Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Ni Nini Kitakachozipata Dini?

Ni Nini Kitakachozipata Dini?

Jifunze Kutoka Katika Neno la Mungu

Ni Nini Kitakachozipata Dini?

Makala hii inazungumzia maswali ambayo huenda umejiuliza na inakuonyesha mahali unapoweza kupata majibu katika Biblia yako. Mashahidi wa Yehova watafurahi kuzungumzia majibu hayo pamoja nawe.

1. Je, dini zote ni nzuri?

Vikundi vingi vya kidini vina watu wanyoofu ambao wanataka kumpendeza Mungu. Anawaona watu hao na anawajali. Hata hivyo, jambo la kusikitisha ni kwamba watu fulani wametumia dini kwa makusudi mabaya. Zamani, viongozi wa kidini hata walikuwa wakiwatesa watu waliowapinga. (2 Wakorintho 4:3, 4; 11:13-15) Kulingana na ripoti za vyombo vya habari leo, viongozi fulani wa kidini wamechochea ugaidi au wameunga mkono vita, au hata wamewatendea watoto vibaya kingono.​—Soma Mathayo 24:3-5, 11, 12.

Biblia inafundisha kwamba kuna aina mbili za dini—dini ya kweli na dini ya uwongo. Dini ya uwongo haifundishi ukweli kumhusu Mungu. Hata hivyo, Yehova Mungu anataka watu wajue ukweli kumhusu.​—Soma 1 Timotheo 2:3-5.

2. Ni nini kitakachozipata dini?

Mungu hataki watu wadanganywe na dini zinazodai kwamba zinampenda lakini hazifundishi ukweli kumhusu. Kwa kweli, wafuasi wa dini hizo wanapenda kufanya urafiki na ulimwengu unaoongozwa na Shetani Ibilisi. (Yakobo 4:4; 1 Yohana 5:19) Neno la Mungu linasema kwamba dini zinazounga mkono serikali za wanadamu badala ya Mungu ni kama kahaba. Biblia inamwita kahaba huyo “Babiloni Mkubwa,” jina linalotokana na jiji la kale ambako dini ya uwongo ilianzishwa baada ya Gharika ya siku za Noa. Hivi karibuni, Mungu ataharibu ghafula dini zote zinazofundisha uwongo na kuwakandamiza wanadamu.​—Soma Ufunuo 17:1, 2, 5, 17; 18:8, 23, 24.

3. Mungu ataletaje shangwe duniani kote?

Bila shaka, hukumu inayokuja dhidi ya dini ya uwongo ni habari njema. Hukumu hiyo italeta kitulizo kwa kuondoa ukandamizaji ulimwenguni pote. Dini za uwongo hazitawapotosha wala kuwatenganisha wanadamu tena. Wanadamu wote wanaoishi wataungana katika ibada ya Mungu wa pekee wa kweli.​—Soma Isaya 11:9; Ufunuo 18:20, 21; 21:3, 4.

4. Watu wanyoofu wanapaswa kufanya nini?

Yehova hajawasahau watu wanyoofu ambao wametawanyika katika dini za uwongo ulimwenguni pote. Anawakusanya watu hao na kuwaunganisha kwa kuwafundisha ukweli.​—Soma Mika 4:2, 5.

Yehova anawakaribisha kwenye familia yake wale wanaotaka kumtumikia. Tunapata faida kubwa tunapoanza kumtumikia Yehova, hata ikiwa rafiki zetu na watu wa ukoo wanakasirika. Tunafaidika kwa kuwa rafiki za Mungu, pia tunakuwa sehemu ya “familia” mpya na yenye upendo, na tunakuwa na tumaini la kupata uzima wa milele.​—Soma Marko 10:29, 30; 2 Wakorintho 6:17, 18.

Kwa habari zaidi, ona sura ya 15 na ya 16 ya kitabu hiki, Biblia Inafundisha Nini Hasa?, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 16]

The Complete Encyclopedia of Illustration/J. G. Heck