SEPTEMBA 26, 2025
NEW CALEDONIA
Dada kutoka New Caledonia wakiwa wameshika machapisho ya lugha za asili (kushoto kwenda kulia) Kidrehu, Kiwalisi, Kinengone, na Kifaransa
Miaka Hamsini ya Kutambuliwa Kisheria Katika Visiwa vya New Caledonia
Septemba 2025 inatimiza miaka 50 tangu Mashahidi wa Yehova waliposajiliwa kisheria katika visiwa vya New Caledonia. Akina ndugu waliwasilisha maombi ya kusajiliwa kisheria mara mbili lakini maombi hayo yalikataliwa. Hatimaye, walifurahi sana waliposajiliwa rasmi Septemba 19, 1975.
Habari njema zilifika kwenye visiwa hivi kwa mara ya kwanza zaidi ya miaka 90 iliyopita. Katika miaka ya 1930, kikundi kidogo cha Mashahidi kilisafiri kwenye visiwa hivi na kusambaza machapisho yanayotegemea Biblia. Miaka ishirini hivi baadaye, ndugu na dada kutoka Australia walihamia kwenye visiwa hivi. Walipoanza kuhubiri, walipata watu wengi ambao walikuwa tayari kujifunza Biblia. Agosti 1956, kutaniko la kwanza lilianzishwa jijini Nouméa.
Ndugu John Hubler na mke wake, Ellen, walipokuwa wakitumikia New Caledonia
Katika mwaka wa 1959, serikali ilikataa ghafla kuwapa wageni viza mpya na hivyo ndugu na dada kutoka Australia walilazimika kurudi nyumbani. Mwaka uliofuata, serikali ilipiga marufuku machapisho yetu yote. Ndugu John Hubler anasema hivi: “Ndugu wenyeji walituambia makasisi walitangaza katika makanisa yao kwamba ‘viongozi’ wa Mashahidi wa Yehova wameondoka na hivyo Mashahidi wenyeji wangerudi kanisani hivi karibuni.”
Ndugu Jean-Pierre Francine, mmoja wa Mashahidi wa kwanza kubatizwa katika nchi hiyo alisema hivi: “Ingawa ndugu na dada zetu wapendwa kutoka Australia walilazimika kuondoka, kikundi kidogo cha wahubiri 15 kilichokuwa katika eneo letu kiliendelea kuhubiri. Machapisho yetu yalikuwa yamepigwa marufuku na hilo lingeweza kutufanya tupunguze bidii yetu, lakini Yehova alitutegemeza. Tulihubiri kwa kutumia Biblia tu. Hata hivyo kikundi chetu kidogo kiliendelea kukua.”
Novemba 1962, marufuku dhidi ya machapisho yetu iliondolewa, lakini magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! yaliendelea kuwa chini ya marufuku. Hatimaye, magazeti hayo yaliondolewa marufuku pia. Tulisajiliwa kisheria Septemba 1975, na mwezi mmoja baadaye, tulipata wahitimu wa Gileadi kwa mara ya kwanza katika visiwa vya New Caledonia. Wahitimu hao walikuwa Marc na Paulina Fosset. Juni 1976, ofisi ya tawi ilifunguliwa jijini Nouméa. Muda mfupi baadaye, Jumba la kwanza la Ufalme la Mashahidi wa Yehova lilijengwa jijini humo.
Kwa zaidi ya miaka 50, ndugu na dada zetu katika visiwa vya New Caledonia wamekuwa wakihubiri habari njema kwa bidii. Leo, kuna wahubiri 2,700 wanaotumikia katika eneo la ofisi ya tawi. Inapendeza kwamba watu 7,833 walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo mwaka wa 2024. Idadi hiyo inazidi idadi ya wahubiri karibu mara tatu.
Washiriki wa familia ya Betheli ya New Caledonia, Septemba 2025. Picha ndogo: Ofisi ya tawi ya sasa iliyopo Nouméa
Tunashangilia kwamba Yehova anaendelea kubariki kazi katika visiwa vya New Caledonia. Miaka 50 imepita tangu ndugu na dada zetu walipopata usajili wa kisheria na bado ‘wanatamani kutangaza habari njema.’—Waroma 1:15.

