Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Barua ya Baraza Lenye Kuongoza

Barua ya Baraza Lenye Kuongoza

Kwa shahidi mwenzetu mupendwa:

Kama vile unajua, Biblia ni kitabu chenye kuzungumuzia sana maisha ya watu. Wengi kati yao walikuwa wanaume na wanawake waaminifu wenye walipata magumu kama yetu. Walikuwa na “hisia kama zetu,” ao walijisikia kama sisi. (Yakobo 5:17) Wamoja walipatwa na magumu na mahangaiko mbalimbali. Wengine walivunjwa moyo sana na watu wa familia yao ao na waabudu wenzao. Na wengine, zamiri zao ziliwaumiza kwa sababu ya makosa waliofanya.

Tunaweza kusema kwamba watumishi hao wa Yehova walimuacha kabisa? Hapana. Wengi walijisikia kama mutunga-zaburi aliyesali hivi: ‘Nimetanga-tanga kama kondoo aliyepotea. Umutafute mutumishi wako, kwa maana sijazisahau amri zako.’ (Zaburi 119:176) Wewe pia unajisikia hivyo?

Yehova hajasahau hata kidogo waabudu wake wenye wameacha kutaniko. Kwa hiyo, anawatafuta; mara nyingi anafanya hivyo kupitia Wakristo wenzao. Kwa mufano, wazia namna Yehova alimusaidia mutumishi wake Ayubu; mwanaume huyo alipata magumu mengi; alipoteza mali yake, watoto wake, na alipatwa na ugonjwa mubaya sana. Ayubu alivumilia pia maneno yenye kuumiza ya watu waliopaswa kumupatia nguvu ao kumufariji. Lakini hakumuacha Yehova hata kidogo, hata kama wakati fulani alikuwa na mawazo mabaya. (Ayubu 1:22; 2:10) Namna gani Yehova alimusaidia Ayubu akuwe tena na mawazo mazuri?

Yehova alimusaidia Ayubu kupitia mwabudu mwenzake, Elihu. Wakati Ayubu alieleza mahangaiko yake, Elihu alimusikiliza na kisha akazungumuza naye. Alimuambia nini? Alitumia maneno ya kumulaumu Ayubu ao kujaribu kumupatisha haya? Elihu alijiona kuwa mwaminifu sana kuliko Ayubu? Hapana. Roho ya Mungu ilimusukuma Elihu aseme hivi: ‘Mimi ni kama wewe tu mbele za Mungu wa kweli; mimi pia niliumbwa kwa udongo.’ Kisha akamuhakikishia Ayubu hivi: ‘Hofu yoyote (woga wowote) kutoka kwangu haitakutisha (haitakutetemesha), wala mukazo kutoka kwangu hautakuwa muzito juu yako.’ (Ayubu 33:6, 7) Kuliko kumuongezea Ayubu mateso mengine, Elihu alimupatia mashauri na kumutia moyo kwa upendo; hayo ndiyo mambo Ayubu alikuwa nayo lazima.

Tafazali, jua kama tulikuwa na mawazo hayohayo wakati tuliandika broshua hii. Kwanza tulisikiliza ndugu na dada fulani walioacha kutaniko; tulichunguza kwa uangalifu hali zao na mambo yenye ilifanya wafikie kuacha kutaniko. (Methali 18:13) Kisha tulisali na tulichunguza katika Maandiko habari za watumishi wa Yehova wa hapo zamani wenye walipatwa na hali hizo, na vile aliwasaidia. Mwishowe, tulilinganisha habari za maisha yao na habari za maisha ya watumishi wa Yehova wa leo ili kuandika broshua hii. Kwa hiyo, tunakuomba kwa furaha usome habari hizi. Tafazali, jua ya kama tunakupenda sana.

Baraza Lenye Kuongoza la Mashahidi wa Yehova