Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

MAONI YA BIBLIA

Ponografia

Ponografia

Je, Biblia inashutumu ponografia?

“Kila mtu ambaye anaendelea kumtazama mwanamke na kumtamani tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake.” —Mathayo 5:28.

KWA NINI SWALI HILO NI MUHIMU

Leo ponografia (picha au habari za ngono) inapendwa sana na inapatikana kwa urahisi zaidi kuliko zamani. Ikiwa unataka kumpendeza Mungu na kuishi maisha yenye furaha, unapaswa kujua maoni ya Mungu kuhusu ponografia.

BIBLIA INASEMA NINI?

Biblia haitaji ponografia moja kwa moja. Hata hivyo, kutazama ponografia kunapingana na kanuni nyingi za Biblia.

Kwa mfano, Biblia inaonya waziwazi kwamba mwanamume aliyeoa ‘anapoendelea kumtazama mwanamke’ ambaye si mke wake na kukuza tamaa ya kufanya ngono naye, jambo hilo linaweza kuongoza kwenye uzinzi. Kanuni iliyo kwenye maneno hayo ya Biblia inaweza kumhusu mtu yeyote, iwe ameoa au ni mseja, ambaye ‘anaendelea kutazama’ picha za ponografia akiwa na tamaa ya kujihusisha katika matendo machafu kingono. Ni wazi kwamba tabia hiyo humchukiza Mungu.

Je, ponografia ni mbaya hata ikiwa haitamwongoza mtu kufanya mambo machafu kingono?

“Viueni viungo vya mwili wenu . . . kwa habari ya uasherati, uchafu, hamu ya ngono, tamaa yenye madhara, na kutamani.”Wakolosai 3:5.

WATU HUSEMA NINI?

Watafiti fulani wanapinga kwamba ponografia inaweza kumwongoza mtu kufanya matendo ya kingono yenye kuchukiza. Lakini je, kweli ponografia ni mbaya hata kama haitamwongoza mtu kufanya uasherati?

BIBLIA INASEMA NINI?

Biblia inasema kwamba “mizaha michafu” ni ukosefu wa maadili. (Waefeso 5:3, 4) Basi ponografia inawezaje kuwa jambo lisilochukiza? Leo, ponografia hutia ndani picha zilizorekodiwa za matendo halisi ya uzinzi, ngono kati ya watu wa jinsia moja, na matendo mengine ya uasherati. Kwa kweli, kufurahia kutazama matendo machafu ya kingono kama hayo kunamchukiza Mungu zaidi kuliko usemi mchafu.

Watafiti wanaendelea kujadiliana kuhusu uwezekano wa mtu kutenda mambo anayotazama kwenye ponografia. Lakini Biblia inaunga mkono wazo la kwamba kutazama ponografia ni jambo linaloharibu uhusiano wa mtu na Mungu na linamchukiza sana Mungu. Biblia inatoa himizo hili: “Kwa hiyo, viueni viungo vya mwili wenu . . . kwa habari ya uasherati [na] hamu ya ngono.” (Wakolosai 3:5) Watu wanaotazama ponografia hufanya kinyume—badala ya kuua tamaa hizo, wanazikuza na kuzichochea.

Ni nini kinachoweza kukusaidia kuepuka kutazama ponografia?

“Tafuteni yaliyo mema, wala si yaliyo mabaya . . . Chukieni yaliyo mabaya, pendeni yaliyo mema.”​—Amosi 5:14, 15.

BIBLIA INASEMA NINI?

Biblia inazungumza kuhusu watu waliokuwa na maadili mapotovu, walevi, na wezi, ambao walifaulu kuacha tabia hizo zenye madhara. (1 Wakorintho 6:9-11) Walifauluje? Kwa kutumia hekima inayopatikana katika Neno la Mungu, Biblia, wamejifunza kuchukia mabaya.

Inawezekana kujifunza kuchukia ponografia kwa kufikiria kwa uangalifu matokeo mabaya ya zoea hilo lenye kudhuru. Uchunguzi wa hivi karibuni uliochapishwa na Chuo Kikuu cha Jimbo la Utah ulionyesha kwamba baadhi ya watu wanaotazama ponografia “hushuka moyo, hujitenga na watu, huharibu mahusiano yao na watu wengine,” na hupatwa na matokeo mengine yenye kusikitisha. Isitoshe, kama ilivyoelezwa awali, kwa kuwa kutazama ponografia humchukiza Mungu, kunaleta madhara mengine mabaya hata zaidi. Kunawazuia wanadamu wasiwe rafiki za Muumba.

Biblia inaweza kutusaidia kujifunza kupenda mema. Kadiri tunavyosoma Biblia, ndivyo tutakavyozidi kupenda viwango vyake vya maadili. Upendo huo utatusaidia kukataa kabisa ponografia na kuhisi kama mtunga-zaburi aliyeandika hivi: “Sitaweka mbele ya macho yangu kitu chochote kisichofaa.”—Zaburi 101:3.