Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Mazungumuzo ya Biblia Pamoja na Jirani—Je, Watu Wote Wazuri Wanaenda Mbinguni?

Mazungumuzo ya Biblia Pamoja na Jirani—Je, Watu Wote Wazuri Wanaenda Mbinguni?

Mazungumuzo ya Biblia Pamoja na Jirani​—Je, Watu Wote Wazuri Wanaenda Mbinguni?

MASHAHIDI WA YEHOVA wanafurahia kuzungumuzia Biblia pamoja na majirani wao. Je, una ulizo fulani ambalo umekwisha kujiuliza juu ya Biblia? Je, ungependa kujua mengi juu ya mambo ambayo Mashahidi wa Yehova wanaamini ao juu ya mambo fulani wanayofanya? Ikiwa jibu ni ndiyo, usisite kuuliza jambo hilo wakati utakutana na Shahidi wa Yehova. Atafurahi kuzungumuzia jambo hilo pamoja nawe.

Habari inayofuata ni mufano wa mazungumuzo ambayo Shahidi wa Yehova fulani anaweza kuwa nayo pamoja na jirani yake. Kwa mufano, Shahidi fulani anayeitwa Marc anamukuta mutu anayeitwa Robert nyumbani kwake.

Wale Wanaoenda Mbinguni Watafanya Nini Huko?

Marc: Unapofikiria wakati ujao, je, unawaza kama hali ya ulimwengu itakuwa nzuri, itaharibika zaidi, ao itabaki namna ilivyo leo?

Robert: Ninawaza hali itakuwa nzuri. Ninangojea kuenda mbinguni ili kukaa pamoja na Bwana.

Marc: Hilo ni tumaini nzuri sana. Biblia inasema mambo mengi juu ya hali ya mbinguni na juu ya pendeleo la kuenda huko. Je, umekwisha kufikiria kwa uzito ikiwa wale wanaoenda mbinguni watafanya nini huko?

Robert: Ndiyo, tutakuwa pamoja na Mungu na kumusifu milele.

Marc: Hilo ni tumaini lenye kupendeza kabisa. Jambo lenye kufurahisha ni kwamba Biblia haizungumuzie tu mapendeleo ambayo wale wanaoenda mbinguni watakuwa nayo, lakini inazungumuzia pia kazi ya lazima ambayo watafanya huko.

Robert: Ni kazi gani?

Marc: Kazi ambayo watafanya inaonyeshwa katika andiko hili la Ufunuo 5:10. Linasema hivi: “Nawe [Yesu] ukawafanya kuwa ufalme na makuhani kwa Mungu wetu, nao watatawala wakiwa wafalme juu ya dunia.” Robert, unaona ni kazi gani ambayo wale wanaoenda mbinguni watafanya huko?

Robert: Andiko hilo linasema kama watakuwa wafalme na watatawala juu ya dunia.

Marc: Hilo ni wazo nzuri, sivyo?

Watatawala juu ya Nani?

Marc: Sasa, ikiwa watakuwa wafalme na watatawala, hauone kama kunapaswa kuwa watu ambao watatawaliwa? Wewe umekwisha kuona serikali ao guvernema isiyokuwa na raia?

Robert: Ninasikia wazo lako.

Marc: Kwa hiyo, ulizo nzuri la kuuliza ni hili, Watatawala juu ya nani?

Robert: Ninawaza tutatawala watu kwenye dunia ambao hawajakufa na kuenda mbinguni.

Marc: Ikiwa watu wote wazuri wanaenda mbinguni​—Hilo linaweza kuwa jambo nzuri. Lakini ona jambo lingine la kufikiria. Je, inawezekana kuwe na watu fulani wazuri ambao hawataenda mbinguni?

Robert: Sijue kama kuna Mukristo ambaye anaweza kuamini hivyo.

Marc: Ninauliza ulizo hilo kwa sababu ya maneno yaliyo katika andiko la Zaburi 37:29. Unaweza kusoma andiko hilo?

Robert: SAWA. Linasema hivi: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”

Marc: Asante. Unaona sasa mahali ambapo watu wengi wazuri wataishi?

Robert: Andiko hilo linasema kama wataishi juu ya dunia.

Marc: Ni vile kabisa​—na hawataishi kwenye dunia kwa muda mufupi tu. Unaona vizuri kama andiko hilo linasema “watakaa milele juu yake.”

Robert: Labda andiko hilo linapenda kusema kama watu wazuri watakuwa duniani sikuzote. Tunapokufa na kuenda mbinguni, watu wengine wazuri wanazaliwa na kuchukua mahali petu.

Marc: Hivyo ndivyo watu wengi wanaweza kufasiria andiko hilo. Lakini, je, unawaza andiko hilo linaweza kusemea mambo mawili kwa wakati mumoja? Linasema tu kama watu wazuri wataishi juu ya dunia hii milele, sivyo?

Robert: Sema, ninakusikiliza.

Paradiso Itakayokuwa Duniani Wakati Ujao

Marc: Sasa, ona yale andiko lingine la Biblia linasema juu ya namna maisha yatakavyokuwa duniani wakati ujao. Tusome Ufunuo 21:4. Juu ya watu ambao wataishi duniani wakati ujao, andiko hilo linasema hivi: “[Mungu] atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” Hilo ni tumaini nzuri kabisa, sivyo?

Robert: Ndiyo. Lakini ninawaza kama andiko hilo linazungumuzia namna maisha yatakavyokuwa huko mbinguni.

Marc: Ni kweli, wale wanaoenda mbinguni watapata baraka kama hizo. Lakini, angalia tena andiko hilo. Andiko hilo linasema nini juu ya kifo?

Robert: Linasema kama “kifo hakitakuwapo tena.”

Marc: Ni vile kabisa. Lakini niko hakika wewe pia unakubali kama, ili kitu fulani kisikuwe tena mahali fulani, inamaanisha kwamba kilikuwa hapo kwanza.

Robert: Ndiyo, ni vile.

Marc: Sasa, je, kifo kimewahi kuwa huko mbinguni? Ni hapa duniani tu ndipo watu wanakufa.

Robert: Hmm. Inaniomba kufikiri juu ya jambo hilo.

Marc: Robert, unaona, Biblia inafundisha kama watu fulani wazuri wataenda mbinguni lakini watu wengine wengi wataishi milele hapa duniani. Kwa kweli, niko hakika kama umekwisha kusikia maneno haya yenye kujulikana sana: “Heri wenye upole: maana wao watariti inchi.”​—Mathayo 5:5, La Sainte Bible en Swahili de la R.D. Congo.

Robert: Ndiyo, nimesikia andiko hilo likisomwa mara nyingi katika kanisa.

Marc: Ikiwa wapole watariti dunia, hilo linamaanisha kama watu wataishi duniani, sivyo? Wale watakaoishi duniani watapata baraka zilizoahidiwa katika kitabu cha Ufunuo. Wataona mabadiliko makubwa duniani kwa sababu Mungu ataondoa mambo yote mabaya​—hata kifo.

Robert: Ninaanza kukuelewa, lakini sizani kama andiko moja ao maandiko mawili tu ndio yanaweza kuonyesha kama unasema kweli.

Marc: Ni kweli, andiko moja ao maandiko mawili tu hayawezi kuhakikisha jambo hilo. Kuna maandiko mengi yanayozungumuzia namna maisha yatakavyokuwa duniani wakati ujao. Ikiwa una wakati, ninaweza kukuonyesha andiko moja kati ya maandiko ninayofurahia sana.

Robert: Ndiyo, ningali na dakika chache.

‘Mutu Muovu Hatakuwako Tena’

Marc: Tumesoma Zaburi ya 37 mustari wa 29. Turudilie tena Zaburi hiyo. Mara hiyo, tusome mustari wa 10 na 11. Utapenda kusoma mistari hiyo?

Robert: Ndiyo. ‘Na bado muda kidogo tu, na mutu muovu hatakuwako tena; nawe hakika utapaangalia mahali pake, naye hatakuwapo. Bali wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.’

Marc: Asante kwa usomaji. Kupatana na mustari wa 11, “wapole,” ao watu wazuri, wataishi wapi?

Robert: Andiko hilo linasema “wataimiliki dunia.” Lakini, ninaona kama andiko hilo linatimizwa leo; kwa sababu leo kuna watu wazuri wanaoishi duniani.

Marc: Ni kweli, Robert. Lakini, andiko hilo linasema pia kama watu wazuri watakuwa na “wingi wa amani.” Je, kuna amani duniani leo?

Robert: Hakuna amani.

Marc: Sasa, ahadi hiyo itatimizwa namna gani? Tufikirie mufano huu: Wazia unapangisha watu katika nyumba yako. Wapangaji fulani ni wazuri, wanatunza nyumba yako vizuri na wanajikaza kuishi vizuri pamoja na majirani. Utafurahia wapangaji hao, sivyo? Lakini wengine ni wapangaji wabaya; wanaharibu nyumba yako na wanawatendea vibaya majirani. Sasa, ikiwa wapangaji hao wabaya hawapende kubadilisha tabia yao, utafanya nini?

Robert: Nitawafukuza.

Marc: Hivyo ndivyo Mungu atawafanyia pia watu wabaya wanaotuzunguka leo. Turudilie tena mustari wa 10. Unasema hivi: ‘Mutu muovu hatakuwako tena.’ Ni kusema, Mungu “ataondoa” watu wanaowatendea wengine vibaya. Kisha ndipo watu wazuri wataweza kuishi duniani katika amani. Ninaona kama wazo hili la kusema watu wazuri wataishi milele duniani linatofautiana kabisa na mambo ambayo ulifundishwa zamani.

Robert: Ndiyo, sijasikia hata siku moja wazo hilo katika kanisa langu.

Marc: Na kama ulivyosema, andiko moja ao maandiko mawili tu hayatoshe. Kwa kweli, ni lazima tuchunguze mambo yote ambayo Biblia inasema juu ya maisha ya watu wazuri wakati ujao. Sasa, kupatana na maandiko ambayo tumesoma, je, unawaza inawezekana watu fulani wazuri waende mbinguni, na wengine wengi waishi milele hapa duniani?

Robert: Mimi siko hakika kabisa. Lakini kulingana na maandiko ambayo umetoka tu kusoma, inawezekana iwe hivyo. Ni lazima nifikirie tena jambo hilo kwa uzito.

Marc: Wakati utafikiria jambo hilo, labda kuna maulizo mengine ambayo unaweza kujiuliza. Kwa mufano, unaweza kujiuliza hivi: Itakuwa namna gani juu ya watu wazuri walioishi mbele yetu? Je, wote walienda mbinguni? Ikiwa hawakuenda mbinguni, wako wapi leo?

Robert: Hayo ni maulizo mazuri sana.

Marc: Labda ninaweza kukusaidia kwa njia mbili. Kwanza, acha nikuandikie maandiko fulani yanayoonyesha kama watu wote wazuri hawaende mbinguni. * Tena, ukiisha kusoma maandiko hayo na kuyafikiria, nitafurahi kurudia ili tuyazungumuzie. Unaona namna gani?

Robert: Ndiyo, ni sawa kabisa. Asante Marc.

[Maelezo ya chini]