Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

MASIMULIZI KUHUSU MAISHA YA WATU

Macho ya Jairo—Yanamusaidia Kutumikia Mungu

Macho ya Jairo—Yanamusaidia Kutumikia Mungu

Wazia hauna uwezo wa kuongoza mwili wako isipokuwa tu macho yako. Ndugu yangu Jairo iko na tatizo hilo. Lakini maisha yake ni yenye maana. Mbele nifasirie sababu gani anaona maisha yake kuwa yenye maana, acha nieleze kwanza habari ya maisha yake.

Jairo alizaliwa na aina fulani ya ugonjwa wa kupooza ubongo wenye kufanya pia mikono na miguu ipooze. * Hilo linafanya ashindwe kuongoza sehemu nyingi za mwili wake. Ubongo wake hauwezi kutuma ujumbe wenye kuwa wazi kwenye misuli yake, kwa hiyo mikono na miguu yake inajinyonga, ao kujikunja-kunja kwa maumivu, bila kuzuiliwa. Wakati fulani, kujikunja-kunja hivyo bila kutazamia kunafanya Jairo hata ajiumize. Watu wenye kuwa karibu yake wanaweza pia kuumizwa ikiwa hawako waangalifu. Inahuzunisha kuwa kila mara inaomba kufunga mikono na miguu yake kwenye kiti chake cha magurudumu ili kuepuka hatari hizo.

AMEKOMAA KWA MAUMIVU

Jairo amekomaa kwa maumivu mengi sana. Wakati alikuwa na miezi tatu, alianza kupata kifafa chenye kilikuwa kinamufanya apoteze ufahamu. Mara nyingi, mama alimubana sana na kumukimbizia kwenye hopitali, akiwa hakika kuwa amekufa.

Kisha wakati fulani, umbo la mifupa ya Jairo lilibadilika kwa sababu ya kubanwa na kukazwa sana. Wakati alikuwa na miaka 16, nyonga (bassin) yake iliteguka na hilo liliomba afanyiwe upasuaji mukubwa kwenye paja (cuisse), kiuno, na nyonga. Ningali ninakumbuka namna Jairo alikuwa analalamika kila usiku kwa sababu ya maumivu alikuwa nayo mbele ya kupona.

Ulemavu mubaya sana wa Jairo unamufanya ategemee kabisa watu wengine katika mambo mbalimbali ya maisha, kwa mufano, kula, kuvaa, na kupanda kwenye kitanda. Kwa kawaida Baba na Mama ndio wanamusaidia kufanya mambo hayo. Hata ikiwa Jairo iko na lazima ya musaada kila wakati, wazazi wetu wanamukumbusha kama maisha yake hayategemee tu watu lakini yanategemea pia Mungu.

ANAPATA NAMNA YA KUZUNGUMUZA

Wazazi wetu ni Mashahidi wa Yehova, na wamekuwa wakimusomea Jairo hadisi za Biblia tangu wakati alikuwa mutoto. Sikuzote, wamejua kuwa maisha yanakuwa na maana zaidi wakati mutu anafanya urafiki na Mungu. Jairo iko na mwili zaifu wenye kushituka-shituka, lakini aliweza kuwa na tumaini la muzuri na lenye nguvu juu ya wakati unaokuja. Hata hivyo, mara kwa mara wazazi wetu walijiuliza ikiwa Jairo atafikia kuelewa mafundisho ya Biblia.

Siku moja, wakati Jairo alikuwa mutoto, Baba alimuuliza, “Jairo, tafazali unaweza kuongea na mimi?” Kisha Baba akaongeza, “Ikiwa unanipenda kweli, utaongea na mimi!” Wakati Baba alikuwa anamubembeleza aseme hata neno moja, Jairo akaanza kulia. Alijikaza kusema maneno fulani ili kueleza namna alikuwa anajisikia moyoni, lakini aliweza tu kutoa sauti zisizoeleweka kwenye koo. Baba alijisikia mubaya sana kuona alimulilisha Jairo. Lakini namna Jairo alitenda ilionyesha kama alisikia mambo Baba alisema. Shida ni kwamba hangeweza kusema.

Kisha muda mufupi, wazazi wetu walitambua kuwa wakati fulani Jairo alikuwa anazungusha macho haraka-haraka, hilo lilionyesha kama alikuwa anajaribu kuonyesha mawazo yake na namna alijisikia moyoni. Jairo alivunjika moyo kwa sababu kila mara hangeweza kufanya wengine wamuelewe. Lakini wakati wazazi wangu walielewa alama za macho yake na kumupatia kile anatafuta, uso wa Jairo ulikuwa wenye furaha sana. Hiyo ilikuwa namna yake ya kusema asante.

Munganga mumoja anayesaidia watu kusema alituambia kuwa ili kuzungumuza na Jairo muzuri, tukuwe tunainua mikono yetu yote mbili juu wakati wa kumuuliza ulizo la kujibu ndiyo ao hapana. Mukono wa kuume unamaanisha ndiyo, na mukono wa kushoto unamaanisha hapana. Kwa hiyo, angeonyesha kile anataka kwa kukazia macho mukono wenye kufaa.

ANAFANYA JAMBO LA MAANA SANA KATIKA MAISHA YAKE

Mara tatu kwa mwaka, Mashahidi wa Yehova wanafanya mikusanyiko. Kwenye mikusanyiko hiyo watu wengi wanasikiliza hotuba zenye kutegemea Biblia. Sikuzote, Jairo alifurahia sana hotuba iliyotolewa kwa ajili ya wale wenye watabatizwa. Siku moja, wakati Jairo alikuwa na miaka 16, Baba alimuuliza, “Jairo, unapenda kubatizwa?” Mara moja, aliangalia sana mukono wa kuume wa Baba ili kuonyesha kuwa alikuwa anapenda kabisa kubatizwa. Kisha Baba akaongeza, “Umeamuahidi Mungu katika sala kama unataka kumutumikia maisha yako yote?” Tena Jairo aliangalia sana kwenye mukono wa kuume wa Baba. Hilo lilionyesha wazi kama Jairo alikuwa tayari ametoa maisha yake kwa Yehova.

Kisha kuzungumuzia Biblia mara nyingi pamoja na Jairo, ilionekana wazi kuwa alielewa maana ya ubatizo wa Kikristo. Kwa hiyo, katika mwaka wa 2004, alijibia ulizo hili la maana sana: “Umejitoa kwa Mungu ili kufanya mapenzi yake?” Jairo alijibia ulizo hilo kwa kuangalia juu. Hiyo ilikuwa namna yake ya kusema ndiyo yenye ilipangwa mbele ya wakati. Kwa hiyo, wakati alikuwa na miaka 17, alibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova.

ANAKAZA MACHO JUU YA MAMBO YA MUNGU

Katika mwaka wa 2011, Jairo alipata njia mupya ya kuzungumuza: ordinatere yenye kuongozwa na macho. Chombo hicho kinafuata mwendo wa mboni ya jicho lake ili kufungua alama zenye kuwa kwenye skrini (écran). Kuchezesha-chezesha kope za macho ao kukazia macho alama moja ni kama vile kufinya kipanya (souris) cha ordinatere. Walimutengenezea Jairo ubao wenye kuwa na picha za alama ya maneno ao misemwa ili kumusaidia kuzungumuza. Wakati anachezesha-chezesha macho kwa kuangalia alama moja kati ya hizo, programu yenye kuwa ndani ya ordinatere hiyo inafanya habari yenye kuandikwa ikuwe sauti ya kielektroniki.

Jairo alipoendelea kuelewa mafundisho ya Biblia, nia yake ya kusaidia wengine kiroho iliongezeka. Wakati wa funzo letu la Biblia katika familia kila juma, kwa kawaida Jairo ananiangalia mimi na ordinatere yake tena na tena. Hiyo ni namna ya kunikumbusha nimuandikie maelezo yenye anaweza kutoa kwenye mikutano ya Kikristo wakati wa vipindi vya maulizo na majibu.

Wakati wa mikutano, anazungusha macho kwa uvumilivu kwenye skrini akitafuta ni alama gani inafaa kufinya, na kisha sauti yake ya kielektroniki inasikika na watu wote. Anaonyesha kabisa uso wa furaha kila wakati anapowatia moyo ndugu na dada wa kutaniko kupitia njia hiyo. Alex, mumoja kati ya marafiki vijana wa Jairo, anasema, “Sikuzote ninashangaa wakati ninasikia maelezo ya Jairo juu ya habari fulani ya Biblia.”

Jairo anatumia ordinatere yake yenye kuongozwa na macho, na sauti ya kielektroniki ya ordinatere hiyo ili kutoa maelezo kwenye mikutano na ili kuelezea wengine mambo anaamini

Jairo anatumia pia macho yake ili kuelezea wengine mambo yenye anaamini. Njia moja yenye kumusaidia kufanya hivyo ni kufinya picha ya alama inayoonyesha bustani ambako wanyama na watu wa rangi zote wanaishi kwa amani. Wakati anafungua alama hiyo, sauti ya ordinatere yake inatangaza, “Tumaini la Biblia ni kwamba dunia itakuwa paradiso. Katika paradiso hiyo hakutakuwa magonjwa na kifo, Ufunuo 21:4.” Ikiwa musikilizaji anapendezwa, Jairo anafinya tena, na ordinatere yake inasema, “Unapenda kujifunza Biblia na mimi?” Jambo la kushangaza ni hili: Tate (nkambo) yetu mwanaume alikubali kujifunza naye. Inapendeza kumuona Jairo wakati anamufundisha tate Biblia, akisaidiwa na Shahidi mwengine! Jambo la kufurahisha ni kwamba tate alibatizwa kwenye mukusanyiko wa eneo uliofanywa Mwezi wa 8, 2014 katika muji wa Madrid.

Walimu kwenye masomo wanaona namna Jairo anajitoa kwa Mungu. Rosario, mumoja kati ya wanganga wake wa kumusaidia kusema, anasema hivi: “Ikiwa siku moja nitapenda kuingia katika dini fulani, nitakuwa Shahidi wa Yehova. Nimeona namna imani ya Jairo imemusaidia kuwa na kusudi katika maisha, ijapokuwa hali yake ngumu.”

Kila mara, macho ya Jairo yanaonyesha furaha wakati ninamusomea ahadi hii ya Biblia: “Kilema atapanda juu kama vile paa anavyofanya, na ulimi wa bubu utapaaza sauti kwa furaha.” (Isaya 35:6) Hata ikiwa wakati fulani anavunjika moyo, mara nyingi yeye ni mwenye furaha. Hilo linawezekana kwa sababu anapitisha wakati mwingi katika mambo ya Mungu na pamoja na marafiki wake Wakristo. Jairo anaendelea kuwa mwenye furaha na iko na imani yenye nguvu, hilo linaonyesha kama kumutumikia Yehova kunafanya maisha magumu yakuwe na maana.

^ fu. 5 Kupooza kwa ubongo ni maneno ya ujumla yenye kutumiwa ili kueleza ugonjwa wa ubongo wenye kufanya viungo fulani vishindwe kufanya kazi. Ugonjwa huo unaweza pia kuleta kifafa, matatizo ya kula, na ya kusema. Aina ya kupooza kwa ubongo inayogusa mikono na miguu ndiyo aina ya kupooza ubongo iliyo kali sana; inaweza kufanya mikono na miguu yote ikauke na kufanya shingo iregee.