Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI KUU

Jinsi ya Kuwa Baba Mzuri

Jinsi ya Kuwa Baba Mzuri

“Kwani nilikosea wapi?” Swali hilo lilimsumbua sana Michael, * anayeishi Afrika Kusini. Ingawa alijitahidi sana kuwa baba mzuri, kila mara alipofikiria kuhusu mwana wake mwenye umri wa miaka 19 aliyeasi, alijiuliza ikiwa alifanya yote aliyoweza ili kuwa mzazi mzuri.

Kwa upande mwingine, inaonekana kwamba Terry, anayeishi Hispania amefaulu kuwa baba mzuri. Andrew, mwana wake, anasema hivi: “Baadhi ya mambo ninayokumbuka kuhusu maisha yangu ya utotoni ni baba yangu akinisomea, akicheza nami, na tukienda matembezi pamoja ili tu mimi na yeye tuwe pamoja. Alinifanya nifurahie kujifunza.”

Ni kweli kwamba si rahisi kuwa baba mzuri. Lakini kuna kanuni za msingi ambazo zinaweza kukusaidia. Akina baba wengi wamegundua kwamba wao na familia zao hunufaika sana wanapofuata hekima iliyo katika Biblia. Acheni tuchunguze baadhi ya mashauri yanayopatikana katika Biblia ambayo yanaweza kuwasaidia akina baba.

1. Tenga Wakati wa Kuwa Pamoja na Familia Yako

Wewe baba unaonyeshaje kwamba watoto wako ni muhimu? Bila shaka kuna mambo mengi ambayo wewe huwafanyia watoto wako, kutia ndani kujinyima mambo fulani ili kuwapa chakula na makao yanayofaa. Hungefanya mambo hayo ikiwa watoto wako si muhimu kwako. Hata hivyo, ikiwa hutumii wakati wa kutosha pamoja na watoto wako, huenda wakaona kwamba kazi yako, marafiki wako, au mambo unayopenda kufanya ni muhimu kuliko wao.

Baba anapaswa kuanza kutenga wakati wa kuwa pamoja na watoto wake wanapokuwa na umri gani? Mama huanza kuwa na uhusiano na mtoto wake anapokuwa bado tumboni. Majuma 16 hivi baada ya mimba kutungwa, mtoto aliye tumboni anaweza kusikia. Wakati huo, baba pia anaweza kuanza kujenga uhusiano wa pekee pamoja na mtoto wake ambaye bado hajazaliwa. Anaweza kusikiliza mapigo ya moyo wa mtoto, kumsikia akicheza, kuzungumza naye, na kumwimbia.

Kanuni ya Biblia: Katika nyakati za Biblia, wanaume walipaswa kuwafundisha watoto wao. Akina baba walitiwa moyo watumie wakati na watoto wao kwa ukawaida, kama inavyoonyeshwa na Biblia kwenye andiko la Kumbukumbu la Torati 6:6, 7, linalosema hivi: “Maneno haya ninayokuamuru leo lazima yawe moyoni mwako; nawe uyakazie kwa mwana wako na kuyasema unapoketi katika nyumba yako na unapotembea barabarani na unapolala na unapoamka.”

2. Baba Wazuri Wanajua Jinsi ya Kuwasiliana

Sikiliza kwa utulivu bila kuhukumu

Ili uwasiliane kwa njia nzuri na watoto wako, lazima uwe msikilizaji mzuri. Unapaswa kusitawisha uwezo wa kusikiliza kwa utulivu.

Ikiwa watoto wako watahisi kwamba utakasirika na kuwahukumu, hawatajihisi huru kukueleza yaliyo moyoni. Lakini ukisikiliza kwa utulivu, unawaonyesha kwamba unawajali kikweli. Ukifanya hivyo, yaelekea watakuambia mawazo na hisia zao za ndani.

Kanuni ya Biblia: Hekima inayopatikana katika Biblia imethibitika kuwa yenye manufaa katika sehemu nyingi za maisha. Kwa mfano, Biblia inasema: “Kila mtu lazima awe mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema, si mwepesi wa ghadhabu.” (Yakobo 1:19) Akina baba wanaofuata kanuni hiyo ya Biblia hufanikiwa kuwasiliana na watoto wao kwa njia nzuri.

3. Toa Nidhamu kwa Upendo na Uwapongeze

Hata wakati ambapo unahisi umekasirika, nidhamu unayotoa inapaswa kuonyesha kwamba unampenda mtoto na unajali maisha yake ya siku zijazo. Nidhamu inatia ndani kumshauri, kumrekebisha, kumwelimisha, na kumwadhibu inapohitajika.

Isitoshe, nidhamu inakuwa na matokeo zaidi ikiwa baba ana zoea la kuwapongeza watoto wake. Methali ya kale inasema hivi: “Neno linalosemwa wakati unaofaa ni kama matunda ya mtofaa ya dhahabu kwenye chombo cha fedha kilichopambwa.” (Methali 25:11) Pongezi humsaidia mtoto kukuza sifa nzuri. Watoto hujiheshimu wanapoona kwamba wazazi wao wanawajali na kuwathamini. Baba anayetumia kila fursa kuwapongeza watoto wake atawasaidia wajiheshimu na kuwachochea kutenda yaliyo sawa.

Kanuni ya Biblia: “Enyi akina baba, msiwe mkiwakasirisha watoto wenu, ili wasivunjike moyo.”Wakolosai 3:21.

4. Mpende na Kumheshimu Mke Wako

Jinsi baba anavyomtendea mke wake kutakuwa na uvutano mzuri au mbaya kwa watoto wake. Wataalamu wa ukuzi wa mtoto wanasema hivi: “Mojawapo ya mambo bora ambayo baba anaweza kuwafanyia watoto wake ni kumheshimu mama yao. . . . Baba na mama wanaoheshimiana na kuacha watoto wao waone jambo hilo huwafanya watoto wawe na furaha na wahisi wanapendwa.”—The Importance of Fathers in the Healthy Development of Children. *

Kanuni ya Biblia: “Enyi waume, endeleeni kuwapenda wake zenu, . . . Kila mtu mmoja-mmoja kati yenu na ampende hivyo mke wake kama vile anavyojipenda mwenyewe.”Waefeso 5:25, 33.

5. Tumia Hekima Kutoka kwa Mungu

Akina baba wanaompenda Mungu kutoka moyoni wanaweza kuwapa watoto wao urithi wenye thamani, yaani, uhusiano wa karibu pamoja na Baba yao wa mbinguni.

Baada ya kufanya kazi ngumu ya kuwalea watoto wake sita kwa miaka mingi, Antonio, ambaye ni Shahidi wa Yehova alipokea barua hii kutoka kwa mmoja wa binti zake: “Baba mpendwa, nilitaka kukushukuru kwa kunilea na kunifundisha kumpenda Yehova Mungu, kujipenda mwenyewe, na kumpenda jirani yangu, yaani, ulinisaidia kuwa mtu mwenye usawaziko. Ulinionyesha kwamba unampenda Yehova na kwamba unanijali. Asante Baba kwa kumtanguliza Yehova maishani mwako na kuwaona watoto wako kuwa zawadi kutoka kwa Mungu!”

Kanuni ya Biblia: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa nguvu zako zote. Na maneno haya ninayokuamuru leo lazima yawe moyoni mwako.”—Kumbukumbu la Torati 6:5, 6.

Ni wazi kwamba kuwa baba kunahusisha mengi zaidi ya mambo hayo matano, na hata ukijitahidi kiasi gani, hutakuwa baba mkamilifu. Lakini ukijitahidi kutumia kanuni hizo kwa upendo na usawaziko, unaweza kuwa baba mzuri. *

^ Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

^ Hata ikiwa baba hana tena uhusiano wa ndoa pamoja na mama ya watoto wake, ingefaa amtendee kwa njia ya heshima na staha ili watoto wawe na uhusiano mzuri pamoja na mama yao.

^ Kwa mwongozo zaidi kuhusu maisha ya familia, soma kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia, ambacho kinapatikana kwenye Tovuti ya www.jw.org/sw.