na Muumbaji mwenyewe, mwenye anaona matendo yetu ya wema kama vile ni deni lenye tumemukopesha. (Methali 19:17) Anaona mambo yenye tunafanya kwa ajili ya watu wa hali ya chini kuwa ya maana sana, na anaahidi kutulipa kwa kutupatia kitu fulani cha maana sana, ni kusema, uzima wa milele katika dunia paradiso​—hilo ni tumaini lenye kufurahisha sana kwa ajili ya wakati wenye kuja!​—Zaburi 37:29; Luka 14:12-14. *

Zaidi ya hilo, Biblia inatufundisha kwamba tunaweza kuwa na maisha yenye kusudi kwa kumuabudu Mungu wa kweli, Yehova. Anastahili tumusifu, tumuheshimie, na tumutii; na Neno lake linatutia moyo kufanya hivyo. (Mhubiri 12:13; Ufunuo 4:11) Wakati tunafanya hivyo, tunatimiza jambo fulani la maana sana: Tunafurahisha Muumbaji wetu. Kwa kweli, anatushauria hivi: ‘Ukuwe na hekima . . . na kuufanya moyo wangu ushangilie.’ (Methali 27:11) Fikiri kidogo; wakati tunakamata maamuzi yenye hekima yenye kutegemea kanuni za Biblia, tunafurahisha moyo wa Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo. Sababu gani? Kwa sababu anatuhangaikia na anapenda tupate faida kwa kufuata muongozo wake. (Isaya 48:17, 18) Kwa kweli, hakuna kusudi kubwa zaidi lenye tunaweza kuwa nalo kuliko kumutumikia Bwana mwenye mamlaka makubwa zaidi na kuishi katika njia yenye itamuletea furaha.

2 KUFANYA URAFIKI PAMOJA NA MUUMBAJI WETU

Biblia inatufundisha pia kufanya urafiki pamoja na Muumbaji wetu. Maandiko yanasema, ‘Mumukaribie Mungu, naye atawakaribia ninyi.’ (Yakobo 4:8) Wakati fulani tunaweza kuwa na mashaka na kujiuliza ikiwa inawezekana kabisa kufanya urafiki pamoja na Muumbaji mweza-yote. Lakini Biblia inatuhakikishia kwamba ikiwa ‘tunamutafuta Mungu, kwa kweli tutamupata,’ kwa sababu ‘hayuko mbali sana na kila mumoja wetu.’ (Matendo 17:27) Mashauri ya Biblia ya kuwa rafiki ya Mungu ni yenye kufaa sana kwa ajili ya wakati wetu wenye kuja. Namna gani?

Tufikirie jambo hili: Hata kama tunajikaza namna gani, hakuna hata mumoja kati yetu mwenye anaweza kuepuka adui wetu wa mwisho, ni kusema, kifo. (1 Wakorintho 15:26) Lakini, Mungu ni wa milele. Hakuna siku atakufa, na anapenda marafiki wake waishi pia milele. Biblia inatumia maneno haya mepesi lakini yenye kupendeza sana ili kuonyesha kile Yehova anapenda kwa ajili ya wale wenye wanamutafuta: “Mioyo yenu na iishi milele.”​—Zaburi 22:26.

Namna gani unaweza kufanya urafiki kama huo pamoja na Mungu? Endelea kujifunza kuhusu Mungu kupitia Neno lake, Biblia. (Yohana 17:3; 2 Timotheo 3:16) Umuombe akusaidie kuelewa Maandiko. Biblia inatuhakikishia kwamba ikiwa ‘tunaendelea kumuomba Mungu’ hekima kwa moyo wetu wote, yeye atatupatia sifa hiyo. * (Yakobo 1:5) Mwishowe, ujikaze kutumikisha mambo yenye unajifunza, kwa kuacha Neno la Mungu likuwe kama vile ‘taa ya muguu [wako]’ na “nuru kwa barabara [yako]”​—leo na milele.​—Zaburi 119:105.

^ fu. 8 Ili kupata habari zaidi juu ya ahadi ya Mungu ya uzima wa milele katika Paradiso, ona sura ya 3 ya kitabu Biblia Inafundisha Kabisa Nini? chenye kuchapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 13 Mashahidi wa Yehova wanajifunza na watu Biblia bila kuwaomba kitu chochote. Funzo hilo linaweza kukusaidia uongeze ujuzi wako wa Maandiko. Ili kujua mengi kuhusu namna wanajifunza Biblia na watu, tafazali uangalie video Tunajifunzaka Biblia na Watu Namna Gani? Unaweza kupata video kwenye www.jw.org.

Mungu ni wa milele, na anapenda marafiki wake waishi pia milele