Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Namna ya Kuishi Unapopungukiwa na Feza

Namna ya Kuishi Unapopungukiwa na Feza

Namna ya Kuishi Unapopungukiwa na Feza

OBED ni baba wa watoto wawili wanaume. Alitumika kwa muda wa miaka kumi katika hoteli nzuri sana huko Nairobi na hakuwa na magumu ya kutolea watu wa familia yake vitu walivyohitaji. Mara kwa mara, alipeleka familia yake kwenye mapumziko mahali ambapo wanyama wanafugwa katika inchi yao. Mambo hayo yote yalikwisha wakati alipoteza kazi yake kwa sababu hawakuwa wakipata tena watu wengi katika hoteli.

Kisha kutumika kwa muda wa miaka zaidi ya 22 kwenye banki fulani kubwa, Stephen alipandishwa cheo, akawa mumoja wa wasimamizi wa banki hiyo. Alipata faida nyingi kwenye kazi hiyo, ni kusema, nyumba kubwa, motokari, watumishi wa nyumbani, na watoto wake walisomea kwenye masomo yenye sifa sana mahali walipoishi. Wakati banki ilipunguza wafanyakazi, Stephen alipoteza pia kazi yake. Alisema hivi: “Mimi na familia yangu tulivurugika sana. Nilivunjika moyo sana kwa sababu nilikosa tumaini, nilikuwa na uchungu moyoni, na niliogopa sana.”

Mambo kama hayo yanawafikia watu wengi. Kwa sababu ya matatizo ya feza yanayoendelea duniani, watu wengi sana waliokuwa na mishahara mizuri wamepoteza kazi zao. Watu wengi ambao wanapata kazi wanakubali mushahara mudogo ijapokuwa bei ya vitu inaendelea kupanda. Inchi zote duniani, iwe inchi zenye kuendelea ao inchi masikini, zote zinakumbwa na matatizo ya feza.

Utumie Hekima

Ikiwa tunapoteza kazi yetu ao tunapungukiwa na feza, tunaweza kusumbuliwa kwa vyepesi na mawazo yasiyofaa. Kwa kweli, hakuna mutu ambaye anakosa hata hangaiko ndogo. Ndiyo maana Sulemani, mutu aliyekuwa na hekima sana alisema hivi: “Je, umejionyesha kuwa umevunjika moyo siku ya taabu? Nguvu zako zitakuwa chache.” (Methali 24:10) Kuliko kuogopa sana tunapopata magumu ya feza ao tunapopoteza kazi, tunahitaji kufanya kama vile Neno la Mungu linavyotushauria, ni kusema, ‘kujiwekea hazina ya hekima.’​—Methali 2:7.

Hata ikiwa Biblia si kitabu kinachofundisha mambo ya feza, kanuni zake zimesaidia watu wengi sana duniani pote kupambana na matatizo ya feza. Acheni tuzungumuzie kanuni fulani.

Uhesabu garama. Ona maneno ambayo Yesu alisema kwenye Luka 14:28: ‘Ni nani kati yenu anayetaka kujenga munara ambaye haketi kwanza na kuhesabu garama, ili aone kama ana kiasi cha kutosha kuukamilisha?’ Kutumia kanuni hiyo kunaweza kunamaanisha kupanga namna utatumia feza zako na kuepuka kununua vitu ambavyo haukupanga kununua. Lakini, kama Obed alivyosema, inaweza kuwa vigumu kufanya hivyo. Alisema hivi: “Mbele ya kupoteza kazi yangu, tulikuwa tunanunua​-nunua vitu kwenye magazini kubwa, hata vitu ambavyo hatukuhitaji kabisa. Hatukuwa na lazima ya kupanga namna ya kutumia feza zetu kwa sababu tulikuwa na feza nyingi ili kununua kitu chochote tulichotaka.” Kupanga mbele ya wakati namna ya kutumia feza ndogo unazopata sasa kunaweza kukusaidia ununue vitu ambavyo familia yako inahitaji kabisa.

Ukubali hali mupya. Kwa kweli, si vyepesi kuzoelea maisha ya hali ya chini, lakini ni jambo la lazima kukubali sasa hali hiyo. Methali moja ya Biblia inasema hivi: ‘Mutu mwerevu anaona musiba na kujificha.’ (Methali 22:3) Tafsiri zingine za Biblia zinatumia maneno ‘kulala chini ao kujishusha’ badala ya ‘kujificha.’ Stephen anasema hivi: “Ili kupunguza garama, mimi na familia yangu tulihamia katika nyumba yetu wenyewe, ijapokuwa ilikuwa ndogo na ilikuwa haijamalizika. Tulihamishia watoto kwenye masomo ambayo haikulipisha feza nyingi lakini ambako walimu walifundisha vizuri.”

Kuzungumuza pamoja katika familia ni jambo la lazima ili kukubali hali mupya. Austin, aliyetumika miaka 9 kwenye banki fulani mbele ya kupoteza kazi yake anasema hivi: “Mimi na bibi yangu tulikaa na kuandika vitu vyote ambavyo tulihitaji kabisa. Tuliacha kununua vyakula vingine vya bei tulivyokuwa tukinunua, mavazi ya bei sana, na tuliacha kwenda kwenye mapumziko yanayoomba feza nyingi. Ninafurahi sana kwa sababu bibi yangu na watoto wetu walikubali mabadiliko hayo.” Kwa kweli, labda watoto hawawezi kabisa kuelewa sababu gani mabadiliko hayo ni ya lazima, lakini wazazi wanaweza kuwasaidia kuelewa jambo hilo.

Ukubali kazi yoyote. Ikiwa umezoea kutumika kazi za biro, inaweza kuwa vigumu kufanya kazi ya mikono. Austin anasema hivi: “Ilikuwa vigumu kwangu kukubali kazi za hali ya chini, kwa sababu nilikuwa na cheo kwenye banki kubwa.” Hilo si jambo lenye kushangaza kwa sababu Biblia inasema hivi katika andiko la Methali 29:25: ‘Kutetemeshwa na wanadamu ndiko kunaleta mutego.’ Kuwaza​-waza juu ya yale ambayo wengine watasema hakutakupatia feza za kulisha familia yako. Basi, ni nini linaloweza kukusaidia usiwe na mawazo yasiyofaa?

Siri ni kuwa munyenyekevu. Wakati Obed alipopoteza kazi yake kwenye hoteli, mufanyakazi mwenzake wa zamani alimuomba ajiunge naye katika kazi ya kutengeneza motokari (magari). Kazi hiyo ilimuomba Obed kufanya safari ndefu kwa miguu katika barabara yenye vumbi ili kutafuta rangi ya kupakala motokari na vifaa vingine. Obed anasema hivi: “Sikupenda kazi hiyo kabisa lakini sikupata kazi nyingine ya kufanya. Sifa ya unyenyekevu ilinisaidia kukubali kufanya kazi hiyo hata ikiwa mushahara wa sasa ulikuwa mudogo mara ine kuliko mushahara wangu wa zamani, lakini ilikuwa ya lazima kwangu ili niwatolee watu wa familia yangu vitu walivyohitaji.” Je, unaweza kuwa na maoni kama yale ya Obed?

Ujifunze kutosheka. Kamusi moja inaeleza kama mutu mwenye kutosheka ni mutu ambaye “kwa kiasi fulani anatosheka na kufurahia namna mambo yalivyo.” Kwa kweli, ni vigumu mutu aliye na matatizo ya feza atosheke na kufurahi kwa kiasi fulani. Lakini, ona maneno ya mutume Paulo, misionere aliyejua maana ya kupungukiwa. Alisema hivi: “Nimejifunza kuwa mwenye kujitosheleza katika hali zozote nilizo nazo. Kwa kweli najua jinsi ya kupungukiwa na vyakula, kwa kweli najua jinsi ya kuwa na wingi.”​—Wafilipi 4:11, 12.

Labda hali yetu ni nzuri leo, lakini kesho mambo yanaweza kubadilika na kufanya hali yetu iwe mbaya zaidi. Ikiwa hali yetu inabadilika, tunaweza kufaidika kabisa ikiwa tunachukua kwa uzito shauri hili la Paulo lililoongozwa na roho: ‘Kwa hakika, hiyo ni njia ya kupata faida kubwa, ujitoaji-kimungu pamoja na ujitoshelevu. Kwa hiyo, tukiwa na chakula na kitu cha kujifunika, [tutatosheka] na vitu hivyo.’ Mutume Paulo hakushauria watu wawe wavivu; kupitia maneno hayo, alionyesha namna ya kutia mambo ya kimwili pa nafasi inayofaa.​—1 Timotheo 6:6, 8.

Kupata Furaha ya Kweli

Furaha ya kweli haitokane na kujikusanyia kila kitu tunachotaka wala kuishi maisha ya raha-raha. Yesu mwenyewe alisema hivi: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” Kwa kweli, tunapata furaha na tunatosheka wakati tunatumia vitu tulivyo navyo ili kuwasaidia wengine na kuwatia moyo.​—Matendo 20:35.

Yehova Mungu, Muumbaji wetu, anajua vizuri zaidi mambo yote tunayohitaji. Katika Neno lake Biblia, anatutolea mashauri yanayofaa ambayo yamesaidia watu wengi sana wawe na maisha mazuri na wasihangaike kupita kiasi. Hilo halimaanishe kama kutumia kanuni hizo kutafanya hali ya mutu ibadilike mara moja ikiwa ana matatizo ya feza. Lakini Yesu aliwahakikishia wale wanaoendelea ‘kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wa Mungu’ kama wataongezewa mahitaji yao ya kila siku.​—Mathayo 6:33.