Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

BIBLIA INABADILISHA MAISHA YA WATU

“Watu Wengi Walinichukia”

“Watu Wengi Walinichukia”
  • ALIZALIWA MWAKA WA 1978

  • ALIZALIWA KATIKA INCHI YA CHILE

  • ALIKUWA MUKALI SANA

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nilikomalia katika Santiago, muji mukubwa wa inchi ya Chile, muji ambamo kutumia dawa za kulewesha, vikundi vya watu wenye kutenda maovu, na uvunjaji wa sheria yalikuwa mambo ya kawaida. Nilipokuwa na miaka mitano, baba yangu aliuawa. Kisha hapo, mama yangu alikuwa akiishi na mwanaume ambaye alikuwa mukali sana. Mara kwa mara alinipiga mimi na mama yangu. Bado ningali na maumivu moyoni kwa sababu ya miaka hiyo.

 

Nilipokuwa ninakomaa, nilikuwa ninatenda kwa ukali sana wakati mutu fulani alinitendea vibaya. Nilikuwa ninasikiliza muziki wenye mudundo mukali, nilikuwa ninakunywa pombe kupita kiasi, na mara kwa mara nilitumia dawa za kulewesha. Kwa kawaida, nilipigana barabarani na watu waliouzisha dawa za kulewesha, ambao mara nyingi walijaribu kuniua. Wakati fulani, kikundi kingine cha watenda maovu kilimulipa feza mutu fulani aliyejulikana kuwa mubaya sana ili aniue, nilikimbia nikiwa na kidonda cha kisu ambacho alinichoma. Wakati mwengine, kikundi cha watu waliouzisha dawa za kulewesha kilinielekezea bunduki kwenye kichwa changu na kujaribu kunifyatulia risasi.

Katika mwaka wa 1996, nilipenda mwanamuke anayeitwa Carolina, na tukaoana katika mwaka wa 1998. Kisha kuzaliwa kwa mutoto wetu mwanaume wa kwanza, niliogopa kwamba kwa sababu ya tabia yangu ya ukali, ningekuwa kama bwana ya mama yangu na kutesa familia yangu. Kwa hiyo, nilienda kutafuta musaada kwenye kituo cha kurekebisha tabia. Nilipata matunzo na dawa, lakini sikubadilika. Niliendelea kuwa mwenye hasira kali hata juu ya kitu kidogo tu; sikuwa ninaweza kujizuia. Ili nisiendelee kutesa familia yangu, nilijaribu kujiua. Jambo la kufurahisha ni kwamba sikuweza kujiua.

Kwa miaka mingi, sikuamini kwamba kuna Mungu, lakini nilitaka sasa kumuamini Mungu. Kwa hiyo, nilijiunga na dini ya kievanjelisti kwa muda fulani. Wakati huohuo, bibi yangu alikuwa anajifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Nilichukia Mashahidi wa Yehova, na mara nyingi niliwatukana kwa sauti kubwa. Lakini sikuzote walinijibu kwa upole, jambo ambalo sikutazamia.

Siku moja, Carolina aliniomba nisome andiko la Zaburi 83:18 katika Biblia yangu mwenyewe. Andiko hilo linasema waziwazi kwamba jina la Mungu ni Yehova. Nilishangaa kuona kwamba katika dini yangu nilijifunza kuhusu mungu fulani, lakini si kuhusu Yehova. Mwanzoni mwa mwaka wa 2000, mimi pia nilianza kujifunza Biblia na Mashahidi.

BIBLIA ILIBADILISHA MAISHA YANGU: Nilipokuwa nikifanya maendeleo, nilifarijiwa kujua kwamba Yehova ni Mungu mwenye huruma na mwenye kusamehe. Kwa mufano, katika andiko la Kutoka 34:6, 7, Biblia inaeleza kuwa Yehova ni ‘Mungu mwenye rehema na neema, si mwepesi wa hasira naye ni mwingi wa fazili zenye upendo na kweli, anayehifazi fazili zenye upendo kwa ajili ya maelfu, anayesamehe kosa na ubaya na zambi.’

 

Hata hivyo, halikuwa jambo rahisi kwangu kufuata mambo ambayo nilikuwa ninajifunza. Nilikuwa na uhakika kwamba sitaweza hata siku moja kuzuia hasira yangu kali. Kila mara niliposhindwa kuzuia hasira yangu, Carolina alinitia moyo kwa upendo. Alinikumbusha kwamba Yehova anaona bidii ambayo nilikuwa ninafanya. Musaada wake ulinitia nguvu kuendelea kujaribu kumupendeza Yehova, hata ikiwa mara nyingi nilijisikia kuwa sikuwa na tumaini la kushinda uzaifu wangu.

Nilifarijiwa kujua kwamba Yehova ni Mungu mwenye huruma na mwenye kusamehe

Siku moja, Alejandro, ndugu aliyekuwa akijifunza na mimi Biblia aliniomba nisome andiko la Wagalatia 5:22, 23. Andiko hilo linasema kwamba tunda la roho ya Mungu ni ‘upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fazili, wema, imani, upole, kujizuia.’ Alejandro alinifasiria kwamba sikupaswa kutegemea nguvu zangu mwenyewe ili kukomalisha sifa hizo, lakini nilipaswa kutegemea roho takatifu ya Mungu. Maneno hayo ya kweli yalibadilisha kabisa-kabisa maoni yangu!

Kisha, nilihuzuria mukusanyiko mukubwa wa Mashahidi wa Yehova. Utaratibu, usafi, na urafiki ambao niliona kwenye mukusanyiko huo, mambo yote hayo yalinihakikishia kwamba nilikuwa nimepata dini ya kweli. (Yohana 13:34, 35) Nilibatizwa Mwezi wa 2, 2001.

FAIDA AMBAYO NIMEPATA: Yehova amebadilisha tabia yangu; nilikuwa mutu mukali sana lakini sasa mimi ni mutu mwenye amani. Ninajisikia kana kwamba alinitoa ndani ya matope ambamo nilikuwa ninazama. Watu wengi walinichukia, na mimi siwaone kuwa wenye makosa. Hata hivyo, sasa ninafurahia kumutumikia Yehova kwa amani pamoja na bibi yangu na watoto wetu wawili wanaume.

 

Watu wa jamaa yangu na marafiki wangu wa zamani wanashangaa kuona nimebadilika sana. Kwa sababu ya mabadiliko ambayo nimefanya, wengi wao wanapendezwa kujifunza mafundisho ya Biblia. Pia, nina pendeleo la kuwasaidia watu wengine wamujue Yehova. Nimekuwa mwenye furaha sana kuona namna mafundisho ya Biblia yamebadilisha maisha yao pia!