Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 IGENI IMANI YAO

“Ijapokuwa Alikufa, Bado Anasema”

“Ijapokuwa Alikufa, Bado Anasema”

ABELI alitazama kundi lake la kondoo likilisha kwa amani kwenye mteremko wa kilima. Kisha, labda alitazama kutoka mahali ambapo kondoo walikuwa na kwa mbali akaona mwali wa moto. Alijua kwamba mahali hapo palikuwa na upanga unaowaka moto uliokuwa ukizunguka-zunguka, na hivyo kufunga njia ya kuingia kwenye bustani ya Edeni. Wakati fulani wazazi wake waliishi huko, lakini sasa wao na wazao wao hawakuruhusiwa kuingia katika bustani hiyo. Wazia upepo wa alasiri ukipuliza nywele za Abeli alipotazama juu na kumfikiria Muumba wake. Je, uhusiano mzuri kati ya Mungu na wanadamu ungerudishwa? Abeli alitaka uhusiano huo urudishwe.

Abeli anazungumza nawe leo. Je, unamsikia? Huenda ukasema jambo kama hilo haliwezekani. Kwa sababu mwana huyo wa pili wa Adamu alikufa zamani za kale. Mabaki ya mwili wake yalioza na kuchanganyika na udongo kwa karibu miaka 6,000. Biblia inatufundisha kwamba wafu: “Hawajui lolote kamwe.” (Mhubiri 9:5, 10) Vilevile, Abeli hakusema neno hata moja ambalo limeandikwa katika Biblia. Basi, anawezaje kuzungumza nasi?

Mtume Paulo aliongozwa na roho ya Mungu kusema hivi kumhusu Abeli: “Kupitia hiyo yeye, ijapokuwa alikufa, bado anasema.” (Waebrania 11:4) Abeli anazungumza kupitia nini? Ni kupitia imani. Abeli alikuwa mwanadamu wa kwanza kusitawisha sifa hiyo yenye kupendeza. Alionyesha imani kwa njia bora sana hivi kwamba mfano wake unaendelea kuishi, ukiwa kiwango imara ambacho tunaweza kuiga leo. Ikiwa tutaiga imani yake na kujitahidi kuifuata, basi mfano wa Abeli utazungumza nasi waziwazi na kwa njia iliyo halisi kabisa.

Hata hivyo, tunaweza kujifunza nini kutokana na Abeli na imani yake kwa sababu Biblia inasema machache sana kumhusu? Acheni tuone.

MAISHA YA UTOTONI MWANZONI MWA ULIMWENGU

Abeli alizaliwa mwanzoni mwa historia ya wanadamu. Baadaye, Yesu alimhusianisha Abeli na “kuwekwa msingi wa ulimwengu.” (Luka 11:50, 51) Inaonekana Yesu alimaanisha ulimwengu wa watu walio na tumaini la kukombolewa kutoka katika dhambi. Ingawa Abeli alikuwa mtu wa nne kuishi duniani, inaonekana ndiye mtu wa kwanza ambaye Mungu aliona kuwa anaweza kukombolewa. * Ni wazi kwamba Abeli hakulelewa kati ya watu wenye uvutano mzuri.

Ingawa wanadamu hawakuwa wameishi kwa muda mrefu, walikabili hali yenye kuhuzunisha sana. Yaelekea wazazi wa Abeli, Adamu na Hawa, walikuwa watu wenye sura na umbo zuri. Lakini walikuwa wamefanya makosa makubwa sana maishani, na walijua hivyo. Wakati fulani walikuwa wakamilifu, wakiwa na tumaini la kuishi milele. Kisha wakamwasi Yehova Mungu na akawafukuza kutoka kwenye makao yao ya Paradiso katika bustani ya Edeni. Kwa kutanguliza tamaa zao bila kujali watu  wengine, kutia ndani hali ya wazao wao, walipoteza ukamilifu na uzima wa milele.—Mwanzo 2:15–3:24.

Walipofukuzwa kutoka kwenye bustani, Adamu na Hawa walikabili maisha magumu. Hata hivyo, mwana wao wa kwanza alipozaliwa, walimwita Kaini, au “Kitu Kilichotokezwa,” na Hawa akasema hivi: “Nimezaa mwanamume kwa msaada wa Yehova.” Huenda maneno yake yanaonyesha kwamba alikumbuka ahadi ambayo Yehova alitoa katika bustani, alipotabiri kwamba mwanamke fulani angetokeza “uzao” ambao siku moja ungemwangamiza yule mwovu ambaye aliwapotosha Adamu na Hawa. (Mwanzo 3:15; 4:1) Je, Hawa aliwazia kwamba alikuwa mwanamke aliyetabiriwa na kwamba Kaini ndiye ule “uzao” ulioahidiwa?

Ikiwa ndivyo, alikuwa amekosea sana. Zaidi ya hayo, ikiwa yeye na Adamu walimwambia Kaini mambo kama hayo alipokuwa mvulana, kwa kweli walimfanya awe na kiburi. Baada ya muda, Hawa alizaa mwana wa pili, lakini hatusomi maneno ya kumsifu. Walimwita Abeli, jina linalomaanisha “Pumzi,” au “Ubatili.” (Mwanzo 4:2) Je, jina hilo linamaanisha kwamba hawakutazamia mengi kutoka kwake, kana kwamba walikuwa na matumaini mengi zaidi katika Kaini kuliko Abeli? Labda walifikiri hivyo.

Vyovyote vile, leo wazazi wanaweza kujifunza mengi kutoka kwa wazazi hao wa kwanza. Kupitia maneno na matendo yenu, je, mtafanya watoto wenu wawe na mwelekeo wa kiburi, kujitakia makuu, na ubinafsi? Au, mtawafundisha kumpenda Yehova Mungu na kusitawisha urafiki pamoja naye? Inasikitisha kwamba wazazi wa kwanza walishindwa kutimiza wajibu wao. Hata hivyo, wazao wao walikuwa na tumaini.

ABELI ALISITAWISHAJE IMANI?

Wavulana hao walipoendelea kukua, inaelekea Adamu aliwazoeza kufanya kazi ambayo ingesaidia familia kupata mahitaji. Kaini alifanya kazi ya ukulima, naye Abeli akafanya kazi ya kuchunga wanyama.

Hata hivyo, Abeli alifanya jambo muhimu zaidi. Kwa miaka mingi, alisitawisha imani, ile sifa muhimu ambayo baadaye Paulo aliandika kuihusu. Hebu fikiria. Abeli hangemwiga mwanadamu yeyote. Basi, alisitawishaje imani katika Yehova Mungu? Hebu ona mambo matatu ambayo huenda yalimsaidia kusitawisha imani yenye nguvu.

Uumbaji wa Yehova.

Ni kweli kwamba Yehova alikuwa amelaani udongo, na hivyo kuufanya utokeze miiba na mibaruti ambayo iliathiri kilimo. Lakini bado dunia ilitokeza kwa wingi chakula ambacho kilisaidia familia ya Abeli iendelee kuishi. Na wanyama hawakuwa wamelaaniwa, kutia ndani ndege na samaki; wala milima, maziwa, mito, na bahari; wala mbingu, mawingu, jua, mwezi, na nyota. Kila mahali alipotazama, Abeli aliona upendo mwingi, hekima, na wema wa Yehova Mungu, ambaye alikuwa ameumba vitu vyote. (Waroma 1:20) Imani yake iliimarishwa alipotafakari kwa uthamini kuhusu vitu hivyo.

Bila shaka, Abeli alitenga wakati wa kufikiria mambo ya kiroho. Mwazie akichunga wanyama wake. Mchungaji alihitaji kutembea sana. Aliwaongoza wanyama kwenye vilima, mabonde, kuvuka mito, kila mara akitafuta majani mabichi zaidi, chemchemi  bora za kunywesha wanyama, na mahali salama zaidi pa kupumzikia. Kati ya viumbe wote wa Mungu, inaonekana kondoo ndio waliohitaji kuchungwa, kana kwamba waliumbwa wakiwa na uhitaji wa kuongozwa na kulindwa na mwanadamu. Je, Abeli aliona kwamba yeye pia alihitaji mwongozo, ulinzi, na utunzaji kutoka kwa Mtu mwenye hekima na uwezo zaidi kuliko wanadamu? Bila shaka, alitaja mambo kama hayo katika sala, na hivyo imani yake ikaendelea kukua.

Kwa kutazama uumbaji, Abeli alipata msingi wa kuwa na imani thabiti katika Muumba

Ahadi za Yehova.

Ni lazima iwe kwamba Adamu na Hawa waliwasimulia wana wao kuhusu matukio katika shamba la Edeni ambayo yalifanya wafukuzwe. Hivyo, Abeli alikuwa na mambo mengi ya kutafakari.

Yehova alisema kwamba udongo ungelaaniwa. Abeli aliona waziwazi miiba na mibaruti ambayo ilitimiza laana hiyo. Yehova alitabiri pia kwamba Hawa angechukua mimba na kuzaa kwa uchungu. Bila shaka, Abeli alijua kwamba maneno hayo yalitimia ndugu na dada zake wadogo walipokuwa wakizaliwa. Yehova alitambua kimbele kwamba Hawa angetamani kupita kiasi kupendwa na kutunzwa na mumewe, na hivyo kutawaliwa naye. Abeli alijionea jambo hilo likitukia. Katika mambo yote hayo, Abeli aliona kwamba maneno ya Yehova yanategemeka kabisa. Hivyo, Abeli alikuwa na msingi thabiti wa kuamini ahadi ya Mungu kuhusu “uzao” ambao siku moja ungerekebisha makosa yaliyoanzia huko Edeni.—Mwanzo 3:15-19.

Watumishi wa Yehova.

Abeli hakuwa na mfano mzuri wa kuiga katika familia ya kibinadamu, lakini mbali na wanadamu, wakati huo kulikuwa pia na viumbe wengine wenye akili duniani. Adamu na Hawa walipofukuzwa kwenye bustani, Yehova alihakikisha kwamba wao pamoja na wazao wao hawangeingia kwenye Paradiso hiyo iliyokuwa duniani. Ili kulinda mwingilio wa bustani hiyo, Yehova aliweka makerubi, yaani, malaika wenye cheo cha juu, pamoja na upanga unaowaka ulioendelea kuzunguka-zunguka.—Mwanzo 3:24.

Wazia Abeli akiwaona makerubi hao alipokuwa mvulana. Wakiwa na miili ya kibinadamu, bila shaka walikuwa wenye nguvu sana. Vilevile, ule “upanga” uliokuwa ukiwaka, na kuendelea kuzunguka, ulikuwa wenye kutisha. Abeli alipoendelea kukua, je, aliona makerubi hao wakichoka na kuondoka mahali hapo? Hapana. Usiku na mchana, mwaka baada ya mwaka, viumbe hao wenye akili na nguvu nyingi waliendelea kusimama mahali hapo. Hivyo, Abeli akajifunza kwamba Yehova Mungu ana watumishi waadilifu, na waaminifu. Kwa kutazama makerubi hao, Abeli aliona ushikamanifu na utii kwa Yehova ambao hakuona katika familia yake. Bila shaka, mfano huo wa malaika uliimarisha imani yake.

Katika maisha yake yote, Abeli aliona kwamba makerubi walikuwa watumishi wa Yehova waaminifu na watiifu

Kwa kutafakari kuhusu mambo yote ambayo Yehova alikuwa amefunua kujihusu kupitia uumbaji, ahadi zake, na mifano ya watumishi wake, imani ya Abeli iliendelea kuimarika. Bila shaka, tunaweza kujifunza mengi sana kutokana na mfano wake. Vijana hasa wanajifunza kwamba wanaweza kusitawisha imani ya kweli katika Yehova Mungu, hata washiriki wa familia yao wasipokuwa washikamanifu. Leo, tukiwa tumezungukwa na maajabu ya uumbaji, na Biblia nzima, vilevile mifano mingi ya wanadamu wenye imani, tuna msingi mzuri wa kutusaidia kujenga imani.

KWA NINI DHABIHU YA ABELI ILIKUWA BORA SANA?

Imani ya Abeli katika Yehova ilipoendelea kukua, alitamani kuionyesha kwa matendo. Lakini, mwanadamu wa kawaida angempa nini Muumba wa ulimwengu mzima? Kwa kweli, Mungu hakuhitaji zawadi au msaada wowote kutoka kwa wanadamu. Baada ya muda, Abeli alielewa ukweli huu muhimu: Ikiwa angemtolea Yehova kitu bora zaidi alichokuwa nacho, kwa mtazamo unaofaa, Baba yake wa mbinguni mwenye upendo angekubali.

Hivyo, Abeli akajitayarisha kutoa kondoo kutoka katika kundi lake. Alichagua walio bora zaidi, yaani, wazaliwa wa kwanza, na akatoa vipande alivyoona kuwa bora kabisa. Wakati uleule, Kaini pia alitafuta baraka na kibali cha Yehova, hivyo akatayarisha toleo kutoka kwa mimea yake. Lakini alikuwa na nia tofauti na ya Abeli. Tofauti hiyo ilionekana wazi ndugu hao walipoleta matoleo yao.

Abeli alitoa dhabihu yake kwa imani; Kaini hakufanya hivyo

 Wana hao wawili wa Adamu walitumia madhabahu na moto kutoa matoleo yao, labda mbele ya makerubi, ambao wakati huo ndio tu waliokuwa wawakilishi walio hai wa Yehova duniani. Yehova alijibu! Tunasoma: “Yehova alikuwa akimtazama Abeli na toleo lake kwa kibali.” (Mwanzo 4:4) Simulizi hilo halisemi jinsi Mungu alivyoonyesha kibali chake. Lakini kwa nini alikubali toleo la Abeli?

Je, alipendezwa na toleo hilo? Abeli alimtoa kiumbe aliye hai anayepumua, na akamwaga damu, yaani, uhai wenye thamani wa kiumbe huyo. Je, Abeli alitambua thamani ya dhabihu kama hiyo? Karne nyingi baada ya wakati wa Abeli, Mungu alitumia dhabihu ya kondoo asiye na kasoro kuwakilisha dhabihu ya Mwana wake mkamilifu, “Mwana-Kondoo wa Mungu,” ambaye damu yake isiyo na hatia ingemwagwa. (Yohana 1:29; Kutoka 12:5-7) Hata hivyo, Abeli hakujua wala kuelewa mambo hayo yote.

Jambo tunalojua kwa hakika ni hili: Abeli alitoa kitu bora zaidi kati ya vitu alivyokuwa navyo. Yehova alimtazama kwa kibali mwanamume huyo na pia toleo lake. Abeli alitenda kwa kuchochewa na upendo na imani ya kweli katika Yehova.

Mambo yalikuwa tofauti kwa Kaini. Yehova “hakumtazama Kaini na toleo lake kwa kibali chochote.” (Mwanzo 4:5) Si kwamba toleo la Kaini lilikuwa na kasoro, kwa sababu baadaye Sheria ya Mungu iliruhusu matoleo ya mazao ya shambani. (Mambo ya Walawi 6:14, 15) Lakini kumhusu Kaini Biblia inasema “matendo yake mwenyewe yalikuwa maovu.” (1 Yohana 3:12) Kama watu wengi leo, Kaini alidhani kujionyesha tu kwamba amejitoa kwa Mungu kwa nje kulitosha. Baada ya muda mfupi, ilionekana wazi kupitia matendo yake kwamba hakuwa na imani ya kweli wala hakumpenda Yehova.

Kaini alipoona kwamba hakupata kibali cha Yehova, je, alijaribu kujifunza kutokana na mfano wa Abeli? Hapana. Alipandwa na hasira kumwelekea ndugu yake. Yehova aliona kilichokuwa moyoni mwa Kaini na akazungumza naye kwa subira. Alimwonya Kaini kwamba mtazamo wake ungemwingiza kwenye dhambi nzito, na akamwambia kuwa ‘angeinuliwa’ ikiwa angebadili njia zake.—Mwanzo 4:6, 7.

Kaini alipuuza onyo la Mungu. Badala yake, alimwomba ndugu yake mdogo asiye na hatia waende shambani. Walipokuwa huko, Kaini akampiga Abeli na kumuua. (Mwanzo 4:8) Hivyo, kwa njia fulani Abeli akawa mtu wa kwanza kuteswa kwa ajili ya dini, mtu wa kwanza kufia imani. Alikufa, lakini hadithi yake haikuisha.

Kwa njia ya mfano, damu ya Abeli ilimlilia Yehova Mungu ili atekeleze haki au kulipiza kisasi. Na Mungu alihakikisha kwamba haki ilitekelezwa, alipomwadhibu Kaini kwa sababu ya uovu wake. (Mwanzo 4:9-12) Jambo muhimu zaidi ni kwamba simulizi kuhusu imani ya Abeli linazungumza nasi leo. Maisha yake—labda miaka mia moja hivi—yalikuwa mafupi kwa wanadamu wakati huo, lakini Abeli aliyatumia vizuri. Alikufa akijua kwamba alipendwa na alikuwa na kibali cha Baba yake wa mbinguni, Yehova. (Waebrania 11:4) Hivyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba yuko salama katika kumbukumbu la Yehova lisilo na mipaka, akingojea kufufuliwa katika paradiso duniani. (Yohana 5:28, 29) Je, utakutana naye huko? Unaweza ikiwa utaazimia kumsikiliza Abeli anapozungumza na uige imani yake yenye nguvu. ▪

^ fu. 8 Maneno “kuwekwa msingi wa ulimwengu” yanahusiana na wazo la kupanda mbegu, yakimaanisha kuzaa, hivyo yanahusiana na mzao wa kwanza kabisa wa wanadamu. Hata hivyo, kwa nini Yesu alihusianisha Abeli na “kuwekwa msingi wa ulimwengu” na si Kaini, ambaye alikuwa mwanadamu wa kwanza kuzaliwa? Maamuzi na matendo ya Kaini yalitokeza uasi wa kimakusudi dhidi ya Yehova Mungu. Kama tu wazazi wake, inawezekana kwamba Kaini hana tumaini la kukombolewa na kufufuliwa.