Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

KICHWA

Kanuni za Mwenendo Zinazofanya Maisha Yawe Mazuri Kabisa

Kanuni za Mwenendo Zinazofanya Maisha Yawe Mazuri Kabisa

Christina alishituka sana! Alikuwa ametoka tu kuokota mukoba mweusi uliokuwa na feza nyingi sana, feza hizo zilikuwa zenye kulingana na mushahara wake wa miaka zaidi ya 20! Na alijua mutu aliyepoteza feza hizo. Wewe ungefanya nini? Halafu Christina angefanya nini? Jibu lako litaonyesha maoni yako juu ya kufuatia haki na ikiwa unashikamana na kanuni hiyo ya mwenendo.

Kanuni za mwenendo ni nini? Ni kanuni ambazo tunaona kuwa nzuri na za maana. Kanuni hizo zinaweza kutia ndani sifa ya kusamehe, uaminifu, upendo, kuheshimu uzima, na kujizuia. Kwa hiyo, kanuni zetu za mwenendo zinachochea tabia yetu, mambo ambayo tunatanguliza katika maisha, mahusiano yetu, na pia muongozo ambao tunawapatia watoto wetu kuhusu mwenendo muzuri. Lakini, hata ikiwa kanuni za mwenendo ni za maana, watu wengi hawazifuate tena.

MWENENDO WA WATU UNAHARIBIKA KABISA

Katika mwaka wa 2008, wachunguzi katika inchi ya Amerika waliuliza mamia ya vijana wakubwa juu ya maoni yao kuhusu kanuni za mwenendo. David Brooks katika gazeti moja alisema hivi: “Jambo lenye kuvunja moyo ni namna wanavyofikiri na kuzungumuza vibaya juu ya kanuni za mwenendo.” (The New York Times) Wengi kati yao walifikiri kwamba kubaka ao kulala mwanamuke kinguvu na kuua ni vibaya, lakini “isipokuwa tu makosa hayo makubwa, hawakufikiri kuhusu mambo ambayo ni mema na yale ambayo ni mabaya, hata wakati walifikiria mambo kama vile mutu kutembeza motokari akiwa mulevi, kuiba majibu kwenye masomo ao mutu kukosa uaminifu kwa bibi ao bwana yake.” Kijana mumoja alisema, “Mara nyingi, sijali kabisa ikiwa jambo ni njema ao ni mbaya.” Watu wengi walikuwa na maoni haya: ‘Ikiwa unaona jambo ni nzuri, ulifanye. Fuata namna moyo wako unakuambia.’ Je, ni jambo la hekima kufikiri hivyo?

Moyo wa mwanadamu unaweza pia kuwa ‘wenye hila na hatari’ hata ikiwa una uwezo wa kuonyesha upendo mukubwa na huruma. (Yeremia 17:9) Jambo hilo la kweli lenye kuhuzunisha linaonyeshwa na tabia za ulimwengu zenye kubadilika-badilika ambazo Biblia ilitabiri. Tangu zamani sana Biblia ilisema kwamba “katika siku za mwisho,” “watu watakuwa na ubinafsi, wenye tamaa ya fedha, wenye majivuno, na wenye kujiona,” na pia watakuwa “wasio na shukrani na waovu.” Tena, “watachukia chochote kilicho chema” na “watapenda anasa kuliko kumpenda Mungu.”​—2 Timotheo 3:1-5, Biblia Habari Njema.

Mambo hayo ya kweli yanapaswa kutuchochea tuchunguze moyo wetu kuliko kuamini kila kitu ambacho moyo unatusukuma tufanye! Kwa kweli, Biblia inasema waziwazi hivi: ‘Anayetegemea moyo wake mwenyewe ni mujinga.’ (Methali 28:26) Andiko hilo linaonyesha kwamba, ili moyo wetu utuongoze vizuri, unahitaji kurekebishwa kupitia kanuni nzuri za mwenendo. Ni wapi tunaweza kupata kanuni kama hizo? Watu wengi wanatafuta kanuni hizo katika Biblia, na wanafurahia hekima iliyo ndani ya kitabu hicho na namna kinavyosema mambo waziwazi.

KANUNI ZA MWENENDO AMBAZO TUNAWEZA KUTUMAINIA!

Kanuni za Biblia za mwenendo zinaonyesha uhakika wa kwamba zilifanywa kabisa kwa ajili ya wanadamu. Tufikirie mifano michache, ni kusema, sifa kama vile upendo, wema, ukarimu, na unyoofu ao uaminifu.

Kupenda watu wengine.

Kitabu kimoja kinasema hivi: “Ikiwa umejifunza kuwapenda watu wengine, utakuwa mwenye furaha kabisa.” (Engineering Happiness​—A New Approach for Building a Joyful Life) Kwa wazi, sisi wanadamu tunahitaji upendo. Bila upendo, hatuwezi kuwa wenye furaha kabisa.

Mambo ambayo Biblia inasema: “Jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.” (Wakolosai 3:14) Muandikaji huyo huyo wa Biblia alisema pia hivi: “Ikiwa . . . sina upendo, mimi si kitu.”​—1 Wakorintho 13:2.

Huo si upendo ambao unategemea ngono wala si musisimuko tu wa moyoni; ni upendo ambao unaongozwa na kanuni. Ni aina ya upendo ambao unatusukuma kumusaidia mugeni aliye na magumu, bila kutazamia atulipe. Katika andiko la 1 Wakorintho 13:4-7, tunasoma hivi: ‘Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fazili. Upendo hauna wivu, haujigambe, haujivune, haujiendeshe bila adabu, hautafute faida zake wenyewe, hauchokozeke. Hauweke hesabu ya ubaya. Haushangilie juu ya ukosefu wa uadilifu, bali unashangilia pamoja na kweli. Unahimili mambo yote, unavumilia mambo yote.’

Ikiwa familia zinakosa upendo kama huo, kila mutu anateseka, zaidi sana watoto. Mwanamuke anayeitwa Monica aliandika kwamba alipokuwa mutoto, alivumilia kutendewa vibaya kimwili, kimoyoni, na alitendewa vibaya kingono. Anasema hivi: “Sikuwa ninapendwa hata kidogo na sikuwa na tumaini lolote.” Kisha, alipokuwa na miaka 15, alienda kuishi na wazazi wa mama yake ambao ni Mashahidi wa Yehova.

Monica anasema hivi: “Katika miaka miwili ambayo niliishi pamoja nao, walinifundisha kuwa muchangamufu, mwenye upendo, na mwenye kuhangaikia watu wengine hata ikiwa nilikuwa kijana mwanamuke mwenye haya. Walinisaidia kuwa kijana mwanamuke mwenye kuheshimika.” Kwa sasa, Monica ni mwenye furaha katika ndoa yake, anawaonyesha watu wengine upendo kwa kuwaelezea ujumbe wa Biblia, akiwa pamoja na bwana yake na watoto wao watatu.

Kupenda vitu vya kimwili ni adui anayeharibu upendo. Watu wanaamini kwamba kuwa na vitu vingi vya kimwili na kufuatia raha ndiyo mambo ya maana zaidi katika maisha. Hata hivyo, inashangaza kwamba uchunguzi uliofanywa na watu wenye elimu umeonyesha tena na tena kuwa watu hawahitaji feza nyingi ili kuwa na furaha. Kwa kweli, watu ambao wanapenda sana vitu vya kimwili wanaweza kujiletea magumu katika maisha na kukosa furaha, na Biblia inakubali pia wazo hilo. Andiko la Mhubiri 5:10 linasema hivi: ‘Anayependa feza hatatosheka na feza, wala anayependa mali hatatosheka na mapato. Hilo pia ni ubatili.’ Biblia inasema pia hivi: “Namna yenu ya maisha iwe bila upendo wa pesa.”​—Waebrania 13:5.

Wema na ukarimu.

Habari fulani iliyoandikwa na shirika la uchunguzi kwenye Masomo ya Juu ya Kalifornia, huko Amerika, ilisema hivi: “Je, halingekuwa jambo la kufurahisha ikiwa ungeenda ndani ya duka fulani na kununua furaha yenye kudumu? Wazo hilo si la kuwazia tu kama linavyosikika kwa sababu kila kitu unachonunua kimekusudiwa kwa ajili ya mutu mwengine.” Hilo linamaanisha nini? Linamaanisha kwamba kutoa kunatuletea furaha zaidi kuliko kupokea.

Mambo ambayo Biblia inasema: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”​—Matendo 20:35.

Mara nyingi, aina ya kutoa ambayo ni nzuri zaidi na yenye kuleta faida zaidi ni kujitoa wenyewe, ni kusema, kutoa wakati wetu na nguvu zetu wenyewe. Kwa mufano, mwanamuke anayeitwa Karen aliona wanawake watatu, ni kusema, mama na watoto wake wawili wanawake, wakikaa katika motokari yao, boneti ao sehemu ya mbele ikiwa yenye kufunguliwa. Mama na mutoto wake mumoja mwanamuke walipaswa kusafiri kwa ndege; lakini motokari yao ilikataa kuwaka, taksi ambayo waliita ilichelewa kufika. Karen alijitolea kuwapeleka na motokari yake, hata ikiwa motokari ilipaswa kutembea dakika 45 ili kufika kwenye uwanja wa ndege. Walikubali Karen awapeleke. Alipokuwa akirudi, Karen alimuona yule mutoto mwanamuke aliyebaki akiendelea kungoja ndani ya motokari yake akiwa mahali pa kuegeshea motokari.

Mutoto huyo mwanamuke alisema hivi: “Bwana yangu yuko njiani anakuja.”

Karen naye akamujibu: “Sawa, ninafurahi kuona uko salama. Ninaenda kufanya kazi katika bustani kwenye Jumba letu la Ufalme, ao kanisa.”

Mwanamuke huyo akamuuliza: “Wewe ni Shahidi wa Yehova?”

Karen akasema: “Ndiyo,” na mazungumuzo mafupi yakafuata.

Majuma machache kisha hapo, Karen alipokea barua kwenye Internete. Sehemu fulani ya barua hiyo inasema hivi: “Mimi na mama yangu hatukusahau jambo nzuri ambalo ulitufanyia. Kwa sababu yako, tulikuta ndege na tukasafiri! Dada yangu alituambia kwamba wewe ni Shahidi wa Yehova, kwa hiyo tukaelewa sababu gani ulitufanyia jambo nzuri kama hilo. Mama yangu ni Shahidi wa Yehova, na mimi ni Shahidi wa Yehova lakini sihubiri tena. Lakini nitajikaza kurekebisha jambo hilo hivi karibuni!” Karen alifurahi sana kwamba alisaidia waamini wenzake wawili. Anasema hivi: “Nililia.”

Muandikaji Charles Dudley Warner aliandika hivi: “Ni moja kati ya zawadi nzuri sana za . . . maisha kwamba hakuna mutu yeyote ambaye anaweza kujaribu kumusaidia kabisa mutu mwengine bila kujisaidia yeye mwenyewe.” Ni hivyo kwa sababu Mungu aliwaumba wanadamu ili waonyeshe sifa zake nzuri sana, hakuwaumba ili wajifikirie wenyewe.​—Mwanzo 1:27.

Unyoofu ao uaminifu.

Kanuni hiyo ni ya maana ili kuwe na utaratibu kati ya watu. Ukosefu wa uaminifu unatokeza woga, kukosa kuaminiana, na kuharibika kwa jamii.

Mambo ambayo Biblia inasema: ‘Ni nani atakayekuwa mugeni katika hema la Mungu?’ Jibu ni: “Yeye anayetembea bila kosa na . . . kusema kweli katika moyo wake.” (Zaburi 15:1, 2) Kwa wazi, uaminifu wa kweli ni sifa ambayo inamutambulisha mutu kipekee, kama vile sifa zingine ambazo tumezungumuzia. Sifa hiyo haijitokeze kwa sababu ya hali ao kwa kuangalia faida.

Unakumbuka Christina ambaye aliokota mukoba uliokuwa na feza? Ni wazi kwamba tamaa ya moyo wake haikuwa kupata utajiri, lakini ilikuwa kumupendeza Mungu. Kwa hiyo, wakati mutu aliyekuwa akihangaika kutafuta feza zake alirudi, Christina alimuambia kwamba feza zake zilipatikana. Mutu huyo alishangazwa na uaminifu wa Christina. Hata mukubwa wake wa kazi alishangaa pia, kwa sababu alimupandisha Christina cheo; akamufanya kuwa musimamizi wa duka la kampuni, cheo ambacho kiliomba mutu mwenye kutumainika kabisa. Maneno ya andiko la 1 Petro 3:10 ni ya kweli kabisa. Andiko hilo linasema hivi: ‘Yeye ambaye anapenda uzima na kuona siku zilizo njema, na azuie . . . midomo yake isiseme udanganyifu.’

‘TEMBEA KATIKA NJIA YA WATU WEMA’

Kanuni za mwenendo zilizo katika Biblia zinaonyesha upendo mwingi wa Muumbaji wetu kutuelekea, kwa sababu kanuni hizo zinatuwezesha “kutembea katika njia ya watu wema.” (Methali 2:20; Isaya 48:17, 18) Ikiwa tunafuata muongozo huo, sisi pia tunaonyesha upendo wetu kwa Mungu na tutapata zawadi nyingi. Kwa kweli, Biblia inaahidi hivi: ‘Shika njia ya Mungu, naye atakuinua uimiliki dunia. Watu waovu watakapokatiliwa mbali, wewe utaona hilo.’​—Zaburi 37:34

Kwa kweli, wakati ujao muzuri sana unawangojea watu wenye kushika kanuni za Biblia, watakuwa na maisha mazuri katika dunia yenye amani ambamo uovu hautakuwa! Bila shaka, tunapaswa kufikiria kanuni za mwenendo zilizo katika Biblia.