Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Namna Neno la Mungu Lilivyosaidia Familia Moja Yenye Bidii Katika Dini ya Kihindu

Namna Neno la Mungu Lilivyosaidia Familia Moja Yenye Bidii Katika Dini ya Kihindu

Namna Neno la Mungu Lilivyosaidia Familia Moja Yenye Bidii Katika Dini ya Kihindu

Nalini Govindsamy anaeleza maisha yake

SITASAHAU hata kidogo chakula cha asubuhi tulichochangia na familia yangu tulipokusanyika pamoja Siku ya Kwanza, tarehe 22 Mwezi wa 8, 2005. Nilikuwa na kivimba kwenye ubongo, kwa hiyo maisha yangu yalikuwa katika hatari. Bwana yangu Krishna, alitoa sala, na kisha nikazungumuza na familia yangu.

Niliwaambia hivi: “Ninaenda kwenye hopitali kwa ajili ya upasuaji ulio hatari; kwa hiyo, munapaswa kujitayarisha kwa jambo lolote linaloweza kutokea. Nimekwisha kufanya mipango kwa ajili ya maziko yangu, ikiwa nitakufa. Ninyi ambao ni waabudu wa Yehova, tafazali, musiache kumuabudu. Na ninyi ambao hamujaanza kumuabudu Yehova, ninawasihi mukubali kujifunza Biblia na muanze kuhuzuria mikutano. Mukifanya hivyo, tunaweza kuonana tena katika ulimwengu mupya unaokaribia ambamo waabudu wa kweli wa Mungu wataishi milele wakiwa na afya kamilifu katika dunia itakayokuwa paradiso.”

Mbele ya kueleza namna upasuaji huo ulivyofanyika, acheni niwaeleze maisha yangu na namna nilivyopata kumujua Mungu wa kweli.

Nilikomalia Katika Familia Yenye Bidii Katika Dini ya Kihindu

Familia yangu iliishi katika nyumba ya mbao na manjanja, iliyojengwa kwenye mulima katika muji wa Durban uliokuwa pembeni ya bahari, huko Afrique du Sud. Ili kufika kwenye mulango wa mbele wa nyumba yetu, kwanza tulipaswa kupanda vidaraja (escaliers) 125 kutoka kwenye barabara kubwa iliyokuwa katika bonde. Kisha kupanda vidaraja hivyo, tulifika kwenye njia fupi iliyokuwa katika miti iliyotuongoza kwenye mulango wa chuma. Hekalu la tate (nkambo) mwanamuke lilikuwa kwenye upande mwengine wa mulango, na lilijaa sanamu na picha za miungu ya Kihindu. Tate aliniambia kama nilikuwa “mutoto wa hekalu” (mandir kī baccā, katika luga ya Kihindi) na kama nilizaliwa kwa sababu ya miungu tuliyoabudu. Upande mwengine wa hekalu kulikuwa vidaraja vyekundu vilivyojengwa vizuri ambavyo viliongoza moja kwa moja kwenye mulango wa mbele wa nyumba. Nyumba yetu ilikuwa kubwa: ilikuwa na njia kubwa katikati, chumba cha kupigia chakula kilichokuwa na jiko kubwa la makaa, vyumba saba vya kulala, na chumba kingine kimoja cha kulala kilichokuwa pembeni. Tulikuwa watu 27 katika vyumba hivyo, ni kusema tate mwanaume na tate mwanamuke, baba yangu, wadogo wake watatu, dada yake mudogo, na familia zao.

Haikuwa vyepesi kushugulikia familia kubwa kama hiyo. Lakini kuishi pamoja kulifanya familia iungane na tulipitisha pamoja nyakati nyingi zenye kufurahisha. Mama yangu, Gargee Devi, na shemeki (demai) zake watatu ndio walioshugulikia kazi za nyumbani. Kila mumoja wao alikuwa na siku yake ya kusafisha nyumba na kupiga chakula. Tate mwanaume ndiye alikuwa anaongoza mambo ya jamaa na kununua chakula kwa ajili ya jamaa nzima. Kila Siku ya Tatu, tate mwanaume na tate mwanamuke walienda sokoni ili kununua nyama, matunda na mboga za majani kwa ajili ya juma nzima. Tulizoea kuwagonjea kwenye kilima chini ya kivuli cha muti wa aina ya musidano (cyprès) tukiangalia kwenye barabara iliyokuwa katika bonde. Mara tu tulipowaona wakishuka katika motokari pamoja na mizigo yao, tulishuka haraka vile vidaraja 125 ili kuwasaidia kupeleka vitu nyumbani.

Katika bustani yetu, tulikuwa na muti murefu wa ngazi, ambako ndege nyeusi zinazoiga sauti za watu kama kasuku zilikuwa zimejenga nyumba zao. Tuliziona zikiruka-ruka na kufanya makelele. Tate mwanamuke alikuwa anakaa kwenye vidaraja mbele ya nyumba na kutuelezea habari, ni kama vile alikuwa anafasiria sauti za ndege. Ninaendelea kukumbuka mambo mengi mazuri tuliyochangia katika nyumba hiyo! Tulicheka, tulilalamika kwa furaha, tulicheza, tulionyesha sura ya kicheko, tulichangia vitu vingi​—tulifurahia kuishi pamoja katika familia moja kubwa. Na jambo la lazima zaidi, tulianza kujifunza juu ya Muumbaji wetu, Yehova, na juu ya Mwana wake Yesu Kristo katika familia hiyo.

Mbele ya kumujua Yehova, tulizoea kufanya desturi nyingi za ibada yetu ya Kihindu kila siku. Tena, tulikuwa tunafanya sikukuu kwa ukawaida. Wakati wa sikukuu hizo, tulialika wageni ili waje tuabudu miungu yetu pamoja. Kwenye sikukuu fulani, tate mwanamuke alikuwa anazungumuza na roho waovu, na katikati ya usiku alikuwa anatolea roho hao sadaka za wanyama ili kuwatuliza. Tate mwanaume alikuwa mwenye kujulikana sana katika eneo letu kwa sababu alikuwa anatoa misaada ya kujenga hekalu za dini ya Kihindu na masomo.

Namna Tulivyojua Ukweli juu ya Yehova

Katika mwaka wa 1972, tate mwanaume aligonjwa na akakufa. Miezi michache kisha hapo, Indervathey, aliyeitwa pia Jane, bibi ya mumoja wa baba zangu wadogo, alikubali magazeti Munara wa Mulinzi na Amkeni! ambayo Mashahidi wa Yehova wawili walimutolea. Alihuzunika sana kwa sababu hakuwakaribisha nyumbani ili kuzungumuza nao. Kila mara, tulikuwa tunawafukuza Mashahidi wa Yehova. Lakini, wakati walitutembelea tena, aliwakaribisha nyumbani na akazungumuza nao juu ya tatizo la ndoa alilokuwa nalo kwa sababu bwana yake alikuwa mulevi. Majirani na watu wa jamaa walimushauria avunje ndoa yake. Mashahidi wa Yehova walimufasiria mawazo ya Mungu juu ya ndoa. (Mathayo 19:6) Alifurahia sana mashauri na ahadi ya Biblia juu ya maisha mazuri yatakayokuwa hapa duniani wakati ujao. * Alibadilisha mawazo aliyokuwa nayo ya kuvunja ndoa yake, na akaanza kujifunza Biblia kwa ukawaida na Mashahidi wa Yehova. Alipokuwa anajifunza nao katika salon ya nyumba yetu, shemeki zake walikuwa wanasikiliza mazungumuzo hayo katika vyumba vyao.

Mwishowe, bibi za baba zangu wadogo wakaanza kujifunza wote Biblia. Jane alikuwa anaelezea wengine mambo aliyokuwa anajifunza na mara nyingi alitusomea na kutufasiria hadisi fulani za kitabu Kumsikiliza Mwalimu Mkuu. * Baba zangu wadogo walipojua kama bibi zao walikuwa wanajifunza Biblia, wakaanza kutupinga. Mumoja wa baba zangu wadogo alichukua vichapo vyetu vyote, na hata Biblia, na kuviunguza. Tulipohuzuria mikutano, baba zangu wadogo walitutukana na kutupiga. Baba yangu tu ndiye hakutupinga; yeye hakutukataza kujifunza juu ya Yehova. Mama yangu na shemeki zake watatu waliendelea kukusanyika na kumupenda Yehova Mungu zaidi.

Katika mwaka wa 1974, Jane alibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova, mama yangu na shemeki zake wengine walibatizwa baadaye. Kisha wakati fulani, tate mwanamuke akaacha desturi zake za dini ya Kihindu. Niliendelea kuhuzuria mikutano kwa miaka mingi. Kisha, kwenye mukusanyiko mukubwa wa Mashahidi wa Yehova, Shahidi anayeitwa Shameela Rampersad, aliniuliza, “Utabatizwa wakati gani?” Nikamujibu, “Siwezi kubatizwa kwa sababu hakuna mutu ambaye amekwisha kunifundisha Biblia.” Akasema kama atafurahi kunifundisha Biblia. Nilibatizwa kwenye mukusanyiko uliofuata, tarehe 16 Mwezi wa 12, 1977. Mwishowe, kati ya watu 27 wa jamaa yetu walioishi pamoja, watu 18 wakabatizwa. Lakini, nilipopasuliwa, baba yangu, Sonny Deva, alikuwa angali katika dini ya Kihindu.

‘Musihangaike juu ya Kitu Chochote’

Maneno ya andiko la Wafilipi 4:6, 7 yamenisaidia sana, zaidi sana wakati niliambiwa kama nina kivimba kwenye ubongo. Andiko hilo linasema hivi: ‘Musihangaike juu ya kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukurani maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.’ Ni vigumu kutohangaika “juu ya kitu chochote,” zaidi sana wakati unaambiwa kama uko katika hatari ya kufa. Nilipoambiwa hivyo, kwanza nililia na kisha nikasali kwa Yehova. Kuanzia wakati huo na kuendelea, nimepata ‘amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote.’

Yehova alishika mukono wangu wa kuume, na nilijisikia kama vile aliniongoza katika njia yangu yote. (Isaya 41:13) Alinisaidia kuwafasiria waganga bila woga kama siwezi kuvunja amri ya Biblia ya kujiepusha na damu. (Matendo 15:28, 29) Kwa hiyo, muganga aliyenipasua na yule aliyenitoboa dawa ya kunifanya nisisikie maumivu wakati wa upasuaji walikubali kunipasua bila kunitia damu. Kisha hapo, muganga aliyenipasua alieleza kama upasuaji ulifanyika bila tatizo na kama kivimba chote kiliondolewa. Pia, alisema kwamba hajaona mugonjwa mwengine anapona haraka kisha upasuaji mukubwa wa ubongo.

Majuma matatu kisha upasuaji, niliongoza funzo la kwanza nikiwa kwenye kitanda nyumbani. Mwishoni mwa juma la saba kisha upasuaji wangu, nilianza kutembeza tena motokari, kuenda kwenye mahubiri, na kuhuzuria mikutano. Nilifurahia sana musaada ambao ndugu na dada walinitolea kwa kuendelea kuhubiri pamoja nami. Hakuna siku waliniacha niende peke yangu katika mahubiri na walikuwa wananisindikiza mupaka nyumbani kisha mahubiri. Niko hakika kama kusikiliza usomaji wa Biblia uliorekodiwa na kuendelea kufanya kazi za kiroho ndilo jambo lililonisaidia nipone haraka.

Tena, nilipokuwa kwenye hopitali, nilifurahi kusikia kama baba yangu alikubali kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Alibatizwa alipokuwa na miaka 73, na sasa anamutumikia Yehova kwa bidii. Sasa, zaidi ya watu 40 wa jamaa yangu wamekuwa Mashahidi wa Yehova. Hata ikiwa jicho langu la kushoto halione tena vizuri, na mufupa wa kichwa changu unaofunika ubongo umeshonwa na vyuma, ninangojea kwa hamu wakati ambapo Yehova atafanya “vitu vyote kuwa vipya” katika Paradiso itakayokuwa duniani wakati ujao.​—Ufunuo 21:3-5.

Nimepata baraka nyingi: bwana mwenye upendo, aliye muzee katika kutaniko, na binti mwenye sura nzuri anayeitwa Clerista ambaye ananitegemeza sana katika utumishi wa wakati wote. Yehova Mungu amebariki sana kazi yangu. Mupaka sasa, nimewasaidia watu wengi ambao nimejifunza nao Biblia wajionee nguvu ya Neno la Mungu katika maisha yao. Sasa, zaidi ya watu 30 kati yao wamejitoa kwa Yehova na kubatizwa.

Kwa moyo wenye kujaa tumaini, ninangojea wakati ambapo Yehova Mungu atatuondolea taabu za dunia hii na kuifanya dunia iwe paradiso.

[Maelezo ya chini]

^ Ili kupata habari zingine juu ya kusudi la Mungu kwa dunia, usome sura ya 3 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ Kilichapishwa na Mashahidi wa Yehova lakini hakichapishwe tena.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Mama ananibeba

[Picha katika ukurasa wa 10]

Nyumba ya jamaa yetu

[Picha katika ukurasa wa 10]

Karibu na vile vidaraja 125

[Picha katika ukurasa wa 11]

Bwana yangu, mimi, mutoto wetu mwanamuke, na wazazi wangu