Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Yesu alitembelea mama-mukwe wa Petro na akamuponyesha.—Mathayo 8:14, 15; Marko 1:29-31

Viongozi wa Dini za Kikristo Wanapaswa Kubaki Bila Kufunga Ndoa?

Viongozi wa Dini za Kikristo Wanapaswa Kubaki Bila Kufunga Ndoa?

DINI nyingi katika dunia, kama vile Kanisa Katoliki, makanisa ya Kiortodoksi, ya Kibuda, na makanisa mengine yanaomba viongozi wa dini zao wabaki waseja, ni kusema wabaki bila kufunga ndoa. Lakini, wengine wanawaza kwamba hiyo ndiyo sababu kubwa yenye kufanya viongozi wa dini mbalimbali wahusike katika matendo mabaya ya ngono ya hivi karibuni.

Kwa hiyo, ni muzuri kujiuliza hivi: Maandiko yanaomba viongozi wa dini za Kikristo wabaki bila kufunga ndoa? Ili kujibia ulizo hilo, tuchunguze kwanza chanzo na historia ya desturi hiyo na tuone pia mawazo ya Mungu juu ya jambo hilo.

KUBAKI BILA KUFUNGA NDOA KATIKA HISTORIA YA DINI

Kulingana na kitabu kimoja, useja ni “hali ya kubaki bila kufunga ndoa, na kwa hiyo, kujiepusha kabisa na ngono, mara nyingi kuhusu viongozi wa dini ao watawa.” (Encyclopædia Britannica) Katika Baraza la Usimamizi la Kanisa Katoliki la mwaka wa 2006, Papa Benoît wa 16 alionyesha kwamba kulazimishwa kubaki bila kufunga ndoa ni “desturi yenye ilianza katika miaka ya karibu na wakati wa Mitume.”

Hata hivyo, Wakristo wa mbele ya mwaka wa 100 hawakukuwa na desturi ya kubaki bila kufunga ndoa. Mutume Paulo mwenye aliishi mbele ya mwaka wa 100 alionya hata waamini kuhusu watu wenye walikuwa wanasema “maneno yaliyoongozwa kwa roho yenye kupotosha” na “wakikataza kufunga ndoa.”—1 Timotheo 4:1-3.

Ni katika kipindi cha kati ya mwaka wa 101 na 200 ndiyo desturi ya kubaki bila kufunga ndoa ilianza kuingia katika makanisa ya “Kikristo” ya Mangaribi. Kulingana na kitabu kimoja, hilo “lilipatana na desturi mupya kuhusu kujizuia kufanya ngono yenye ilitokea katika Utawala wa Roma.”—Celibacy and Religious Traditions.

Katika miaka yenye ilifuata, mikutano ya wakubwa wa dini na wenye kuitwa Mababa wa Kanisa walieneza desturi ya kwamba viongozi wa dini wanapaswa kubaki bila kufunga ndoa. Walifikiri kwamba ngono ilichafua madaraka ya viongozi wa dini na haikupatana na madaraka yao. Hata hivyo, Encyclopædia Britannica inaonyesha kwamba “kufikia mwaka wa 1000, mapadri wengi na hata maaskofu fulani walikuwa na bibi.”

Desturi ya mapadri kubaki bila kufunga ndoa ilikubaliwa waziwazi katika Mabaraza ya Kilateri yenye ilifanywa Roma katika mwaka wa 1123 na 1139, na desturi hiyo imeendelea kukubaliwa na Kanisa Katoliki la Roma mupaka leo. Kupitia mupango huo, kanisa lilizuia kupoteza mamlaka na mali kwa sababu mapadri wenye walikuwa wamefunga ndoa walikuwa wanaachia watoto wao mali ya kanisa.

MAWAZO YA MUNGU JUU YA KUBAKI BILA KUFUNGA NDOA

Mawazo ya Mungu juu ya kubaki bila kufunga ndoa yanaonyeshwa waziwazi katika Neno lake Biblia. Katika Biblia, tunasoma maneno ya Yesu juu ya wale wenye walibaki bila kufunga ndoa kama yeye, “kwa sababu ya Ufalme wa mbinguni.” (Mathayo 19:12) Pia mutume Paulo alizungumuza kuhusu Wakristo wenye waliamua kufuata mufano wake wa kubaki bila kufunga ndoa “kwa ajili ya habari njema.”—1 Wakorintho 7:37, 38; 9:23.

Lakini, Yesu na Paulo hawakuamuru Wakristo wenye kuongoza wabaki bila kufunga ndoa. Yesu alisema kama kubaki bila kufunga ndoa ilikuwa “zawadi,” lakini haiko wanafunzi wake wote ndio walikuwa na zawadi hiyo. Wakati Paulo aliandika juu ya “mabikira [ao, wale wenye walibaki bila kufunga ndoa],” alikubali hivi waziwazi: “Sina amri kutoka kwa Bwana, lakini natoa maoni yangu.”—Mathayo 19:11; 1 Wakorintho 7:25.

Tena, Biblia inaonyesha kama Wakristo wenye walikuwa wanaongoza wakati wa mitume, kutia ndani mutume Petro, walikuwa wanaume wenye kufunga ndoa. (Mathayo 8:14; Marko 1:29-31; 1 Wakorintho 9:5) Kwa sababu matendo ya uasherati yalikuwa yameenea katika utawala wa Roma wakati huo, Paulo aliandika kwamba ikiwa mwangalizi Mukristo alikuwa amefunga ndoa, alipaswa kuwa ‘mume wa muke mumoja’ na “mwenye watoto wanaojitiisha.”—1 Timotheo 3:2, 4.

Ndoa hizo hazikukuwa ndoa za kubaki bila kufanya ngono, kwa sababu Biblia inasema waziwazi kwamba ‘mume [anapaswa] kumupa muke wake haki yake’ na kwamba bibi na bwana hawapaswe ‘kunyimana haki’ ya kitendo cha ndoa. (1 Wakorintho 7:3-5) Kwa kweli, Mungu haombe watu wabaki bila kufunga ndoa, wala halazimishe Wakristo wenye kuongoza wabaki bila kufunga ndoa.

KWA AJILI YA HABARI NJEMA

Ikiwa hakuna amri yenye kulazimisha watu wabaki bila kufunga ndoa, sababu gani Yesu na Paulo walisifu hali hiyo? Kwa sababu kubaki bila kufunga ndoa kunaweza kutolea mutu nafasi nyingi za kutangazia wengine habari njema. Watu wenye hawajafunga ndoa wanaweza kujitoa ili kufanya mengi zaidi kwa sababu hawana mahangaiko yenye wale wenye wamefunga ndoa wanapata.​—1 Wakorintho 7:32-35.

Fikiria mufano wa David, mwenye aliamua kuacha kazi yake yenye alikuwa analipwa feza nyingi katika muji wa Mexico na kuhamia katika eneo la kijiji katika Costa Rica ili kufundisha wengine Biblia. David anaona kwamba aliweza kufanya hivyo kwa sababu hakuwa amefunga ndoa? Anasema hivi: “Ndiyo kabisa. Ilikuwa vigumu kuzoea desturi mupya na hali tofauti ya maisha, lakini kwa sababu sikukuwa na mutu mwengine wa kuhangaikia, ilikuwa mwepesi zaidi kuzoea.”

Claudia, Mukristo mwenye hajafunga ndoa alihamia katika eneo lenye kuwa na lazima ya wahubiri. Anasema hivi: “Ninafurahia utumishi wangu kwa Mungu. Imani yangu na urafiki wangu pamoja na Mungu unatiwa nguvu wakati ninaona namna ananihangaikia.”

“Iwe umefunga ndoa ao hapana, utakuwa mwenye furaha ikiwa unamutumikia Yehova Mungu kwa uwezo wako wote.”—Claudia

Kubaki bila kufunga ndoa hakupaswe kuwa muzigo. Claudia anaongezea hivi: “Iwe umefunga ndoa ao hapana, utakuwa mwenye furaha ikiwa unamutumikia Yehova Mungu kwa uwezo wako wote.”—Zaburi 119:1, 2.