Miaka Sabini ya Shule ya Gileadi

Miaka Sabini ya Shule ya Gileadi

Mnamo Februari 1, 1943, darasa la kwanza la shule ya pekee sana lilianzishwa katika sehemu ya kaskazini ya New York. Shule hiyo (sasa inajulikana kama Shule ya Gileadi), imewapa mafunzo maalumu wanaume na wanawake zaidi ya 8,000 kutoka nchi mbalimbali duniani.

Juu: Mlango wa mbele wa Shule ya Gileadi, South Lansing, New York. Chini: Mwalimu wa Gileadi akiwahutubia wanafunzi wa darasa la 31 wa shule ya Gileadi, ndani ya ukumbi

Jonathan, mhitimu wa darasa la hivi karibuni la Gileadi, anasema hivi: “Elimu tuliyopata, ambayo inategemea Neno la Mungu, itatusaidia tupate matokeo mazuri mahali popote na katika utamaduni wowote.” Marnie, mke wake, anaongezea hivi: “Sasa kuliko wakati mwingine wowote, ninatamani sana kuwasaidia watu ili waone kwamba hakuna njia ya maisha iliyo bora zaidi kuliko ile ambayo Muumba wetu anatupatia. Nina hakika kwamba kuwasaidia watu wamjue Yehova kutaboresha maisha yao.”

Masomo ya shule ya Gileadi hufundishwa bila malipo, nayo ni kozi ya miezi mitano. Mambo ya msingi yanayokaziwa zaidi katika shule hiyo ni Biblia na kazi ya kueneza injili. Kusudi la shule ya Gileadi ni kuwazoeza wahitimu ili hatimaye wawaimarishe na kuwajenga watu wa Mungu, na pia kuwasaidia wahitimu wakuze sifa za kiroho ambazo wanahitaji ili wakabiliane na hali ngumu zinazowakabili. Wakati wa kozi hiyo, wanafunzi wanazungumzia kanuni za Maandiko ambazo zinawasaidia waimarishe uhusiano mzuri na Mungu wao, Yehova.

Juu: Mwaka 1958 Albert Schroeder akiwafundisha wanafunzi wa Gileadi kwa kutumia mfano wa maskani. Chini: Mwaka 1968 Ulysses Glass akiwafundisha wanafunzi wa darasa la 46 la shule ya Gileadi

Wenzi wa ndoa wanaohudhuria Gileadi tayari wao ni wahudumu wa wakati wote. Baada ya kuhitimu, huenda wakarudi katika migawo yao au wakapewa mgawo wa kwenda nchi nyingine. Baadhi yao hupewa mgawo wa kutumikia katika mojawapo ya ofisi za tawi zaidi ya 90 za Mashahidi wa Yehova. Wengi wao hupewa mgawo wa kutumikia katika maeneo yenye watu wengi sana, mahali ambako wanaweza kupata matokeo mazuri zaidi katika kazi ya kuhubiri.

Tangu ilipoanzishwa Shule ya Gileadi ilikuwa kwenye eneo la Shamba la Ufalme, ambalo liko katika eneo la South Lansing, New York. Mnamo 1961, shule hiyo ilihamishwa na kupelekwa katika makao makuu ya Mashahidi wa Yehova ambayo yako Brooklyn, New York. Kuanzia mwaka 1988 hadi 1995, shule hiyo ilifanywa kwenye Shamba la Ufalme, ambalo liko Wallkill, New York. Hatimaye mwaka 1995, shule hiyo ikahamishwa na kupelekwa katika Kituo cha Elimu cha Watchtower, kilichopo Patterson, New York, hadi sasa shule ya Gileadi inafanywa katika kituo hicho. Mnamo Machi 2013, wanafunzi wa darasa la 134 walihitimu.

Juu: Mwaka 2003 wanafunzi wanasoma ndani ya maktaba ya Gileadi. Chini: Mwaka 2011 wanafunzi wa darasa la 116 wa shule ya Gileadi wakiwa darasani

Kwa miaka 70 sasa, wahitimu wa Shule ya Gileadi wameweka mfano mzuri sana wa kuigwa kwa kutoa ushahidi kwa uaminifu kuhusu Yehova.