Angalisho! Biblia Si Hirizi
Angalisho! Biblia Si Hirizi
“NENO la Mungu liko hai nalo lina nguvu.” (Ebr. 4:12) Kupitia maneno hayo mutume Paulo alionyesha kama neno la Mungu lina nguvu ya kugusa moyo na kubadili maisha ya mutu.
Lakini, uasi-imani ulipotokea kisha kifo cha mitume, kama ilivyotabiriwa, watu walianza kuwa na maoni mabaya kuhusu nguvu ya Biblia. (2 Pet. 2:1-3) Baadaye, viongozi wa makanisa walianza kuonyesha kwamba Neno la Mungu lina nguvu fulani ya kiuchawi. Profesere Harry Gamble aliandika kuhusu “kutumia maandiko ya Kikristo kama hirizi.” Alionyesha kwamba katika miaka ya 201-299 kisha Yesu, Baba wa kanisa aliyeitwa Origène alisema kwamba “kusikiliza maandiko matakatifu kunaleta faida. Ikiwa maneno yana nguvu katika mambo ya uchawi ya wapagani, basi maneno ya kweli ya Mungu yaliyo katika maandiko yana nguvu nyingi zaidi.” Jean Chrysostome aliyeishi mwishoni mwa miaka 301-399 aliandika kwamba “Shetani hatasubutu kukaribia nyumba ambamo munapatikana Injili.” Alionyesha pia kwamba watu fulani wanafunga sehemu za Injili kwenye shingo zao kama hirizi (kitu cha kuwalinda na jambo mbaya.) Profesere Gamble alionyesha pia kwamba mwanateolojia Mukatoliki Augustin “alisema kwamba ikiwa kichwa cha mutu kinauma alipaswa kuweka Injili ya Yohana chini ya kichwa chake anapolala.” Kwa hiyo, maandishi ya Biblia yalitumiwa kama hirizi. Je, wewe unafikiri Biblia ni kama hirizi, kitu kinacholeta bahati nzuri, ao chombo kinachoweza kumulinda mutu asipatwe na jambo mbaya?
Labda bibliomansia ndilo zoea linaloenea sana la kutumia Biblia kama hirizi. Zoea hilo linafanywa namna gani? Mutu anafungua Biblia kwa gafula na kusoma andiko la kwanza analoona akifikiri kwamba maneno ya andiko hilo yatamupa musaada ao uongozi anaohitaji. Kwa mufano, Profesere Gamble alisema kwamba, siku moja Augustin alisikia sauti ya mutoto katika nyumba jirani ikisema: “Kamata usome, kamata usome,” basi Augustin alifikiri kwamba Mungu ndiye anayemuambia afungue Biblia na asome andiko la kwanza tu atakaloona.
Je, umekwisha kusikia kuhusu watu waliomuomba Mungu wakati wanapopambana na tatizo fulani, kisha wanafungua Biblia mara moja ao kwa gafula, wakiamini kwamba andiko la kwanza watakaloona litawasaidia kushinda tatizo lao? Ijapokuwa mutu anaweza kufanya hivyo kwa nia nzuri, hiyo si njia ambayo Wakristo wanashauriwa kutumia ili kutafuta uongozi katika Maandiko.
Yesu aliwahakikishia wanafunzi wake kwamba atawatumia ‘musaidizi, roho takatifu.’ Na kwamba ‘itawafundisha mambo yote na kuwakumbusha mambo yote aliyowaambia.’ (Yoh. 14:26) Roho ya Mungu inakumbusha mutu mambo ambayo amejifunza, lakini zoea la bibliomansia haliombe mutu awe na ujuzi wa Maandiko.
Zoea hilo na mazoea mengine ya kutumia Biblia kama hirizi yameenea sana. Lakini, Neno la Mungu linakataza kutafuta ishara za bahati. (Law. 19:26; Kumb. 18:9-12; Mdo. 19:19) “Neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu,” lakini tunapaswa kulitumia kwa ufundi. Kutumia ujuzi wa kweli, wala si kutumia Biblia kama hirizi, ndiyo njia inayoweza kufanya maisha ya watu yawe mazuri. Kuwa na ujuzi huo kumewasaidia wengi kufuata kanuni zenye hekima, kuachana na maisha yanayoleta matatizo, kufanya maisha ya familia yawe mazuri, kuwa na urafiki muzuri na wa pekee pamoja na Mutungaji wa Biblia.