Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Jiji la Kale la Yerusalemu Liliharibiwa Mwaka Gani?—Sehemu ya Pili

Jiji la Kale la Yerusalemu Liliharibiwa Mwaka Gani?—Sehemu ya Pili

Jiji la Kale la Yerusalemu Liliharibiwa Mwaka Gani?​—Sehemu ya Pili

Mabamba ya Udongo Yanaonyesha Nini Hasa?

Hii ni makala ya pili kati ya makala mbili katika matoleo mawili yanayofuatana ya Mnara wa Mlinzi ambayo yanazungumzia maswali ya wasomi kuhusu mwaka wa kuharibiwa kwa jiji la kale la Yerusalemu kwa mara ya kwanza. Sehemu hizi mbili zinazofuatana zinazungumzia majibu ya maswali ambayo yamewatatanisha wasomaji fulani. Majibu hayo yaliyofanyiwa utafiti kikamili yanategemea Biblia.

Sehemu ya Kwanza Ilithibitisha Mambo Yafuatayo:

▪ Wanahistoria wanasema kwamba jiji la Yerusalemu liliharibiwa mwaka wa 587 K.W.K. *

▪ Kulingana na mfuatano wa matukio katika Biblia, uharibifu huo ulitokea mwaka wa 607 K.W.K.

▪ Wanahistoria wamefikia maamuzi yao kwa kutegemea maandishi ya wanahistoria wa kale na orodha ya Ptolemy.

▪ Maandishi fulani ya wanahistoria wa kale yana makosa makubwa na nyakati nyingine yanatofautiana na maandishi kwenye mabamba ya udongo. *

BIBLIA inasema kwamba Wayahudi waliotekwa walipaswa kukaa uhamishoni Babiloni ‘mpaka miaka sabini itimie ili kulitimiza neno la BWANA kwa kinywa cha Yeremia.’ Waliachiliwa huru mwaka gani? Katika “mwaka wa kwanza wa [utawala wa] Koreshi, mfalme wa Uajemi.” (2 Mambo ya Nyakati 36:21, 22, Union Version) Kulingana na Biblia na wanahistoria, uhamisho huo uliisha baada ya Koreshi kushinda Babiloni na kuwakomboa Wayahudi ambao walirudi Yerusalemu mwaka wa 537 K.W.K. Kwa kuwa Biblia inasema waziwazi kwamba Wayahudi walikaa uhamishoni kwa miaka 70, lazima uhamisho huo uwe ulianza mwaka wa 607 K.W.K.

Hata hivyo, wasomi wengi wanasema jiji la Yerusalemu liliharibiwa mwaka wa 587 K.W.K. Hilo linamaanisha kwamba uhamisho huo ulikuwa wa miaka 50 tu. Kwa nini wanasema hivyo? Wanafanya hesabu zao kwa kutumia hati za maandishi ya kale ya kikabari ambayo yanaeleza kwa undani kipindi cha utawala cha Nebukadneza wa Pili na wafalme waliofuata.1 Nyingi za hati hizo ziliandikwa na watu walioishi wakati Yerusalemu lilipoharibiwa au karibu na wakati huo. Lakini hesabu zinazoonyesha mwaka wa 587 K.W.K. zinategemeka kwa kadiri gani? Hati hizo zinaonyesha nini hasa?

Ili kujibu maswali hayo, ona maandishi kwenye hati tatu ambazo wasomi wanategemea mara nyingi: (1) Maandishi ya mfuatano wa matukio kuhusu Babiloni, (2) mabamba ya mambo ya kibiashara, na (3) mabamba ya wataalamu wa nyota.

Maandishi ya mfuatano wa matukio kuhusu Babiloni.

Maandishi hayo ni nini? Ni maandishi yaliyo kwenye mabamba kadhaa kuhusu matukio makubwa katika historia ya Babiloni.2

Wataalamu wamesema nini? R. H. Sack, mtaalamu wa maandishi ya kikabari, anasema kwamba maandishi hayo hayana habari kamili kuhusu matukio muhimu. * Aliandika kwamba wanahistoria wanapaswa kuchunguza “vyanzo vingine . . . ili kujua kilichotukia hasa.”

Maandishi hayo yanaonyesha nini? Kuna mapengo katika historia iliyorekodiwa katika maandishi ya mfuatano wa matukio kuhusu Babiloni.3 (Ona  sanduku lililo hapa chini.) Hivyo basi, inafaa kuuliza, Maamuzi yanayotegemea historia kama hiyo yenye mapengo yanategemeka kwa kadiri gani?

Mabamba ya mambo ya kibiashara.

Mabamba hayo ni nini? Mabamba mengi ya kipindi cha Milki Mpya ya Babiloni ni risiti zilizotambulika kisheria. Mabamba hayo yaliandikwa tarehe iliyoonyesha siku, mwezi, na mwaka wa mfalme aliyekuwa akitawala. Kwa mfano, bamba moja linasema kwamba ununuzi fulani ulifanywa “Nisani, tarehe 27, katika mwaka wa 11 wa Nebukadreza [ambaye pia aliitwa Nebukadneza wa Pili], mfalme wa Babiloni.”4

Mfalme alipokufa au kuondolewa mamlakani na mfalme mpya kuanza kutawala, miezi iliyobaki katika mwaka wake wa utawala ilionwa kuwa mwaka wa kupokea mamlaka wa mfalme mpya. *5 Hiyo inamaanisha kwamba kuondoka kwa mtawala mmoja na mwingine kupokea mamlaka kulitokea mwaka uleule kwenye kalenda ya Wababiloni. Kwa hiyo, ni jambo linalopatana na akili kusema kwamba mabamba yaliyoonyesha mwaka ambao mfalme mpya alipokea mamlaka yanapaswa kuwa ya miezi iliyofuata mwezi wa mwisho wa mfalme aliyetangulia.

Wataalamu wamesema nini? R. H. Sack alichunguza mabamba mengi ya mambo ya kibiashara ya kipindi cha Milki Mpya ya Babiloni. Katika mwaka wa 1972, Sack alichunguza mabamba mapya yanayopatikana katika Jumba la Makumbusho la Uingereza na ambayo hayajachapishwa na kuandika kwamba “yanavuruga kabisa” maoni ya awali kuhusu kipindi cha kuondoka mamlakani cha Nebukadneza wa Pili na kumpisha mwana wake Amel-Marduk (ambaye pia anaitwa Evil-merodach).6 Jinsi gani? Sack alijua mabamba yalionyesha kwamba Nebukadneza wa Pili alikuwa bado anatawala katika mwezi wa sita wa mwaka wake wa mwisho (mwaka wa 43). Lakini uchunguzi wa mabamba hayo mapya kuhusu mwaka ambao mfalme aliyefuata, Amel-Marduk, alipokea mamlaka, umeonyesha kwamba mabamba hayo ni ya mwezi wa nne na wa tano wa mwaka ambao ulifikiriwa kuwa mwaka wa mwisho wa Nebukadneza wa Pili.7 Bila shaka, miezi hiyo haipatani.

Maandishi hayo yanaonyesha nini? Yanaonyesha kwamba muda uliopita baada ya mfalme mmoja kuondoka na mwingine kupokea mamlaka, haupatani. Kwa mfano, hati moja inaonyesha kwamba Nebukadneza wa Pili alikuwa bado anatawala katika mwezi wake wa kumi—miezi sita baada ya kipindi ambacho inawaziwa mtawala aliyepokea mamlaka baada yake alikuwa ameanza kutawala.8 Pia, kuna kutopatana kuhusiana na muda uliopita baada ya kuondoka kwa Amel-Marduk na kupokea mamlaka kwa Neriglisa, mtawala aliyefuata.9

Kwa nini kutopatana huko ni muhimu? Kama ilivyotajwa awali, mapengo katika maandishi ya mfuatano wa matukio kuhusu Babiloni yanaonyesha kwamba huenda hakuna rekodi kamili ya mfuatano wa matukio hayo.10 Je, huenda kuna wafalme wengine wasiotajwa ambao walitawala katika vipindi hivyo vya kuondoka na kupokea mamlaka kwa wafalme? Ikiwa ndivyo, miaka kadhaa inapaswa kuongezwa kwenye kipindi cha Milki Mpya ya Babiloni. Kwa hiyo, maandishi ya mfuatano wa matukio kuhusu Babiloni na mabamba ya mambo ya kibiashara hayawezi kutumiwa kama msingi hakika wa kuthibitisha kwamba jiji la Yerusalemu liliharibiwa mwaka wa 587 K.W.K. *

Mabamba ya wataalamu wa nyota.

Mabamba hayo ni nini? Hayo ni mabamba ya kikabari yenye maelezo ya mpangilio wa jua, mwezi, sayari, na nyota, pamoja na habari za kihistoria kama vile mwaka wa utawala wa mfalme hususa. Kwa mfano, maandishi ya wataalamu wa nyota yaliyo hapa chini yanaonyesha kupatwa kwa mwezi kulikotokea mwezi wa kwanza wa mwaka wa kwanza wa utawala wa Mfalme Mukin-zeri.11

Wataalamu wamesema nini? Wanakubali kwamba Wababiloni walikuwa na chati na orodha nyingi sana waliyotumia kufanya hesabu ili kubashiri wakati ambapo yaelekea mwezi ungepatwa.12

Lakini je, Wababiloni wangeweza kuhesabu kwa kurudi nyuma ili kujua wakati ambapo kupatwa kwa mwezi kulitokea wakati uliopita? Profesa John Steele anasema: “Inawezekana kwamba baadhi ya ubashiri wa kwanza kabisa ulitolewa kwa kuhesabu kurudi nyuma wakati maandishi hayo yalipokuwa yakiandikwa.” (Italiki ni zetu.)13 Profesa David Brown, anayeamini kwamba chati hizo kuhusu mpangilio wa mwezi, sayari, na nyota zilikuwa na ubashiri uliokuwa umetolewa muda mfupi kabla ya matukio yaliyotajwa kutokea, anasema inawezekana kwamba baadhi ya “hesabu hizo zilifanywa kwa kurudi nyuma na waandishi katika karne ya nne Kabla ya Kristo na karne za baadaye.”14 Ikiwa hesabu hizo zilifanywa kwa kurudi nyuma, je, zinaweza kutegemeka kabisa bila kuungwa mkono na uthibitisho mwingine?

Hata kama kupatwa kwa mwezi kulitokea tarehe fulani, je, hilo linamaanisha kwamba habari za kihistoria ambazo mwandishi anahusianisha na tarehe hiyo ni sahihi? Si lazima iwe hivyo. Msomi R. J. van der Spek anaeleza: “Walioandika habari hizo walikuwa wataalamu wa nyota bali si wanahistoria.” Anaeleza kwamba habari za kihistoria kwenye sehemu fulani za mabamba hayo ni “za kijuujuu tu,” na kuonya kwamba ni lazima “zitumiwe kwa tahadhari.”15

Maandishi hayo yanaonyesha nini? Kwa mfano, fikiria bamba la VAT 4956. Mstari wa kwanza katika bamba hilo unasema: “Mwaka wa 37 wa Nebukadneza, mfalme wa Babiloni.”16 Kisha, linaeleza kwa undani mahali ambapo mwezi na sayari zilikuwa angani kwa kulinganishwa na nyota na makundi ya nyota. Pia, lina habari kuhusu tukio moja la kupatwa kwa mwezi. Wasomi wanasema kwamba mipangilio hiyo ya mwezi, sayari, na nyota ilitukia mwaka wa 568/567 K.W.K., kumaanisha kwamba mwaka wa 18 wa utawala wa Nebukadneza wa Pili ulikuwa 587 K.W.K., wakati alipoharibu jiji la Yerusalemu. Lakini je, marejeo hayo yanayotegemea uchunguzi wa mpangilio wa mwezi, sayari, na nyota yanaonyesha tu mwaka wa 568/567 K.W.K.?

Bamba hilo linataja tukio la kupatwa kwa mwezi ambalo hesabu za wataalamu wa nyota zinaonyesha lilitokea siku ya 15 ya mwezi wa tatu, au Simanu, katika kalenda ya Babiloni. Hapana shaka kwamba tukio hilo la kupatwa kwa mwezi lilitokea mwezi huo wa Simanu, tarehe inayolingana na Julai 4 (katika kalenda ya Yulio), mwaka wa 568 K.W.K. Hata hivyo, kulikuwa na tukio lingine la kupatwa kwa mwezi miaka 20 mapema, mnamo Julai 15, mwaka wa 588 K.W.K.17

Ikiwa mwaka 588 K.W.K. ndio mwaka wa 37 wa Nebukadneza wa Pili, basi mwaka wa 18 wa utawala wake ulikuwa 607 K.W.K.—mwaka ambao jiji la Yerusalemu liliharibiwa kulingana na mfuatano wa matukio ya Biblia! (Ona  mfuatano wa matukio ulio hapa chini.) Lakini je, bamba la VAT 4956 lina habari zaidi zinazounga mkono mwaka wa 607 K.W.K.?

Mbali na tukio la kupatwa kwa mwezi ambalo limetajwa, bamba hilo lina rekodi 13 za uchunguzi wa mwezi, na rekodi 15 za uchunguzi wa sayari. Rekodi hizo zinaonyesha mahali ambapo mwezi au sayari zilikuwa angani kwa kulinganishwa na nyota au makundi ya nyota.18 Pia, kuna vipindi vinane vya wakati, kati ya kuchomoza na kutua kwa jua au mwezi.18a

Kwa sababu habari kuhusu mahali ambapo mwezi ulikuwa angani kwa kulinganishwa na nyota nyingine zinategemeka sana, watafiti wamechunguza kwa makini rekodi hizo 13 kwenye bamba la VAT 4956. Walichunguza rekodi hizo kwa kutumia programu fulani ya kompyuta inayoweza kuonyesha mipangilio ya mwezi, sayari, na nyota katika tarehe fulani wakati uliopita.19 Uchunguzi wao ulifunua nini? Ingawa si rekodi zote kuhusu mipangilio hiyo zinazolingana na mwaka wa 568/567 K.W.K., zile rekodi 13 zinapatana na mahali ambapo mwezi ulikuwa angani miaka 20 mapema, yaani, mwaka wa 588/587 K.W.K.

Kuna sehemu moja ya bamba la 4956 ambayo imeonyeshwa kwenye kurasa hizi inayoonyesha kwamba mpangilio wa mwezi na nyota nyingine ulilingana na mwaka wa 588 K.W.K. vizuri zaidi kuliko mwaka wa 568 K.W.K. Mstari wa 3 wa bamba hilo unasema kwamba mwezi ulikuwa mahali fulani angani mnamo “usiku wa tarehe 9 [mwezi wa Nisanu].” Hata hivyo, wasomi walioonyesha mara ya kwanza kuwa mpangilio huo ulitokea mwaka wa 568 K.W.K. walisema kwamba katika mwaka huo wa 568 K.W.K., mwezi ulikuwa mahali hapo “tarehe 8 ya mwezi wa Nisanu, bali si tarehe 9.” Ili waunge mkono mwaka huo wa 568 K.W.K., walisema kwamba mwandishi aliandika kimakosa nambari “9” badala ya “8.”20 Lakini mahali ambapo mwezi ulikuwa kulingana na mstari wa 3 panalingana kabisa na Nisanu 9, mwaka wa 588 K.W.K.21

Kwa wazi, habari za wataalamu wa nyota katika bamba la VAT 4956 zinaonyesha kuwa mwaka wa 588 K.W.K. ndio mwaka wa 37 wa Nebukadneza wa Pili. Kwa hiyo, jambo hilo linaunga mkono mwaka wa 607 K.W.K. kuwa mwaka ambao jiji la Yerusalemu liliharibiwa—kama Biblia inavyoonyesha.

Kwa Nini Uiamini Biblia?

Leo, wanahistoria wengi wanaamini kwamba jiji la Yerusalemu liliharibiwa mwaka wa 587 K.W.K. Hata hivyo, waandikaji wa Biblia, Yeremia na Danieli, wanasema waziwazi kwamba Wayahudi walikaa uhamishoni kwa miaka 70, si miaka 50. (Yeremia 25:1, 2, 11; 29:10; Danieli 9:2) Maandiko hayo yanaonyesha waziwazi kwamba Yerusalemu liliharibiwa mwaka wa 607 K.W.K. Kama uthibitisho uliotajwa unavyoonyesha, maandiko hayo yanaungwa mkono kwa kadiri fulani na maandishi mengine ya kihistoria.

Wataalamu mbalimbali wametilia shaka usahihi wa Biblia. Hata hivyo, uthibitisho zaidi unapopatikana, Biblia inathibitika tena na tena kuwa sahihi. * Wale wanaoiamini Biblia wana sababu nzuri ya kufanya hivyo. Maoni yao yanategemea uthibitisho wa kwamba Biblia ni sahihi kihistoria, kisayansi, na kinabii. Uthibitisho huo unawachochea kuamini jambo ambalo Biblia inasema, kwamba ni Neno la Mungu lililoongozwa kwa roho yake. (2 Timotheo 3:16) Tunakutia moyo uchunguze uthibitisho huo wewe mwenyewe. Huenda ukawa na maoni hayohayo.

[Maelezo ya Chini]

^ Kuna njia tofauti-tofauti za kuonyesha miaka. Katika makala hii, herufi K.W.K. zinamaanisha “Kabla ya Wakati wa Kawaida.”

^ Taarifa: Hakuna hata mmoja wa wataalamu ambao wametajwa katika makala hii ambaye anaamini kwamba jiji la Yerusalemu liliharibiwa mwaka wa 607 K.W.K.

^ Mwaka wa kupokea mamlaka haukuhesabiwa kuwa sehemu ya miaka ya utawala wa mfalme mpya; ulirejelea miezi iliyobaki katika mwaka mpaka mfalme mpya alipowekwa rasmi mamlakani.

^ Kuna mabamba ya mambo ya kibiashara kuhusu kipindi chote cha watawala wa Milki Mpya ya Babiloni. Miaka ya utawala wa wafalme hao inapojumlishwa na kuihesabu kurudi nyuma, kuanzia wakati wa Nabonido, mtawala wa mwisho wa Milki Mpya ya Babiloni, inaonekana kwamba jiji la Yerusalemu liliharibiwa mwaka wa 587 K.W.K. Hata hivyo, njia hiyo ya kuhesabu inaweza tu kuwa sahihi ikiwa kila mfalme alianza kutawala mwaka uleule ambao mfalme aliyemtangulia aliondoka, bila kipindi fulani kupita kati ya watawala hao.

^ Ili upate mifano hususa, ona sura ya 4 na ya 5 ya kitabu Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku/​Chati katika ukurasa wa 23]

 (Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

MAANDISHI YA MFUATANO WA MATUKIO KUHUSU BABILONI​—HISTORIA YENYE MAPENGO

Maandishi ya mfuatano wa matukio kuhusu Babiloni yanazungumzia miaka 35 tu ya kipindi cha Milki Mpya ya Babiloni, kilichowaziwa kuwa na urefu wa miaka 88.

MWAKA USIO NA MAANDISHI YA MFUATANO WA MATUKIO

MWAKA WENYE MAANDISHI YA MFUATANO WA MATUKIO

BM 21901 BM 21946 BM 35382

KIPINDI CHA MILKI

MPYA YA BABILONI WAAJEMI

Nabopolasa Nebukadneza wa Pili Amel-Marduk Nabonido

Neriglisa Labashi-Marduk

BM 25127 BM 22047 BM 25124

[Hisani]

BM 21901 and BM 35382: Photograph taken by courtesy of the British Museum; BM 21946: Copyright British Museum; BM 22047, 25124, 25127: © The Trustees of the British Museum

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 24]

MAANDISHI YA WATAALAMU WA NYOTA KWENYE BAMBA LA BM 32238

Bamba hili lina habari kuhusu matukio ya kupatwa kwa mwezi, lakini habari hizo ziliandikwa baada ya tukio la mwisho la kupatwa kwa mwezi, lililotokea miaka 400 hivi baada ya tukio la kwanza. Kwa kuwa mwandishi wa matukio hayo hakuyaona yote, huenda alifanya hesabu ili kuamua wakati matukio yaliyotangulia tukio la mwisho yalipotokea. Lakini bila uthibitisho unaounga mkono maamuzi yake, huenda matokeo ya hesabu zake yasiwe chanzo chenye kutegemeka kuhusu mfuatano wa matukio.

[Hisani]

© The Trustees of the British Museum

[Sanduku/​Picha katika ukurasa wa 26, 27]

BAMBA LA VAT 4956 LINASEMA NINI HASA?

Kwa nini kuna mabishano? Mstari wa tatu kwenye bamba hili unasema kwamba “usiku wa tarehe 9” katika mwezi wa kwanza (Nisanu/​Nisani), “mwezi ulikuwa umbali wa mkono mmoja mbele ya nyota ya ß Virginis.” Hata hivyo, katika mwaka wa 1915, Neugebauer na Weidner waliandika kuhusu mwaka wa 568 K.W.K. (ambao ungeonyesha kuwa jiji la Yerusalemu liliharibiwa 587 K.W.K.) kwamba “mwezi ulikuwa urefu wa mkono mmoja mbele ya nyota hiyo mnamo Nisani tarehe 8, na si Nisani tarehe 9.” (Italiki ni zetu.) Hata hivyo, mahali mwezi ulipokuwa panalingana kabisa na Nisani 9, mwaka wa 588 K.W.K., ambao unatuleta kwenye mwaka wa 607 K.W.K.

Je, ni siku ya 9 au ya 8?

(1) Kama inavyoonyeshwa kwenye picha iliyo hapa, alama ya Kiakadi iliyotumiwa badala ya nambari 9 inaonekana waziwazi.

(2) Wakati Neugebauer na Weidner walipotohoa maandishi hayo ya kikabari, walibadili nambari “9” ikawa “8.”

(3) Ni maelezo ya chini tu yanayoonyesha kulikuwa na nambari “9” kwenye maandishi ya awali.

(4) Hata katika tafsiri yao ya Kijerumani, waliweka nambari “8.”

(5) Katika mwaka wa 1988, Sachs na Hunger walichapisha maandishi hayo yakiwa na nambari “9,” bila kubadili chochote.

(6) Hata hivyo, katika tafsiri yao ya Kiingereza waliweka nambari “8” wakisema nambari “9” iliwekwa “kimakosa.”

[Hisani]

bpk/​Vorderasiatisches Museum, SMB/​Olaf M. Teßmer

[Picha katika ukurasa wa 28]

Marejeo Kuhusu “Jiji la Kale la Yerusalemu Liliharibiwa Mwaka Gani?—Sehemu ya Pili”

1. Maandishi ya kikabari yana umbo la kabari. Mwandishi aliweka alama mbalimbali kwenye bamba laini la udongo akitumia kifaa fulani kilichochongoka.

2. Kitabu Assyrian and Babylonian Chronicles, cha A. K. Grayson, kilichochapishwa mwaka 1975, chapa ya 2000, ukurasa wa 8.

3. Kipindi cha Milki Mpya ya Babiloni kilianza karne ya saba K.W.K., wakati watawala wa ukoo wa Wakaldayo walipotawala Milki ya Babiloni. Mtawala wa kwanza alikuwa Nabopolassar, baba ya Nebukadneza wa Pili. Kipindi hicho kiliisha wakati mfalme wa mwisho, Nabonido, alipoondolewa mamlakani na Mfalme Koreshi wa Uajemi mwaka wa 539 K.W.K.

4. Kitabu Neo-Babylonian Business and Administrative Documents, cha Ellen Whitley Moore, kilichochapishwa mwaka wa 1935, ukurasa wa 33.

5. Kitabu Archimedes, Volume 4, New Studies in the History and Philosophy of Science and Technology, “Observations and Predictions of Eclipse Times by Early Astronomers,” cha John M. Steele, kilichochapishwa mwaka wa 2000, ukurasa wa 36.

6. Kitabu Amel-Marduk 562-560 B.C.—A Study Based on Cuneiform, Old Testament, Greek, Latin and Rabbinical Sources. With Plates, cha Ronald H. Sack, kilichochapishwa mwaka wa 1972, ukurasa wa 3.

7. Mabamba ya BM 80920 na BM 58872 yaliandikwa mwezi wa nne na watano wa mwaka ambao Evil-merodach alipokea mamlaka. Mabamba hayo yalichapishwa na Sack katika kitabu Amel-Marduk 562-560 B.C.—A Study Based on Cuneiform, Old Testament, Greek, Latin and Rabbinical Sources. With Plates, ukurasa wa 3, 90, na 106.

8. Bamba lililo kwenye Jumba la Makumbusho la Uingereza (BM 55806) liliandikwa mwezi wa kumi, mwaka wa 43.

9. Mabamba ya BM 75106 na BM 61325 yaliandikwa mwezi wa saba na wa kumi wa kipindi kinachowaziwa kuwa mwaka wa mwisho (au wa pili) wa Mfalme Evil-merodach. Hata hivyo, bamba la BM 75489 liliandikwa mwezi wa pili wa mwaka wa kupokea mamlaka wa Neriglisa, aliyetawala baada yake.—Kitabu Catalogue of the Babylonian Tablets in the British Museum, Buku la 8, (Tablets From Sippar 3) cha Erle Leichty, J. J. Finkelstein, na C.B.F. Walker, kilichochapishwa mwaka wa 1988, ukurasa wa 25 na 35.

Kitabu Catalogue of the Babylonian Tablets in the British Museum, Buku la 7, (Tablets From Sippar 2) cha Erle Leichty na A. K. Grayson, kilichochapishwa mwaka wa 1987, ukurasa wa 36.

Kitabu Neriglissar—King of Babylon, cha Ronald H. Sack, kilichochapishwa mwaka wa 1994, ukurasa wa 232. Mwezi unaoonyeshwa kwenye bamba hili ni Ajaru (mwezi wa pili).

10. Fikiria mfano wa Neriglisa. Maandishi ya kifalme kumhusu yanasema kwamba alikuwa “mwana wa Bêl-shum-ishkun,” aliyekuwa “mfalme wa Babiloni.” (Italiki ni zetu.) Katika maandishi mengine anaitwa Bêl-shum-ishkun “mwana-mfalme mwenye hekima.” Neno la awali rubû, lililotafsiriwa “mwana-mfalme,” ni jina la cheo linalomaanisha “mfalme au mtawala.” Kwa kuwa kuna kutopatana kati ya kipindi cha utawala cha Neriglisa na mtangulizi wake, Amel-Marduk, je, inawezekana kwamba Bêl-shum-ishkun, anayeitwa “mfalme wa Babiloni,” alitawala kwa muda fulani kati ya wafalme hao wawili? Profesa R. P. Dougherty anasema kwamba “uthibitisho wa kwamba Neriglisa alikuwa wa ukoo wa kifalme hauwezi kupuuzwa.”—Nabonidus and Belshazzar—A Study of the Closing Events of the Neo-Babylonian Empire, cha Raymond P. Dougherty, kilichochapishwa mwaka wa 1929, ukurasa wa 61.

11. Kitabu Astronomical Diaries and Related Texts From Babylonia, Buku la 5, kilichosahihishwa na Hermann Hunger na kuchapishwa mwaka wa 2001, ukurasa wa 2-3.

12. Kitabu Journal of Cuneiform Studies, Buku la 2, Na. 4, 1948, “A Classification of the Babylonian Astronomical Tablets of the Seleucid Period,” cha A. Sachs, ukurasa wa 282-283.

13. Kitabu Astronomical Diaries and Related Texts From Babylonia, Buku la Tano, ukurasa wa 391.

14. Kitabu Mesopotamian Planetary Astronomy-Astrology, cha David Brown, kilichochapishwa mwaka wa 2000, ukurasa wa 164, 201-202.

15. Kitabu Bibliotheca Orientalis, L N° 1/2, Januari-Maart, 1993, “The Astronomical Diaries as a Source for Achaemenid and Seleucid History,” cha R. J. van der Spek, ukurasa wa 94, 102.

16. Kitabu Astronomical Diaries and Related Texts From Babylonia, Buku la Kwanza, cha Abraham J. Sachs, kilichokamilishwa na kusahihishwa na Hermann Hunger, kilichapishwa mwaka wa 1988, ukurasa wa 47.

17. Kitabu Babylonian Eclipse Observations From 750 BC to 1 BC, cha Peter J. Huber na Salvo De Meis, kilichochapishwa mwaka wa 2004, ukurasa wa 186. Kulingana na bamba la VAT 4956, tukio hili la kupatwa kwa mwezi lilitokea siku ya 15 ya mwezi wa tatu katika kalenda ya Babiloni, jambo linalodokeza kwamba mwezi wa Simanu ulianza siku 15 mapema. Ikiwa tukio hilo la kupatwa kwa mwezi lilitokea Julai 15, 588 K.W.K. kulingana na kalenda ya Yulio, basi siku ya kwanza ya mwezi wa Simanu ingekuwa Juni 30/Julai 1, 588 K.W.K. Kwa hiyo, mwezi wa (Nisanu) katika kalenda ya Babiloni ndio ungekuwa mwezi wa kwanza wa mwaka mpya ambao ungeanza miezi miwili mapema, mnamo Mei 2/3. Ingawa kwa kawaida mwaka wa tukio hilo la kupatwa kwa mwezi ungeanza Aprili 3/4, bamba la VAT 4956 linasema kwenye mstari wa 6 kwamba mwezi wa ziada uliongezwa baada ya mwezi wa (mwisho) wa 12 (Addaru) wa mwaka uliotangulia. (Bamba hilo linasema: “Siku ya 8 ya mwezi wa XII2 [mwezi 13].”) Kwa hiyo, mwaka mpya haungeanza mpaka Mei 2/3. Hivyo, tarehe hiyo ya kupatwa kwa mwezi katika mwaka wa 588 K.W.K. inalingana kabisa na maandishi ya bamba hilo.

18. Kulingana na Berichte über die Verhandlungen der Königl. Sächsischen Gesellschaft der Wissenschaften zu Leipzig (Ripoti Kuhusu Mazungumzo ya Taasisi ya Royal Saxonian Society of Sciences huko Leipzig); Buku la 67; Mei 1, 1915; katika makala “Ein astronomischer Beobachtungstext aus dem 37. Jahre Nebukadnezars II” (Maandishi ya Mtaalamu wa Nyota Kuhusu Mwaka wa 37 wa Nebukadneza wa Pili), cha Paul V. Neugebauer na Ernst F. Weidner, ukurasa wa 67-76, kuna rekodi 13 za uchunguzi wa mwezi ambazo zinaeleza mahali ambapo mwezi ulikuwa angani kwa kulinganishwa na nyota fulani au kundi la nyota. Pia, wameorodhesha rekodi 15 za uchunguzi wa sayari. (Ukurasa wa 72-76) Ingawa alama ya kikabari ya mwezi inaonekana waziwazi kabisa, alama nyingine za majina ya sayari na mahali zilipokuwa hazionekani vizuri. (Kitabu Mesopotamian Planetary Astronomy—Astrology, cha David Brown, kilichochapishwa mwaka wa 2000, ukurasa wa 53-57) Kwa sababu hiyo, mipangilio hiyo ya sayari inaweza kusababisha udadisi na kufasiriwa kwa njia tofauti-tofauti. Kwa kuwa mzunguko wa mwezi wakati uliopita unaweza kutambuliwa kwa urahisi na wataalamu wa nyota, sayari na nyota nyingine ambazo zimetajwa kwenye bamba la VAT 4956 na kuhusianishwa na mwezi zinaweza kutambuliwa. Pia, inawezekana kukadiria kwa usahihi wa kadiri fulani tarehe ambapo mipangilio hiyo ilitokea.

18a. Vipindi hivyo ni kipimo cha wakati, kwa mfano, kuanzia kuchomoza na kutua kwa mwezi katika siku ya kwanza ya mwezi na nyakati nyingine mbili baadaye katika mwezi. Wasomi wamelinganisha vipimo hivyo na tarehe kwenye kalenda. (Makala “The Earliest Datable Observation of the Aurora Borealis” iliyoandikwa na F. R. Stephenson na David M. Willis, katika kitabu Under One Sky—Astronomy and Mathematics in the Ancient Near East, kilichosahihishwa na John M. Steele na Annette Imhausen, kilichochapishwa mwaka wa 2002, ukurasa wa 420-428) Wataalamu wa kale wa nyota walihitaji saa ya aina fulani ili waweze kupima kipindi hicho cha wakati. Vipimo hivyo havikutegemeka. (Kitabu Archimedes, Volume 4, New Studies in the History and Philosophy of Science and Technology, “Observations and Predictions of Eclipse Times by Early Astronomers,” cha John M. Steele, kilichochapishwa mwaka wa 2000, ukurasa wa 65-66) Kwa upande mwingine, hesabu ya kuchunguza mahali ambapo mwezi ulikuwa angani kwa kulinganishwa na sayari na nyota nyingine, ilifanywa kwa uhakika zaidi.

19. Uchunguzi huu ulifanywa kwa kutumia programu fulani ya kompyuta iliyoitwa TheSky6™. Zaidi ya hayo, uchunguzi huu ulifanywa kwa makini zaidi kwa kutumia programu nyingine ya kompyuta inayoitwa Cartes du Ciel/Sky Charts (CDC), na pia programu ya kugeuza tarehe iliyotolewa na kituo cha kuchunguza anga cha jeshi la wanamaji la Marekani. Kwa kuwa alama za kikabari zinazoonyesha mipangilio ya sayari zinaweza kusababisha udadisi na kufasiriwa kwa njia tofauti-tofauti, mipangilio hiyo haikutumiwa katika uchunguzi huu ili kuonyesha mwaka hususa uliokusudiwa katika maandishi hayo ya wataalamu wa nyota.

20. Kitabu Berichte über die Verhandlungen der Königl. Sächsischen Gesellschaft der Wissenschaften zu Leipzig (Ripoti Kuhusu Mazungumzo ya Taasisi ya Royal Saxonian Society of Sciences huko Leipzig); Buku la 67; Mei 1, 1915; Kitabu“Ein astronomischer Beobachtungstext aus dem 37. Jahre Nebukadnezars II, (-567/66)” (Maandishi ya Uchunguzi wa Mtaalamu wa Nyota Kuhusu Mwaka wa 37 wa Utawala wa Nebukadneza wa Pili), cha Paul V. Neugebauer na Ernst F. Weidner, ukurasa wa 41.

21. Bamba la VAT 4956 linasema hivi kwenye mstari wa tatu: “Mwezi ulisimama umbali wa mkono mmoja [au digrii 2] mbele ya nyota ya ß Virginis.” Uchunguzi huu ambao ulikuwa umetajwa awali ulionyesha kwamba siku ya Nisanu 9, mwezi ulikuwa digrii 2 na nyuzi 04 mbele ya nyota ß Virginis na digrii 0 chini yake. Ilionekana kuwa vipimo hivyo vinalingana kabisa.

[Chati katika ukurasa wa 25]

 (Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

BAMBA LA VAT 4956 LINAONYESHA JIJI LA YERUSALEMU LILIHARIBIWA MWAKA GANI—587 K.W.K. AU 607 K.W.K.?

◼ Bamba hilo linataja matukio yanayohusiana na mpangilio wa mwezi na nyota ambayo yalitokea mwaka wa 37 wa utawala wa Nebukadneza wa Pili.

◼ Nebukadneza wa Pili aliharibu jiji la Yerusalemu katika mwaka 18 wa utawala wake.—Yeremia 32:1.

Ikiwa mwaka wa 568 K.W.K.,

ndio mwaka wa 37 wa Nebukadneza

wa Pili, basi jiji la

Yerusalemu liliharibiwa mwaka

wa 587 K.W.K.

587 ← ← katika 587 K.W.K.

610 K.W.K. 600 590 580 570 560

607 ← ← Ikiwa mwaka wa 588 K.W.K.,

ndio mwaka wake wa 37,

basi jiji la Yerusalemu

liliharibiwa mwaka wa 607 K.W.K.,

mwaka ambao unaonyeshwa katika

mfuatano wa matukio ya Biblia.

◼ Bamba la VAT 4956 linaonyesha waziwazi mwaka wa 607 K.W.K.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 22]

Photograph taken by courtesy of the British Museum