Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Peshitta ya Kisiria—Ni Njia ya Kujua Mengi Juu ya Historia ya Tafsiri za Kwanza-Kwanza za Biblia

Peshitta ya Kisiria—Ni Njia ya Kujua Mengi Juu ya Historia ya Tafsiri za Kwanza-Kwanza za Biblia

Kwa muda wa siku kenda katika mwaka wa 1892, wanawake wawili mapacha Agnes Smith Lewis na Margaret Dunlop Gibson walisafiri kwa ngamia katika jangwa mupaka kwenye Makao ya Watawa ya Sainte-Catherine. Makao hayo yalikuwa chini ya Mulima Sinai. Sababu gani wanawake hao wawili waliokaribia miaka 50 walifanya safari kama hiyo wakati ambapo ilikuwa hatari sana kusafiri katika eneo lililoitwa Mashariki? Jibu linaweza kukusaidia uamini sana kwamba Biblia haina makosa.

Agnes Smith Lewis na Makao ya Watawa ya Sainte-Catherine

MBELE tu ya kurudia mbinguni, Yesu aliwaagiza wanafunzi wake watoe ushahidi juu yake ‘katika Yerusalemu na pia katika Yudea yote na Samaria na mupaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.’ (Matendo 1:8) Wanafunzi walifanya kazi hiyo kwa bidii na uhodari. Lakini, mahubiri yao katika Yerusalemu yaliwaletea upinzani mukali, na kwa sababu ya upinzani huo Stefano aliuawa juu ya imani yake. Wengi kati ya wanafunzi wa Yesu walikimbilia Antiokia, huko Siria, muji mumoja kati ya miji mikubwa ya Utawala wa Roma. Muji huo ulikuwa kwenye kilometa 550 hivi kaskazini mwa Yerusalemu.—Matendo 11:19.

Katika Antiokia, wanafunzi waliendelea kuhubiri “habari njema” juu ya Yesu, na watu wengi ambao hawakuwa Wayahudi wakaamini. (Matendo 11:20, 21) Hata ikiwa Kigiriki ndiyo luga moja iliyozungumuzwa katika muji wa Antiokia, Kisiria ndiyo luga iliyozungumuzwa na watu katika maeneo ya inje ya muji huo na katika jimbo.

HABARI NJEMA ILIYOTAFSIRIWA KATIKA KISIRIA

Wakati hesabu ya Wakristo waliozungumuza Kisiria iliongezeka kati ya mwaka wa 101 na 200, kukakuwa ulazima wa kutafsiri habari njemakatika luga yao. Kwa hiyo, inaonekana kwamba luga ya watu wa kawaida ambamo sehemu fulani za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo zilitafsiriwa kwanza ni Kisiria, wala si Kilatini.

 Kufikia mwaka wa 170 kisha kuzaliwa kwa Yesu, muandishi Musiria Tatian (karibu mwaka wa 120-173 kisha kuzaliwa kwa Yesu) aliunganisha Injili ine zinazokubalika na kutokeza, katika Kigiriki ao Kisiria, kitabu kinachoitwa na watu wengi Diatessaron, neno la Kigiriki linalomaanisha “kupitia [Injili] ine.” Kisha, Ephraem Musiria (karibu mwaka wa 310-373 kisha kuzaliwa kwa Yesu) aliandika maelezo juu ya Diatessaron. Hilo linahakikisha kwamba Wakristo Wasiria walitumia sana kitabu hicho.

Kitabu Diatessaron kinatupendeza sana leo. Sababu gani? Kati ya mwaka wa 1801 na 1900, watu fulani wenye elimu walibishana ikiwa Injili ziliandikwa kati ya mwaka wa 130 na 170 kisha kuzaliwa kwa Yesu, na kwamba Injili hazingekuwa habari za kweli juu ya maisha ya Yesu. Hata hivyo, maandishi ya zamani ya Diatessaron ambayo yalikuwa yamevumbuliwa kuanzia wakati huo yalihakikisha kwamba Injili ya Mathayo, Marko, Luka, na Yohana zilikuwa zimeenea sana kufikia mwaka wa 150 hivi. Kwa hiyo, Injili hizo zilipaswa kuwa ziliandikwa mbele ya hapo. Zaidi ya hilo, wakati Tatian aliunganisha Diatessaron, hakutumia kitabu chochote cha zile zinazoitwa injili za apokrifa (vitabu vingine vinavyosemwa kuwa Injili) kama vile alivyotumia Injili ine zinazokubaliwa. Hilo linaonyesha wazi kwamba injili za apokrifa hazikuonekana kuwa za kweli na zenye kukubalika.

Peshitta ya Kisiria ya Pantateki, mwaka wa 464 kisha kuzaliwa kwa Yesu, ni maandishi ya Biblia ya pili ya zamani sana yenye kuwa na tarehe

Kufikia mwanzo wa miaka kati ya 401 na 500, tafsiri ya Biblia katika Kisiria ilianza kutumiwa sana kaskazini mwa Mesopotamia. Tafsiri hiyo ambayo labda ilifanywa kati ya mwaka wa 101 na 200 ao kati ya mwaka wa 201 na 300 kisha kuzaliwa kwa Yesu, ilikuwa na vitabu vyote vya Biblia isipokuwa tu 2 Petro, 2 na 3 Yohana, Yuda, na Ufunuo. Tafsiri hiyo inaitwa Peshitta, jina linalomaanisha “Nyepesi” ao “Wazi.” Peshitta ni kati ya vitabu vya zamani na vya maana sana vilivyosaidia kueneza maandishi ya Biblia.

Jambo lenye kupendeza ni kwamba maandishi moja ya Peshitta yana tarehe inayolingana na mwaka wa 459/460 kisha kuzaliwa kwa Yesu. Kwa sababu ya tarehe hiyo, Peshitta inaonekana kuwa ndiyo maandishi ya zamani sana ya Biblia yaliyo na tarehe kamili. Katika mwaka wa 508 hivi kisha kuzaliwa kwa Yesu, Peshitta ilirekebishwa na ikakuwa na vitabu vitano ambavyo havikukuwa ndani. Peshitta iliyorekebishwa ilikuja kuitwa Philoxenian Version.

MAANDISHI MENGINE YA KISIRIA YALIYOVUMBULIWA

Kufikia mwaka kati ya 1801 na 1900, karibu kopi zote za Kigiriki za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo zilikuwa za tangu mwaka kati ya 401 na 500 ao miaka mingi kisha hapo. Kwa sababu hiyo, watu wenye elimu ya Biblia walipendezwa zaidi sana na tafsiri kama hizo za kwanza-kwanza, kwa mufano Vulgate ya Kilatini na Peshitta ya Kisiria. Wakati huo, watu fulani walisadiki kwamba Peshitta ilitokana na tafsiri ya zamani ya Kisiria iliyorekebishwa. Lakini tafsiri kama hiyo haikujulikana. Kwa sababu Biblia ya Kisiria iliandikwa tangu mwaka kati ya 101 na 200, tafsiri kama hiyo ingesaidia kuelewa maandishi ya Biblia tangu mwanzoni, na bila shaka ingekuwa ya lazima sana kwa watu wenye elimu ya Biblia! Kulikuwa kabisa tafsiri ya Kisiria ya zamani? Ingepatikana?

Palimpseste inayoitwa maandishi ya Kisiria ya Sinai. Maandishi ya Injili yaliyoandikwa chini yanaonekana katika sehemu ya pembeni-pembeni

Ndiyo, bila shaka! Kwa kweli, maandishi mawili kama hayo ya maana sana ya Kisiria yalipatikana. Maandishi ya kwanza yalikuwa ya kati ya mwaka wa 401 na 500. Yalikuwa kati ya hesabu kubwa ya maandishi ya Kisiria yaliyopatikana kwenye Jumba la Makumbusho la Uingereza katika mwaka wa 1842, yalitoka kwenye makao ya watawa (monastère) katika Jangwa la Nitrian la Misri. Maandishi hayo yaliitwa Curetonia ya Kisiria kwa sababu yalivumbuliwa na kugawanywa na William Cureton, mutunzaji musaidizi wa maandishi katika jumba la kuwekea maandishi. Maandishi hayo ya maana sana yalikuwa na Injili ine zenye kupangwa kuanzia Mathayo, Marko, Yohana, na Luka.

Maandishi ya pili yaliyochungwa mupaka siku zetu ni Tafsiri ya Kisiria ya Sinai. Maandishi hayo yalivumbuliwa kwa sababu ya uhodari wa wanawake wawili mapacha waliotajwa kwenye mwanzo wa habari hii. Hata ikiwa Agnes hakusoma masomo ya juu, alijifunza luga munane, kutia ndani Kisiria. Katika mwaka wa 1892, Agnes alivumbua kitu cha maana sana katika makao ya watawa ya Sainte-Catherine katika Misri.

 Huko, katika kabati lenye giza, alipata maandishi ya Kisiria. Kulingana na maelezo yake mwenyewe, “yalikuwa yanafanana mubaya kwa sababu yalikuwa machafu sana, karatasi zake zilikuwa karibu zenye kukamatana kwa sababu zilibakia bila kugeuzwa” kwa mamia ya miaka. Yalikuwa maandishi ya palimpseste *, ni kusema, maandishi yake ya kwanza yalivutwa na kwenye kurasa hizo kuliandikwa maandishi ya Kisiria yenye kuhusu watakatifu wanawake. Lakini, Agnes aliona maandishi fulani yaliyofichwa chini na pia maneno “ya Mathayo,” “ya Marko,” ao “ya Luka” kwenye sehemu ya juu. Kile alichovumbua ilikuwa kodeksi karibu yote ya Kisiria ya Injili ine! Leo, watu wenye elimu wanaamini kwamba kodeksi hiyo iliandikwa kwenye mwisho wa miaka kati ya 301 na 400.

Tafsiri ya Kisiria ya Sinai inaonwa kuwa moja kati ya maandishi ya Biblia ya maana sana yaliyovumbuliwa, maandishi ya Kigiriki kama vile Kodeksi ya Sinai na Kodeksi ya Vatikani yanaonwa pia hivyo. Kwa kawaida, watu wanaamini kwamba maandishi yanayoitwa Curetonia na maandishi ya Sinai ni kopi za sasa za Injili za Kisiria za zamani za tangu mwisho wa miaka kati ya 101 na 200 ao mwanzo wa miaka kati ya 201 na 300.

NENO LA MUNGU WETU LINADUMU MILELE

Maandishi hayo yanaweza kusaidia wanafunzi wa Biblia leo? Bila shaka! Tuchukue mufano wa ule unaoitwa umalizio murefu wa Injili ya Marko, ambao katika Biblia fulani unafuata andiko la Marko 16:8. Umalizio huo unapatikana katika Kodeksi ya Aleksandria ya Kigiriki ya kati ya mwaka wa 401 na 500, katika Vulgate ya Kilatini, na katika maandishi mengine. Hata hivyo, maandishi mawili ya Kigiriki yenye kutegemeka, ni kusema, Kodeksi ya Sinai na Kodeksi ya Vatikani, yote mawili yanaisha na Marko 16:8. Maandishi ya Kisiria ya Sinai hayana umalizio huo murefu. Hilo linahakikisha zaidi kwamba umalizio huo murefu ni sehemu iliyoongezwa baadaye na haikuwa sehemu ya maandishi ya kwanza ya Injili ya Marko.

Tuchukue mufano mwengine. Kati ya mwaka wa 1801 na 1900, karibu tafsiri zote za Biblia zilikuwa na maneno ya uongo kuhusu Utatu yaliyoongezwa kwenye andiko la 1 Yohana 5:7. Lakini, maneno hayo yaliyoongezwa hayapatikane katika maandishi ya zamani ya Kigiriki na hayapatikane katika Peshitta. Hilo linaonyesha kwamba maneno hayo yaliyoongezwa kwenye andiko la 1 Yohana 5:7 ni maelezo yaliyoharibisha maandishi ya Biblia.

Kwa kweli, Yehova Mungu amelinda Neno lake Takatifu, kama alivyoahidi. Katika Neno hilo, tunahakikishiwa hivi: ‘Majani mabichi yamekauka, ua limenyauka; lakini kwa habari ya neno la Mungu wetu, litadumu mupaka wakati usio na kipimo [ao milele].’ (Isaya 40:8; 1 Petro 1:25) Tafsiri inayoitwa Peshitta inatimiza kazi ndogo lakini ya maana katika kueneza ujumbe wa Biblia kwa watu wote bila makosa.

^ fu. 15 Neno la Kigiriki pa·lim’pse·stos linamaanisha “kilichokwaruzwa tena.”