Je, Umewahi Kuhisi Kama Umetengwa na Wengine?

Je, Umewahi Kuhisi Kama Umetengwa na Wengine?

Wafundishe Watoto Wako

Je, Umewahi Kuhisi Kama Umetengwa na Wengine?

MTU aliyetengwa na wengine ni yule asiyekubaliwa kujiunga na kikundi chao. Huenda rangi ya ngozi yake ikawa tofauti na yao au akawa ametoka nchi nyingine, ama akawa anaongea au kufanya mambo kwa njia tofauti nao. Je, kuna wakati unapohisi kama umetengwa? *

Hebu tuzungumze kuhusu mtu mmoja aliyehisi kuwa ametengwa na wengine. Jina lake ni Mefiboshethi. Acheni tuchunguze yeye alikuwa nani na kwa nini alihisi hivyo. Ikiwa wewe unahisi kuwa umetengwa na wengine, unaweza kujifunza mambo mengi kutokana na Mefiboshethi.

Mefiboshethi alikuwa mwana wa Yonathani, rafiki mkubwa wa Daudi. Kabla ya Yonathani kufa vitani, alimwambia Daudi hivi: ‘Watendee wema watoto wangu.’ Miaka kadhaa baada ya Daudi kuwa mfalme, alikumbuka maneno ya Yonathani. Lakini Mefiboshethi ndiye mtoto pekee wa Yonathani aliyekuwa hai. Alipokuwa mdogo, Mefiboshethi alipatwa na aksidenti mbaya na hakuweza kutembea vizuri maishani mwake. Je, unaweza kuona ni kwa nini alihisi kuwa ametengwa?

Daudi alitaka kumtendea wema mwana wa Yonathani. Kwa hiyo, Daudi alifanya mipango ili Mefiboshethi apate makao karibu na nyumba yake katika jiji la Yerusalemu, na pia akampa mahali pa kuketi kwenye meza ya kulia chakula ya Daudi. Ziba pamoja na watoto wake na wafanyakazi, walipewa kazi ya kumtumikia Mefiboshethi. Kwa kweli, Daudi alimheshimu sana mwana wa Yonathani! Je, unajua kilichotokea?

Daudi alipatwa na matatizo katika nyumba yake. Absalomu, mmoja wa wana wa Daudi, alimpinga baba yake na akajaribu kumnyang’anya utawala. Daudi alilazimika kukimbia ili aokoe maisha yake. Mefiboshethi alitaka kukimbia pamoja na Daudi wakati watu wengine wengi walipokimbia. Marafiki hao wa Daudi walijua kwamba yeye ndiye mwenye haki ya kuwa mtawala. Lakini Mefiboshethi hangeweza kwenda pamoja nao kwa kuwa hangeweza kutembea vizuri.

Kisha Ziba akamwambia Daudi kwamba Mefiboshethi alibaki kwa sababu alitaka sana kuwa mfalme. Daudi aliamini uwongo huo! Kwa hiyo, akampa Ziba mali yote ya Mefiboshethi. Muda mfupi baadaye, Daudi alimshinda Absalomu vitani na akarudi Yerusalemu. Sasa Daudi alimpa Mefiboshethi nafasi ya kujieleza. Hata hivyo, Daudi aliamua kwamba Mefiboshethi na Ziba wanapaswa kugawanya mali ya Mefiboshethi. Unafikiri Mefiboshethi alifanya nini?

Hakulalamika kuwa Daudi alifanya uamuzi usiofaa. Mefiboshethi alitambua kwamba mfalme alihitaji kuwa na amani ya akili ili afanye kazi yake vyema. Hivyo, akasema Ziba apewe mali yote. Jambo lililokuwa muhimu kwa Mefiboshethi ni kwamba mtumishi wa Yehova, Daudi, alikuwa amerudi Yerusalemu akiwa mfalme.

Mefiboshethi aliteseka sana. Mara nyingi alihisi kama mtu aliyetengwa na wengine. Lakini Yehova alimpenda na kumtunza. Tunaweza kujifunza nini kutokana na kisa hicho?— Hata tunapofanya lililo sawa, wengine wanaweza kusema uwongo kutuhusu. Yesu alisema: “Ikiwa ulimwengu unawachukia ninyi, mnajua kwamba umenichukia mimi kabla ya kuwachukia ninyi.” Watu hata walimuua Yesu! Tunaweza kuwa na uhakika kwamba tukitenda mema, Mungu wa kweli Yehova na Mwana wake Yesu, watatupenda.

Soma katika Biblia yako

1 Samweli 20:15-17, 41, 42

2 Samweli 4:4; 9:1-10; 19:24-30

Yohana 15:18

[Maelezo ya Chini]

^ Kama unasoma sehemu hii pamoja na mtoto, unapoona kistari kama hiki (—), tua na umtie moyo mtoto atoe maoni yake.