MEI 12, 2025
URENO
Kwa miaka 100, Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakiwasadia watu nchini Ureno kujifunza kuhusu Neno la Mungu
Mashahidi wa Yehova Watimiza Miaka 100 ya Kuwafundisha Watu Biblia Nchini Ureno
Tangazo katika gazeti la habari la Mei 1925 likiwaalika watu wahudhurie hotuba ya Ndugu Rutherford jijini Lisbon
Mwanzoni mwa 1925, Ndugu George Young aliwasili nchini Ureno na akaanza kuhubiri ujumbe wa Biblia. Ilikuwa mara ya kwanza kwa watu wengi nchini humo kusikia habari njema. Kisha, Mei 13, mwaka huohuo, Ndugu J. F. Rutherford akatoa hotuba ya Biblia yenye kichwa “Jinsi ya Kuishi Duniani Milele.” Hotuba ya Ndugu Rutherford ilitangazwa kwenye magazeti ya habari ya eneo hilo na watu 2,000 hivi wakakusanyika kwenye ukumbi wa Shule ya Sekondari ya Luís de Camões jijini Lisbon ili kusikiliza hotuba yake. Watu walikuwa wengi sana, hivi kwamba, watu wengine 2,000 hivi hawakukubaliwa kuingia kwa sababu ukumbi huo ulikuwa tayari umejaa. Hotuba hiyo iliwachochea wengi kupendezwa na kweli za Biblia na kuanza kumtumikia Yehova. Baadaye mwaka huo, toleo la kwanza la gazeti la Mnara wa Mlinzi la Kireno (cha Ureno) lilichapishwa, na ofisi ya tawi ikaanzishwa jijini Lisbon. Hata hivyo, ndugu zetu wangekabili hali ngumu.
Mwaka wa 1926, serikali mpya ya kidikteta ilianza kutawala nchini Ureno. Serikali hiyo ilipinga tena na tena jitihada za ofisi ya tawi za kupata usajili wa kisheria ambao ungewawezesha kuendeleza kazi ya kuhubiri na kufundisha. Hata hivyo, ndugu na dada zetu waliendelea kuhubiri habari njema kwa ujasiri. Kwa kusikitisha, hali zilizorota mwezi Machi 1961. Kufuatia vuguvugu la kisiasa lililotokea Angola, ambayo ilikuwa koloni ya Ureno wakati huo, ndugu zetu vijana nchini Ureno walianza kuteswa vikali kwa sababu ya msimamo wao wa kutounga mkono upande wowote. Wengi wao walikamatwa na kutendewa vibaya kwa kukataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri. Ndugu David Mota, aliyekabili hali ngumu alipokuwa gerezani kwa sababu ya kukataa kujiunga na jeshi, anasema hivi: “Licha ya kwamba niliteswa isivyo haki kwa sababu ya imani yangu, kuwa sehemu ya tengenezo la Yehova kumeniwezesha kuwa na maisha yenye furaha na kusudi.”
Hatimaye, katika mwaka wa 1974, serikali ya Ureno iliwasajili kisheria Mashahidi wa Yehova, na hilo liliwawezesha ndugu zetu kuwa na uhuru mkubwa zaidi wa kuhubiri ujumbe wa Biblia. Kisha, Juni 22, 2009, serikali hiyo iliwapatia Mashahidi wa Yehova hadhi ya juu kabisa ya kisheria inayopewa dini ambazo zimekuwepo kwa muda mrefu. Ndugu Carlos Reixa, mwenye umri wa miaka 75, alipokuwa akitafakari kuhusu matukio nchini humo, alisema hivi: “Inapendeza sana kuona jinsi ambavyo kazi ya kuhubiri imekuwa na matokeo mazuri nchini Ureno. Mwaka wa 1961, kulikuwa na wahubiri 1,000 hivi nchini. Leo, kuna zaidi ya wahubiri 57,000!”
Wahubiri wawili kati ya 57,000 walio nchini Ureno wakihubiri habari njema
Tunaweza kusema kwa uhakika kwamba, Yehova amewatunza ndugu na dada zetu nchini Ureno kwa miaka hiyo 100 iliyopita. Hilo linathibitisha kwamba hakuna chochote kinachoweza kumzuia ‘kufanya mahali pa hema lake pawe na nafasi kubwa zaidi.’—Isaya 54:2.