Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

BIBLIA INABADILISHA MAISHA YA WATU

“Nilianza Kufikiri kwa Uzito Ikiwa Maisha Yangu Yalikuwa Yanaelekea Wapi”

“Nilianza Kufikiri kwa Uzito Ikiwa Maisha Yangu Yalikuwa Yanaelekea Wapi”
  • ALIZALIWA MWAKA WA 1941

  • ALIZALIWA KATIKA INCHI YA AUSTRALIA

  • ALIKUWA ANAVUTA SIGARETI, NA KUNYWA POMBE SANA

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nilikomalia katika Warialda, muji mudogo wa mashambani huko Nouvelle​-Galles du Sud. Katika eneo la Warialda watu wanafuga kondoo na ngombe, wanalima mbegu na mimea mingine midogo​-midogo. Muji huo ni safi, na hakuna matendo mengi ya uvunjaji wa sheria.

 

Kwa sababu mimi ndiye mukubwa kati ya watoto kumi, nilipokuwa na miaka 13, nilianza kufanya kazi ili kusaidia familia yetu kupata mahitaji ya kimwili. Kwa sababu sikusoma sana, nilifanya kazi katika mashamba. Nilipofikia miaka 15, nilianza kufanya kazi ya kuchunga mifugo, na kuzoeza farasi wa porini wazoeane na watu.

Kufanya kazi katika mashamba kuliniletea baraka mbalimbali. Kwa upande mwengine, nilifurahia sana kazi hiyo, na pia mazingira. Nilifurahia kuota moto usiku na kutazama mwezi na mbingu zenye kujaa nyota wakati upepo wenye baridi wa mangaribi ulipoeneza harufu nzuri katika musitu ulionizunguka. Ninakumbuka wakati nilikuwa ninafikiri kwamba ni lazima kuwe mutu fulani ambaye aliumba vitu hivyo vyote vizuri sana. Lakini, huko mashambani nilikuwa ninashawishiwa kufuata mazoea mabaya. Mara nyingi nilisikia watu wakitumia masemi yasiyofaa, na ilikuwa vyepesi kwangu kupata sigareti. Bila kukawia, nikazoea kutumia masemi yasiyofaa na kuvuta sigareti.

Nilipoeneza miaka 18, nilihamia huko Sydney. Nilijaribu kuingia katika jeshi lakini sikukubaliwa kwa sababu sikusoma sana. Nilipata kazi na nikabakia huko Sydney kwa muda wa mwaka mumoja. Wakati huo ndipo nilikutana kwa mara ya kwanza na Mashahidi wa Yehova. Nilikubali waliponialika kuhuzuria mukutano wao mumoja, na bila kukawia nikatambua kwamba mafundisho yao ni ya kweli.

Lakini, muda mufupi kisha hapo, niliamua kurudia mashambani. Mwishowe, nilienda Goondiwindi, huko Queensland. Huko nilipata kazi, nikaoa, na jambo lenye kuhuzunisha ni kwamba nikaanza kunywa pombe sana.

Mimi na bibi yangu tulizaa watoto wawili wanaume. Kisha watoto hao kuzaliwa, nilianza kufikiri kwa uzito ikiwa maisha yangu yalikuwa yanaelekea wapi. Nilikumbuka mambo ambayo nilisikia kwenye mukutano ule wa Mashahidi wa Yehova huko Sydney na nikaamua kufanya jambo fulani juu ya mambo niliyosikia kwenye mukutano huo.

Nilipata gazeti la zamani la Munara wa Mulinzi, ambalo lilikuwa na adresi ya ofisi ao biro ya tawi la Mashahidi wa Yehova wa Australia. Nilituma barua ili kuomba musaada. Walinijibu kwa kumutuma Shahidi mumoja anitembelee, Shahidi huyo alikuwa mwema na mwenye upendo. Bila kukawia, alianza kunifundisha Biblia.

BIBLIA ILIBADILISHA MAISHA YANGU: Nilipokuwa ninajifunza Biblia, nilitambua kwamba nilihitaji kufanya mabadiliko makubwa katika maisha yangu. Andiko moja la Biblia ambalo lilinigusa moyo sana ni 2 Wakorintho 7:1. Andiko hilo linatutia moyo “tujisafishe wenyewe kila unajisi [ao uchafu] wa mwili.”

 

Niliamua kwamba ningepaswa kuacha kuvuta sigareti na kunywa pombe sana. Haikuwa vyepesi kufanya mabadiliko hayo, kwa sababu nilikuwa nimezoea kunywa pombe sana na kuvuta sigareti kwa muda murefu. Lakini nilikusudia kuishi maisha ambayo yanamufurahisha Mungu. Jambo ambalo lilinisaidia sana ilikuwa kufuata kanuni iliyo katika andiko la Waroma 12:2: ‘Acheni kufanyizwa kulingana na mufumo huu wa mambo, bali mugeuzwe kwa kufanya upya akili yenu.’ Nilitambua kwamba ili kubadilisha tabia zangu, nilipaswa kubadilisha namna yangu ya kufikiri na kuona tabia zangu kama Mungu alivyoziona, ni kusema, kuziona kuwa tabia zenye kuharibu. Kwa musaada wa Mungu, niliweza kuacha kuvuta sigareti na kunywa pombe sana.

“Nilitambua kwamba ili kubadilisha tabia zangu, nilipaswa kubadilisha namna yangu ya kufikiri”

Hata hivyo, haikuwa vyepesi kwangu kuacha kutumia masemi yasiyofaa. Nilijua shauri la Biblia lililo katika andiko la Waefeso 4:29 ambalo linasema hivi: “Neno lililooza na lisitoke kinywani mwenu.” Hata hivyo, sikuacha mara moja kutumia masemi yasiyofaa. Niliona kwamba ilikuwa vizuri kutafakari ao kufikiri sana juu ya maneno ya andiko la Isaya 40:26. Kuhusu mbingu zenye nyota nyingi, andiko hilo linasema hivi: ‘Inueni macho yenu juu, muone. Ni nani ameviumba vitu hivi? Ni Yeye anayelileta jeshi lake kulingana na hesabu, ambaye zote anaziita kwa jina. Kutokana na wingi wa nguvu zenye musukumo, yeye pia akiwa hodari katika nguvu, hakuna hata moja kati ya hizo inayokosekana.’ Nilifikiri kwamba ikiwa Mungu ana nguvu za kuumba ulimwengu wetu mukubwa, ambao nilifurahia sana kutazama, bila shaka angenipa nguvu za kufanya mabadiliko ili kumufurahisha. Kwa kusali sana na kufanya bidii, polepole nilifikia kuacha kutumia masemi yasiyofaa.

FAIDA AMBAYO NIMEPATA: Nikiwa muchungaji wa mifugo, sikuwa na nafasi nyingi za kuzungumuza na watu, kwa sababu hapakuwa na watu wengi kwenye mashamba ambako nilikuwa ninatumikia. Lakini, kupitia mazoezi ambayo nilipata kwenye mikutano ya Mashahidi wa Yehova, nilijifunza namna ya kuzungumuza na watu. Zaidi ya hayo, mazoezi hayo yameniwezesha kuzungumuza na watu wengine juu ya habari njema ya Ufalme wa Mungu.​—Mathayo 6:9, 10; 24:14.

 

Kwa miaka mingi iliyopita, nimefurahia kutumika nikiwa muzee katika kutaniko. Ninaona kwamba ni pendeleo kufanya yote ninayoweza ili kusaidia Wakristo wenzangu. Hata hiyo, baraka kubwa ambayo nimepata ni kuungana na bibi yangu mwaminifu na mwenye upendo na pia watoto wangu wenye sura nzuri katika kumutumikia Yehova.

Ninamushukuru Yehova kwa kuniruhusu nifundishwe naye, hata ikiwa mimi ni mutu ambaye hakusoma sana. (Isaya 54:13) Ninakubali kabisa kwamba maneno ya andiko la Methali 10:22 ni ya kweli. Andiko hilo linasema hivi: “Baraka ya Yehova​—hiyo ndiyo hutajirisha.” Mimi na familia yangu tunangojea kujifunza mambo mengi juu ya Yehova na kumutumikia milele.