Je, Jina Lako Linaandikwa Katika “Kitabu cha Kumbukumbu” cha Mungu?

Je, Jina Lako Linaandikwa Katika “Kitabu cha Kumbukumbu” cha Mungu?

Umukaribie Mungu

Je, Jina Lako Linaandikwa Katika “Kitabu cha Kumbukumbu” cha Mungu?

JE, YEHOVA anaona bidii ambayo waabudu wake wanafanya ili kumupendeza? Ndiyo, anaona! Lakini anaona zaidi ya matendo yao ya kumuogopa na maneno yao ya kumusifu. Anatambua hata wakati wanapofikiri mambo mazuri juu ya yake. Na jambo la lazima zaidi ni kwamba Yehova hatasahau hata kidogo watu wake na mambo wanayofanya. Ni nini kinatuhakikishia jambo hilo? Jibu linapatikana katika maneno ya nabii Malaki.​—Soma Malaki 3:16.

Malaki alipotabiri katika miaka ya 400 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, mwenendo wa watu na hali za kidini katika Israeli zilikuwa mbaya sana. Makuhani walipuuza kazi zao, na watu kwa ujumla wakaanza kufanya matendo yanayomukosea Mungu heshima, kama vile uchawi, uzinifu, na udanganyifu. (Malaki 2:8; 3:5) Hata hivyo, ijapokuwa matendo hayo maovu, Waisraeli wengi walibaki waaminifu. Ni nini kiliwasaidia kubaki waaminifu?

Malaki alieleza hivi: ‘Wale waliomuogopa Yehova walisemezana, kila mumoja na mwenzake.’ Kumuogopa Mungu ni sifa nzuri. Katika andiko hilo, Malaki anazungumuza juu ya Waisraeli waliomuheshimu sana Mungu na kuogopa kufanya mambo yasiyomupendeza. Ona kwamba watu hao waliomuogopa Mungu ‘walisemezana kila mumoja na mwenzake.’ Ni wazi kwamba walikutana pamoja ili kusema mambo mazuri juu ya Yehova na kutiana moyo, na hilo liliwasaidia wasivunjike moyo na kuambukizwa na matendo mabaya ya Waisraeli wengine.

Waisraeli hao waaminifu walimuonyesha Yehova heshima katika njia nyingine ya maana: Walikuwa ‘wanalifikiria jina lake.’ Tafsiri nyingine inasema “waliheshimu jina Lake.” Waisraeli hao waliomuogopa Mungu walimuheshimu hata katika mawazo yao. Katika mioyo yao, walikuwa wanatafakari ao kufikiri sana mambo mazuri juu ya Yehova na jina lake kubwa. Je, Yehova aliona mambo hayo waliyokuwa wanafanya?

Malaki anasema hivi: “Yehova akaendelea kutoa uangalifu na kusikiliza.” Kutoka makao yake ya juu sana huko mbinguni, Yehova alitega sikio lake na kusikiliza kila neno la kumusifu ambalo waabudu wake walisemezana kila mumoja na mwenzake. Pia, aliwasikiliza kwa uangalifu walipotafakari juu yake kwa siri. (Zaburi 94:11) Lakini, zaidi ya kukazia tu uangalifu maneno na mawazo yao mazuri, alifanya mambo mengine.

Malaki anasema hivi: “Kitabu cha kumbukumbu kikaanza kuandikwa mbele zake.” Kitabu hicho ni kumbukumbu la Mungu juu ya wale wote ambao wamemutumikia kwa uaminifu. Ona kwamba kitabu hicho kinaitwa “kitabu cha kumbukumbu.” * Hilo linatuonyesha kama Yehova hatasahau hata kidogo waabudu wake waaminifu na yote ambayo wamefanya ili kumusifu, ni kusema kila tendo, neno, na wazo lao njema. Lakini kuna sababu inayomufanya Mungu awakumbuke. Anaahidi kuwapa uzima wa milele wale wote ambao majina yao yameandikwa kwa kudumu katika kitabu chake cha kumbukumbu. *​—Zaburi 37:29.

Ni jambo lenye kufariji sana kujua kama Yehova anapendezwa na mambo yote tunayofanya ili kumuabudu kwa njia inayokubalika. Maneno ya Malaki 3:16 yanapaswa kutufanya tufikiri kwa uzito juu ya urafiki wetu pamoja na Yehova. Ni vizuri kila mutu ajiulize, ‘Je, jina langu linaandikwa katika “kitabu cha kumbukumbu” cha Mungu?’ Jina la kila mumoja wetu litaandikwa ikiwa tunafanya yote tunayoweza ili kutenda, kusema, na kufikiri kila siku kwa njia ambayo itamufanya Yehova atukumbuke.

Tafazali, mwezi huu wa 12, soma Maandiko haya katika Biblia:

Nahumu sura ya 1-3 mupaka Malaki sura ya 1-4

[Maelezo ya chini]

^ Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “kumbukumbu” linamaanisha mengi zaidi ya kukumbuka tu kitu fulani. Linaweza pia kumaanisha kufanya jambo fulani kwa ajili ya kitu ambacho mutu anakumbuka.

^ Ili kujua mengi zaidi juu ya ahadi ya Mungu ya uzima wa milele, soma sura ya 3 ya kitabu Biblia Inafundisha Kabisa Nini? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.