Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Hazina Iliyofichwa kwa Mamia ya Miaka

Hazina Iliyofichwa kwa Mamia ya Miaka

Mutu aliyesoma sana anashangaa na jambo ambalo anaona. Anachunguza kwa uangalifu sana tena na tena kipande cha maandishi ya zamani. Ufundi wa kuandika na mupangilio wa sarufi vinamusadikisha kwamba amepata sehemu za tafsiri ya Biblia ya zamani zaidi inayojulikana ya luga ya Kijojia!

HAZINA hiyo ilivumbuliwa mwishoni mwa Mwezi wa 12, mwaka wa 1922, wakati Ivané Javakhishvili, mujojia aliyesoma sana, alikuwa anatafuta habari juu ya namna alfabeti ao mupangilio wa herufi za luga ya Kijojia ilivyoanzishwa. Alipata kopi ya kitabu cha dini ya Wayahudi kinachoitwa Talmud ya Yerusalemu. Alipoichunguza, aliona chini ya maandishi ya Kiebrania maandishi fulani ya luga ya Kijojia ambayo yalikuwa yamefutwa juujuu tu. *

Maandishi hayo “yaliyofichwa” ambayo yangeweza kuonekana chini ya maandishi ya Talmud ilikuwa kopi ya sehemu ya kitabu cha Biblia cha Yeremia, kopi hiyo ilikuwa ya tangu kati ya mwaka wa 401 na 500 kisha kuzaliwa kwa Yesu. Mbele ya kuvumbua maandishi hayo, tafsiri ya Biblia ya zamani zaidi inayojulikana ya luga ya Kijojia ilikuwa ya tangu kati ya mwaka wa 801 na 900 kisha kuzaliwa kwa Yesu. Kisha hapo, sehemu za vitabu vingine vya Biblia za tangu kati ya mwaka wa 401 na 500 kisha kuzaliwa kwa Yesu ao hata mbele ya hapo zilipatikana. Wazia unavumbua maandishi ya Biblia yaliyoandikwa mamia ya miaka tu kisha wakati wa Yesu na mitume wake!

Ni nani aliyetafsiri maandishi hayo? Je, ilikuwa kazi ya mutu mumoja ao ya kikundi cha watafsiri waliojitoa? Mupaka sasa, hakuna habari za kihistoria ambazo zimevumbuliwa ili kujibu ulizo hilo. Kwa vyovyote vile, ni wazi kwamba Biblia, ao sehemu zake, ilitafsiriwa katika Kijojia mwanzoni mwa miaka kati ya 301 na 400 na kwamba Neno la Mungu limepatikana ao kujulikana kwa Wajojia katika luga yao ya asili tangu wakati huo.

Habari inayoonyesha ni kwa kadiri gani Wajojia walijua Maandiko inapatikana katika kitabu kimoja (The Martyrdom of St. Shushanik the Queen), ambacho labda kiliandikwa mwishoni mwa miaka kati ya 401 na 500. Anapoeleza habari yenye kuhuzunisha juu ya malkia, mwandikaji anataja neno kwa neno na kuzungumuzia maneno ya Zaburi, Injili, na sehemu zingine za Biblia. Anaeleza pia kwamba ili kutuliza mabwana wa Perse, bwana ya Shushanik anayeitwa Varsken, gavana ao liwali wa Ufalme wa Jojia wa Kartli, aliacha “Ukristo,” akawa muamini wa dini ya Zoroaster ya Kiperse, na akamuomba bibi yake pia aingie katika dini hiyo. Kulingana na kitabu hicho, Shushanik alikataa kuacha dini yake na akapata faraja kutokana na Maandiko mbele ya kuuawa.

Tangu kati ya mwaka wa 401 na wa 500 kisha kuzaliwa kwa Yesu, ni wazi kwamba kazi ya kutafsiri na kuchapisha Biblia katika luga ya Kijojia haijasimama. Uwingi wa maandishi ya Biblia katika luga ya Kijojia unaonyesha kazi ya bidii ya waandishi na watafsiri waliojitoa kabisa. Acheni tuzungumuzie mambo mawili kuhusu habari hiyo yenye kuvutia, ni kusema, kutafsiriwa na kuchapishwa kwa Biblia katika luga ya Kijojia.

BIBLIA ZINATAFSIRIWA KWA UWINGI

“Mimi, Giorgi, mutawa wa hali ya chini, nimetafsiri katika Kijojia kitabu hiki cha Zaburi kutoka katika Kigiriki kipya kwa bidii kubwa na kwa kujikaza sana.” Hayo ni maneno ya Giorgi Mtatsmindeli, mutawa Mujojia wa kati ya mwaka wa 1 001 na 1 100 kisha kuzaliwa kwa Yesu. Sababu gani kulikuwa uhitaji wa kutafsiri Biblia ijapokuwa Biblia ilikuwa imekwisha kutafsiriwa katika Kijojia kwa mamia fulani ya miaka?

Kuanzia kati ya mwaka wa 1001 na 1100, maandishi machache ya Biblia ya Kijojia yaliyoandikwa kwa mukono yalikuwa bado yanapatikana. Vitabu fulani vilikuwa vimekwisha kupotea kabisa. Pia, kwa njia fulani luga ilikuwa imebadilika, kwa hiyo ilikuwa vigumu kwa wasomaji kuelewa kopi za zamani sana. Ijapokuwa watafsiri wengi walijikaza kutafsiri upya Biblia ya Kijojia, kazi ya Giorgi ndiyo iliyokuwa ya maana zaidi. Alilinganisha tafsiri za Kijojia na maandishi ya Kigiriki na akatafsiri sehemu zilizokosekana, hata vitabu vizima-vizima. Muchana, alishugulika na kazi zake akiwa kiongozi wa makao ya watawa, na usiku alifanya kazi ya kutafsiri Biblia.

Ephrem Mtsire, aliyeishi wakati mumoja na Giorgi aliendeleza kazi ya Giorgi. Aliandika kitabu ambacho kilikuwa mwongozo kwa ajili ya watafsiri. Kitabu hicho kilikuwa na kanuni za musingi za utafsiri, kama vile kutafsiri kutokana na luga chanzo kadiri inavyowezekana na kufuata kwa ukaribu maandishi ya luga chanzo na hata hivyo kutafsiri namna watu wanaongea kwa ukawaida. Pia alianzisha ufundi wa kuandika maelezo ya chini na marejeo ya pembeni katika tafsiri za Kijojia. Ephrem alifanya tafsiri mupya kabisa ya vitabu vingi vya Biblia. Kazi ya Giorgi na Ephrem iliweka musingi wenye nguvu kwa ajili ya kazi kubwa ya kutafsiri ambayo ingefanywa baadaye.

Katika miaka 100 iliyofuata, vitabu viliandikwa kwa uwingi katika inchi ya Jojia. Masomo mbalimbali ya juu yalianzishwa katika muji wa Gelati na Ikalto. Watu wengi waliosoma sana wanaamini kwamba Biblia inayoitwa Biblia ya Gelati, ambayo kwa sasa inachungwa katika Kituo cha Kitaifa cha Jojia cha Kuwekea Maandishi ya Zamani, ni tafsiri mupya kabisa ya Biblia iliyofanywa na mumoja wa watu waliosoma sana wa muji wa Gelati ao Ikalto.

Namna gani kazi hiyo ya kutafsiri Biblia iliwasaidia watu wa Jojia? Kati ya mwaka wa 1101 na 1200, Shota Rustaveli, mwandikaji wa mashairi ao maandishi yaliyopangwa kwa utaratibu fulani, aliandika kitabu kinachoitwa Vepkhis-tqaosani (Shujaa Katika Ngozi ya Chui), kitabu ambacho kilikuwa na uvutano mwingi juu ya watu kwa mamia ya miaka hivi kwamba kiliitwa Biblia ya pili ya Wajojia. K. Kekelidze, Mujojia aliyesoma sana wa siku za leo anasema kwamba iwe mwandikaji huyo wa mashairi alitaja moja kwa moja mambo kutoka katika Biblia ao hapana, “maoni yake fulani yanaonyesha moja kwa moja mawazo ya maandiko mbalimbali ya Biblia.” Shairi ao maandishi hayo, ijapokuwa yalitilia mambo chumvi sana, yanazungumuzia mara kwa mara mambo kama vile urafiki wa kweli, ukarimu, kuheshimu wanawake, upendo usio na uchoyo kuelekea wageni. Kanuni hizo na kanuni zingine zinazofundishwa na Biblia ziliongoza sana namna ya kufikiri ya Wajojia kwa vizazi vingi na bado zinaendelea kuwaongoza katika namna yao ya kujiendesha.

KUCHAPISHA BIBLIA ILIKUWA KAZI YA KIFALME

Mwishoni mwa miaka kati ya 1601 na 1700, familia ya kifalme ya Jojia ilitaka sana Biblia ichapishwe. Kwa hiyo, Mufalme Vakhtang VI alijengesha kiwanda cha uchapishaji katika muji mukuu wa Jojia, Tbilisi. Hata hivyo, maandishi ya Biblia hayakuwa tayari ili kuchapishwa. Kwa njia fulani, ni kama vile Biblia ilifichwa tena katika luga ya Kijojia. Ni maandishi fulani tu yasiyoenea ya sehemu fulani za Biblia ndiyo yalipatikana, na luga iliyotumiwa ilikuwa ya zamani kabisa. Sulkhan-Saba Orbeliani, mutu mwenye elimu ya luga, ndiye aliyepewa kazi ya kufanya upya na kurudisha maandishi ya Biblia katika hali nzuri.

Orbeliani alianza kazi hiyo kwa uangalifu sana. Kwa sababu alijua luga nyingi, kutia ndani Kigiriki na Kilatini, aliweza kuchunguza maandishi mbalimbali ya zamani zaidi ya maandishi ya Kijojia yaliyopatikana wakati huo. Hata hivyo, mutazamo wake wa kusema mambo wazi haukufurahisha Kanisa la Ortodoksi. Viongozi wa kanisa walimushitaki kwamba anasaliti kanisa na walijaribu kumusadikisha mufalme amuzuie kuendelea na kazi ya kutafsiri Biblia. Kulingana na maandishi fulani ya Kijojia, viongozi wa kidini walimulazimisha Orbeliani achome Biblia ambayo alikuwa amefanyia kazi kwa miaka mingi!

Jambo la maana ni kwamba, kopi moja ya Maandishi ya Mtskheta (Mcxeta), inayojulikana kwa jina Biblia ya Saba, ambayo inaendelea kuonekana mupaka leo ina maelezo ya Orbeliani yaliyoandikwa kwa mukono. Hata hivyo, watu fulani wana mashaka kuhusu Biblia hiyo, hawaamini kwamba hiyo ndiyo Biblia ambayo viongozi wa kidini walishambulia. Watu wana uhakika kwamba ni habari tu zilizo katika nyongeza ndizo aliandika.

Ijapokuwa magumu, kazi ya kuchapisha Biblia iliendelea kuwa ya maana sana kwa watu fulani wa familia ya kifalme. Kati ya mwaka wa 1705 na 1711, sehemu fulani za Biblia zilichapishwa. Kwa sababu ya bidii ya Bakari na Vakhushti, wana wa kifalme wa inchi ya Jojia, Biblia nzima ilichapishwa katika mwaka wa 1743. Biblia haingeweza kufichwa tena.

^ Katika nyakati za zamani, vitu vilivyotumiwa kama karatasi ili kuandika juu yake havikupatikana kwa urahisi na vilikuwa vya bei kali. Kwa hiyo, ilikuwa kawaida kufuta maandishi ya kwanza yaliyoandikwa juu ya vitu hivyo na kuvitumia tena ili kuandika mambo mapya. Vitu hivyo vilivyotumiwa tena viliitwa palimpseste, kutokana na neno la Kigiriki linalomaanisha “kilichokwaruzwa tena.”

Kituo cha Kitaifa cha Kuwekea Maandishi ya Zamani