Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

MASIMULIZI KUHUSU MAISHA YA WATU

Kupata Nguvu Katika Uzaifu

Kupata Nguvu Katika Uzaifu

Hakuna mutu anayeniona anayeweza kufikiri kwamba nina nguvu. Ninakaa katika kiti cha magurudumu cha walemavu na ninapima kilo 29. Lakini, mwili wangu unapokuwa zaifu, nguvu za moyoni zinanisaidia kuendelea kuishi. Acheni niwafasirie namna nguvu na uzaifu vimebadilisha maisha yangu.

Nikiwa na miaka ine

Ninapofikiria wakati nilikuwa mutoto, ninakumbuka siku zenye furaha ndani ya nyumba ndogo katika muji wa mashambani kusini mwa inchi ya Ufaransa, ambako wazazi wangu walikuwa wanaishi. Baba yangu alinitengenezea kiti kinachoninginia kwenye kamba mbili, na nilipenda sana kukimbia katika bustani. Katika mwaka wa 1966, Mashahidi wa Yehova walitutembelea nyumbani na wakazungumuza kwa muda murefu na baba yangu. Miezi saba tu kisha hapo, baba yangu aliamua kuwa Shahidi wa Yehova. Mama yangu pia akakuwa Shahidi bila kukawia, na wakanikomalisha katika familia yenye furaha.

Magumu yangu yalianza muda mufupi kisha kurudia katika inchi ya Hispania, kwenye wazazi wangu walizaliwa. Nilianza kusikia maumivu makali ndani ya mikono na katika maunganisho ya miguu yangu. Miaka miwili kisha kuonana na waganga wengi, tulipata muganga mwenye kujulikana sana wa mifupa, aliyesema hivi kwa huzuni, “Hakuna tena tumaini la kupona.” Mama yangu akaanza kulia. Muganga huyo aliwaambia wazazi wangu kwamba nina ugonjwa wa mifupa usiopona wa watoto na kwamba mufumo wangu wa kulinda mwili unashambulia na kuharibu chembe za mwili, na hilo linaleta maumivu na kufanya maunganisho ya mwili yavimbe. Hata ikiwa sikuelewa mengi juu ya jambo hilo kwa sababu nilikuwa tu na miaka kumi, nilitambua kwamba hiyo ilikuwa habari mbaya.

Muganga aliomba wazazi wangu nitunzwe katika hospitali ya watoto walio na magonjwa ya muda murefu. Nilipofika huko, nyumba hiyo kubwa iliniogopesha sana. Maadibisho yalikuwa makali: Watawa wanawake walinikata nywele na wakanivalisha nguo zisizovutia zenye kufanana na za watoto wengine. Niliwaza hivi nikiwa mwenye kulia, ‘Namna gani nitaweza kuvumilia maisha hapa?’

NINATAMBUA MUSAADA WA YEHOVA

Kwa sababu wazazi wangu walikuwa wamenifundisha kumutumikia Yehova, nilikataa kushiriki ibada za Wakatoliki katika hospitali hiyo. Ilikuwa vigumu kwa watawa hao kuelewa sababu gani nilikataa. Nilimuomba Yehova asiniache, na bila kukawia nilijisikia kuwa nilikuwa ninazungukwa na mukono wake wa ulinzi, kama vile kumbatio changamufu na lenye nguvu la baba mwenye upendo.

Wazazi wangu waliruhusiwa kunitembelea kwa muda mufupi kila Siku ya Sita. Waliniletea vitabu vinavyotegemea Biblia vya kusoma ili imani yangu iendelee kuwa nguvu. Kwa kawaida watoto hawangepaswa kuwa na vitabu vyao wenyewe, lakini watawa hao waliniruhusu kuweka vitabu hivyo pamoja na Biblia yangu, ambayo nilikuwa ninasoma kila siku. Niliwaelezea watoto wengine wanawake juu ya tumaini langu la kuishi milele katika Paradiso duniani, ambamo hakuna mutu atakayegonjwa. (Ufunuo 21:3, 4) Hata ikiwa wakati fulani nilihuzunika na kujisikia kuwa peke yangu, nilifurahi kwamba imani yangu na tumaini langu kwa Yehova vilikuwa vinaendelea kuwa nguvu.

Kisha miezi sita ambayo niliona kuwa mirefu sana, waganga walinituma nyumbani. Ugonjwa wangu haukuwa umepungua, lakini nilifurahi kurudia nyumbani ili kukaa na wazazi wangu. Maunganisho ya mwili wangu yalibadili umbo sana, na nilisumbuliwa na maumivu zaidi. Nilianza miaka yangu ya ujana nikiwa zaifu sana. Lakini, nilipokuwa na miaka 14, nilibatizwa, nikiwa na uamuzi wa kumutumikia Baba yangu wa mbinguni kwa nguvu zangu zote. Hata hivyo, wakati fulani nilijisikia kuwa ninamukasirikia Yehova. Nilisali hivi: “Sababu gani mimi? Tafazali, uniponyeshe. Hauone namna ninavyoteseka?”

Ujana ulikuwa wakati mugumu kwangu. Nililazimika kukubali kwamba sitapona. Niliendelea kujilinganisha na marafiki wangu, waliokuwa na afya nzuri na waliofurahia maisha. Nilijisikia kuwa mutu wa hali ya chini, na sikupenda tena kuongea na mutu yeyote. Lakini, watu wa familia yangu na marafiki wangu walinitegemeza. Ninamukumbuka kwa furaha Alicia, anayenipita miaka 20, aliyekuwa rafiki yangu wa kweli. Alinisaidia kutokukazia akili ugonjwa wangu na kupendezwa na watu wengine kuliko kuhangaikia sana magumu yangu.

NINAPATA NJIA ZA KUFANYA MAISHA YANGU KUWA YENYE KUSUDI

Nilipokuwa na miaka 18, hali yangu ilirudi kuwa mbaya sana, na hata kuhuzuria mikutano ya Kikristo kulinifanya kuwa mwenye kuchoka sana. Hata hivyo, nikiwa nyumbani, nilitumia wakati mwingi niliopata ili kusoma Biblia kwa uangalifu. Kitabu cha Ayubu na cha Zaburi vilinisaidia kuelewa kwamba leo Yehova Mungu anatulinda zaidi sana kiroho lakini hatulinde kimwili. Kusali kwa ukawaida kulinisaidia kupata “nguvu zinazopita zile za kawaida” na “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote.”​—2 Wakorintho 4:7; Wafilipi 4:6, 7.

Nilipokuwa na miaka 22, nilielewa kwamba inaniomba tu nitembee kwa kutumia kiti cha magurudumu. Niliogopa kwamba watu watakuwa wanaona tu mwanamuke muzaifu ndani ya kiti bila kutambua kuwa ni mimi. Lakini, kiti hicho kilinisaidia nijisikie kuwa huru tena kwa njia fulani, na “laana” ikageuka kuwa baraka. Rafiki yangu anayeitwa Isabel alinishauria nifanye mupango wa kupitisha saa 60 pamoja naye katika mahubiri muda wa mwezi mumoja.

Kwanza, nilifikiri kwamba wazo hilo halikuwa nzuri. Lakini nilimuomba Yehova musaada, na pia kwa sababu familia yangu na marafiki wangu walinitegemeza, nilihubiri saa hizo. Mwezi huo wenye kazi nyingi ulipita haraka, na nilitambua kuwa nilishinda woga na haya niliyokuwa nayo. Nilifurahia sana mwezi huo na kwa hiyo katika mwaka wa 1996 niliamua kuwa painia wa kawaida, nikipitisha saa 90 kila mwezi katika mahubiri. Uamuzi huo ulikuwa moja kati ya maamuzi mazuri ambayo nimekwisha kuchukua, ulinifanya nimukaribie Mungu zaidi na hata ulinifanya niwe mwenye nguvu kimwili. Kuhubiri sana kuliniwezesha kuelezea watu wengi mambo ninayoamini na kusaidia wamoja kati yao wawe marafiki wa Mungu.

YEHOVA ANAENDELEA KUNITEGEMEZA

Katika kipindi cha joto cha mwaka wa 2001, nilifanya aksidenti mbaya ya motokari na nikavunjika miguu yote miwili. Nilipokuwa nikilazwa kwenye kitanda cha hospitali nikiwa na maumivu makali sana, nilisali kwa bidii kimyakimya kwa kusema hivi: “Tafazali, Yehova, usiniache!” Kisha tu hapo, mwanamuke aliyekuwa kwenye kitanda kilichokuwa karibu na mimi aliniuliza, “Wewe ni Shahidi wa Yehova?” Kwa sababu sikuwa na nguvu za kujibia, nilikubali tu kwa kutikisa kichwa. Mwanamuke huyo akasema hivi: “Ninawajua! Ninazoea kusoma magazeti yenu.” Maneno hayo yalinitia moyo sana. Hata katika hali yangu yenye kuhuzunisha, ningeweza kutoa ushahidi juu ya Yehova. Hilo lilikuwa pendeleo kabisa!

Wakati nilijisikia muzuri kidogo, niliamua kuhubiri tena zaidi. Nikiwa katika kiti changu cha magurudumu, mama yangu alinitembeza kuzunguka hospitali miguu yangu miwili ikiwa katika sima. Kila siku, tulitembelea wagonjwa wachache, tuliwauliza wanajisikia namna gani, na tuliwaachia vichapo fulani vinavyotegemea Biblia. Kufanya hivyo kulinichokesha sana, lakini Yehova alinipatia nguvu nilizohitaji.

Mimi na wazazi wangu katika mwaka wa 2003

Katika miaka michache iliyopita, maumivu yangu yaliongezeka na kufiwa na baba yangu kuliniongezea huzuni. Hata hivyo, ninajikaza kuendelea kuwa na mawazo mazuri. Namna gani? Wakati wowote inapowezekana, ninajikaza kuwa pamoja na marafiki na watu wa jamaa, na hilo linanisaidia kusahau magumu yangu. Na ninapokuwa peke yangu, ninasoma na kujifunza Biblia, ao kuhubiria watu wengine kupitia simu ao telefone.

Mara kwa mara ninafunga macho yangu na ninajiona katika dunia mupya ambayo Mungu anaahidi

Ninajaribu pia kufurahia mambo mepesi ya kufurahisha, kama vile upepo unaopeperushwa kwenye uso wangu na harufu nzuri ya maua. Mambo hayo yananisaidia kuwa mwenye shukrani. Kupenda mambo yenye kuchekesha kunanisaidia pia. Siku moja tulipokuwa katika mahubiri, rafiki yangu, aliyekuwa anasukuma kiti changu cha magurudumu alisimama ili kuandika jambo fulani. Kwa gafula, niliporomoka bila kuongozwa, na nikajigonga kwenye motokari iliyokuwa inasimama. Sisi wawili tulishituka, lakini wakati tuliona kwamba sikuumia, tulipasuka na cheko.

Kuna mambo mengi ambayo siwezi kufanya katika maisha. Ninaita mambo hayo mahitaji yangu yatakayotimia wakati unaokuja. Mara kwa mara ninafunga macho yangu na ninajiona katika dunia mupya ambayo Mungu anaahidi. (2 Petro 3:13) Ninajifikiria nikiwa na afya nzuri, nikiwa mwenye kutembea na kufurahia maisha kabisa. Ninachukua kwa uzito maneno haya ya Mufalme Daudi: ‘Mutumainie Yehova; uwe hodari na moyo wako uwe na nguvu.’ (Zaburi 27:14) Hata ikiwa mwili wangu umeendelea kuwa zaifu, Yehova amenifanya kuwa mwenye nguvu. Ninaendelea kupata nguvu katika uzaifu wangu.