Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Je, Ulijua?

Je, Ulijua?

Je, Ulijua?

Je, kuna mambo yanayoonyesha kama Wakristo walikimbia inchi ya Yudea mbele ya uharibifu wa Yerusalemu mwaka wa 70?

‘Mutakapoona Yerusalemu limezingirwa na majeshi yaliyopiga kambi, ndipo jueni kwamba kufanywa ukiwa kwake kumekaribia. Ndipo wale walio katika Yudea waanze kukimbilia milimani, na wale walio katikati yake na waondoke.’ (Luka 21:20, 21) Hayo ni maagizo ambayo Yesu aliwapatia wanafunzi wake kuhusu uharibifu ambao ungekuja juu ya muji wa Yerusalemu. Je, kuna mambo yanayoonyesha kama wanafunzi walitii onyo la Yesu?

Miaka mingi kisha Yesu kufa, jeshi la Waroma lililoongozwa na Cestius Gallus liliingia Palestina ili kumaliza uasi. Mwanahistoria Muyahudi Josèphe aliyeishi wakati huo, alihakikisha jambo hilo. Jeshi hilo lilizunguka muji wa Yerusalemu na lilikuwa tayari kuukamata. Bila kutazamia, Gallus akaagiza jeshi lake liondoke. Eusèbe, mwanahistoria wa mambo ya dini, anaeleza kama Wakristo wa Yudea walichukua nafasi hiyo ili kukimbilia muji wa Pela uliokuwa kwenye milima katika eneo la Dekapoli.

Miaka michache baadaye, katika mwaka wa 70, jeshi lingine la Waroma, lililoongozwa na Jenerali Titus, lilizunguka muji wa Yerusalemu na kuuharibu kabisa; jambo ambalo jeshi la Gallus halikufanya. Watu wengi sana walinaswa katika Yerusalemu na kuuawa.

Ni nani waliokuwa “wana wa manabii”?

Habari zilizo katika Biblia juu ya nabii Samweli, Eliya, na Elisha zinazungumuzia watu walioitwa “wana wa manabii.” Kwa mufano, Elisha alimutuma ‘mumoja wa wana wa manabii’ amutie Yehu mafuta ili kumufanya awe mufalme wa Israeli.​—2 Wafalme 9:1-4.

Watu wanaofasiria Biblia wanawaza kama maneno “wana wa manabii” yanaleta wazo la masomo ya maagizo ao kikundi cha watu wanaoishi na kutumika pamoja, lakini hayamaanishe watoto wa manabii. Gazeti moja (Journal of Biblical Literature) linasema kama, labda washiriki wa vikundi hivyo walikuwa watu “waliojitoa kwa ajili ya utumishi wa Yahweh [Yehova] na waliongozwa na nabii ambaye alikuwa . . . baba yao wa kiroho.” (2 Wafalme 2:12) Biblia inaonyesha kama, ili kumutia Yehu mafuta, Elisha alituma ‘mutumishi wa nabii.’​—2 Wafalme 9:4.

“Wana wa manabii” waliishi maisha mepesi. Biblia inaonyesha kama wakati wa Elisha kikundi kimoja cha wana wa manabii waliotafuta kujenga makao yao walitumia shoka ya kuazima. (2 Wafalme 6:1-5) Inaonekana kama watu fulani katika vikundi hivyo walikuwa wenye kuoa, kwa sababu Biblia inazungumuzia mujane fulani “wa wana wa manabii.” (2 Wafalme 4:1) Ni wazi kama Waisraeli waaminifu walipendezwa na wana wa manabii kwa sababu Biblia inaonyesha kama waliwatolea zawadi ya chakula wakati fulani.​—2 Wafalme 4:38, 42.