Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

VITU VYA MAANA SANA VYA HISTORIA YETU

“Nilienda na Nyumba Yangu Kila Mahali Kama Kobe”

“Nilienda na Nyumba Yangu Kila Mahali Kama Kobe”

WAKATI wa kampanye ya siku kenda ya kuhubiri iliyopita haraka sana ya Mwezi wa 8 na Mwezi wa 9, 1929, zaidi ya wahubiri 10 000 walitembea katika Amerika yote. Waliwatolea watu vitabu na vijitabu 25 000. Kati ya wahubiri hao wa Ufalme, kulikuwa wakolportere 1 000. Hesabu yao iliongezeka kabisa! Kikaratasi kilichoitwa Bulletin * kilisema hivi: “Lilikuwa jambo la kushangaza” kuona kwamba hesabu ya mapainia iliongezeka mara tatu tangu 1927 mupaka 1929.

Mwishoni mwa 1929, kulitokea matatizo makubwa ya feza. Siku ya Pili, tarehe 29 Mwezi wa 10, 1929, kuanguka kwa bei katika soko kubwa la New York ambako watu wanabadilisha mali na feza, kulitokeza matatizo makubwa ya feza ulimwenguni. Benki nyingi zilifunga milango. Wakulima waliacha shuguli zao. Izine kubwa-kubwa zilifunga milango yao. Watu wengi walipoteza kazi. Katika 1933, kila siku watu 1 000 huko Amerika walifukuzwa katika nyumba zao kwa sababu ya kushindwa kulipa madeni yao.

Namna gani wahubiri wa wakati wote wangeweza kuhubiri katika kipindi hicho kigumu? Jambo moja ambalo lingewasaidia ni kuwa na nyumba zenye kukokotwa na motokari. Kwa kuwa haikuomba kulipa feza za kupanga ao takse kwa ajili ya nyumba hizo, hilo liliwapunguzia mapainia wengi garama na kuwasaidia waendelee na utumishi wao. * Pia, wakati wa mukusanyiko, mutu angelala katika nyumba zenye kukokotwa bila malipo yoyote. Katika 1934, Bulletin ilitoa maelezo yaliyo wazi kuhusu namna ya kujenga nyumba ndogo lakini nzuri na iliyo na maji, chombo cha kupikia chakula, kitanda cha kukunja, na chombo cha kuleta joto.

Katika sehemu zingine za ulimwengu, wahubiri wenye kujiweza walianza kujijengea nyumba zenye kukokotwa. Victor Blackwell alisema hivi: “Noa alikuwa hajajenga safina katika maisha yake, na mimi nilikuwa sijajenga nyumba yenye kukokotwa hata siku moja.” Lakini, ndugu Victor Blackwell aliweza kufanya hivyo.

Nyumba yenye kukokotwa iliyo karibu kuvukishwa upande mwingine wa muto wakati wa majira ya mvua nyingi huko India

Avery na bibi yake Lovenia Bristow walikuwa na nyumba yenye kukokotwa. Avery alisema hivi: “Nilienda na nyumba yangu kila mahali kama kobe.” Bristow na bibi yake walifanya upainia pamoja na Conrow na bibi yake Anne, waliokuwa na nyumba iliyofunikwa kwa karatasi nzito yenye lami. Vipande vya karatasi vilikuwa vikianguka kila mara waliposafiri na nyumba yao. Avery alisema hivi: “Nyumba kama hiyo ilikuwa haijaonekana hapo mbele na tangu wakati huo mupaka leo hakujakuwa nyumba kama hiyo!” Lakini Avery alisema kwamba Conrow, bibi yake na watoto wao wawili “walifanyiza familia yenye furaha sana.” Ndugu Harvey Conrow aliandika hivi: “Hatukukosa kitu chochote, na tulijisikia salama kabisa katika kazi ya Yehova na chini ya ulinzi wake wenye upendo.” Baadaye Conrow, bibi yake na watoto wao wawili, walisoma Masomo ya Gileadi na walitumwa kuwa wamisionere katika inchi ya Peru.

Familia ya ndugu Battaino pia ilifanya kazi ya upainia. Walipojua kwamba wangezaa mutoto, Giusto na Vincenza Battaino waligeuza motokari yao Ford Modèle A ya 1929 kuwa nyumba “iliyokuwa kama hoteli nzuri kabisa” ilipolinganishwa na mahema ambamo waliishi hapo mbele. Waliendelea pamoja na binti wao mudogo kutumika katika mugawo wao wa maana wa kuwahubiria Waitaliano wanaoishi huko Amerika.

Watu wengi walisikiliza habari njema, lakini kwa kuwa walikuwa masikini na hawakuwa na kazi, ilikuwa vigumu kwao kutoa michango kwa ajili ya vichapo. Walitoa vitu mbalimbali kama michango kwa ajili ya vichapo. Dada mapainia wawili walipata aina 64 ya vitu ambavyo watu hao wenye kupendezwa walitoa. Vitu hivyo vilikuwa kamba vitu vinavyopatikana katika duka la kijijini.

Fred Anderson alikutana na mukulima fulani aliyetaka kupata vitabu vyetu, mukulima huyo alitoa miwani ao linete iliyokuwa ya mama yake ili apate vitabu. Kwenye shamba lingine, mwanaume mumoja alipendezwa na vichapo vyetu, lakini alisema hivi: “Sina miwani ya kunisaidia kusoma.” Lakini alipovaa miwani ya jirani yake, aliweza kusoma vizuri vitabu vyetu na alifurahia kutoa muchango ili Anderson amutolee vitabu na miwani aliyopewa na yule mukulima mwengine.

Herbert Abbott alikuwa anatembea na nyumba ya kuku katika motokari yake. Kisha kupata kuku tatu ao ine kwa kubadilishana na vichapo, alienda kuziuzisha kwenye soko na kuuza esanse. Aliandika hivi: “Wakati fulani tulikosewa na feza kabisa. Lakini hilo halikutuzuia kuhubiri. Wakati tulikuwa na esanse katika motokari, tuliendelea na kazi yetu tukitumaini kama Yehova angetutegemeza wakati tungekosa esanse.”

Kumutegemea Yehova na kuazimia sana kufanya kazi yake kuliwasaidia watumishi wa Mungu katika kipindi hicho kigumu. Katika zoruba ya mvua Maxwell na Emmy Lewis walitoka katika nyumba yao yenye kukokotwa mbele ivunjwe mara mbili na muti ulioanguka juu yake. Maxwell aliandika hivi: “Mambo hayo hayakutuzuia, yalikuwa tu matukio ya kawaida na wazo la kuacha kazi ya kuhubiri halikuingia katika akili yetu hata kidogo. Kulikuwa kazi kubwa ya kufanya, na tulitamani kuifanya.” Bila kuogopa na pamoja na musaada wa marafiki wenye upendo, Maxwell na Emmy walijenga tena nyumba yao yenye kukokotwa.

Katika wakati wetu wenye matatizo, mamilioni ya Mashahidi wa Yehova wenye bidii wanaendelea kuonyesha roho ya kujitolea kama hiyo. Zaidi ya hilo, kama mapainia hao wa kwanza-kwanza, tumeazimia kuendelea kufanya kazi ya kuhubiri mupaka Yehova aseme kwamba inatosha.

^ Leo kikaratasi hicho kinaitwa Huduma Yetu ya Ufalme.

^ Wakati huo, mapainia wengi hawakuwa wanafanya kazi ya kimwili. Walipewa vichapo vya Biblia kwa bei ya chini na kisha kuvitolea watu, walitumia michango waliyopata ili kutosheleza mahitaji yao ya lazima.