Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Kipepeo Mwenye Rangi Nyingi—Siri Inafunuliwa

Kipepeo Mwenye Rangi Nyingi—Siri Inafunuliwa

WATU wa Ulaya wanaotazama vipepeo wenye rangi nyingi wamevutiwa kwa muda murefu na vipepeo hao na wamejiuliza ni nini kinawapata vipepeo hao wakati kila kipindi cha kipwa kinaisha. Je, wanakufa wakati kipindi cha baridi kinaanza? Uchunguzi wa hivi karibuni umeonyesha habari ya ajabu sana. Vipepeo hao wanasafiri kila mwaka kutoka Ulaya kaskazini na kuenda Afrika.

Wachunguzi walichanga habari walizopata kupitia rada ao vyombo vya uchunguzi vya hali ya juu pamoja na maelfu ya habari walizopewa na watu wa Ulaya wanaotazama vipepeo hao. Habari walizopata zilionyesha kwamba wakati kipwa kinaisha, mamilioni ya vipepeo hao wenye rangi nyingi wanahamia upande wa kusini, mara nyingi wakiruka kwa umbali wa kilometa zaidi ya 500 angani, na hivyo watu hawawaone tena kwa vyepesi. Vipepeo hao wenye rangi nyingi wanangojea upepo mwingi, unaowasafirisha kwa mwendo wa kilometa 45 kwa saa moja katika safari yao ndefu kuelekea Afrika. Safari yao ya kila mwaka ya kuhama inayofikia kilometa 15 000, inaanzia kaskazini upande wa Arktiki na inamalizikia mbali upande wa kusini kwenye tropiki za Afrika Magaribi. Safari ambayo kipepeo mwenye rangi nyingi anafanya ni mara mbili ya ile inayofanywa na kipepeo wa Amerika ya Kaskazini anayeitwa “kipepeo mufalme” [Danaus plexippus]. Vipepeo hao wenye rangi nyingi wanazaana na kufa wakiwa katika safari, kizazi cha sita ndicho kinarudia mahali walipotoka.

Jane Hill, Mwalimu wa Masomo ya Juu katika muji wa York, Uingereza, anaeleza hivi: “Kipepeo Mwenye Rangi Nyingi anaendelea na safari yake, akizaa, na kusonga mbele.” Kila mwaka, vipepeo hao wote wanasafiri, wakizaana njiani, na kusonga mbele na safari yao kutoka Ulaya kaskazini mupaka Afrika na wanafanya vilevile wakati wa kurudia mahali walipotoka.

Richard Fox, musimamizi wa shirika la kulinda vipepeo, anasema hivi: “Kiumbe hiki kidogo sana ambacho uzito wake haufikie gramu moja, kina ubongo ulio kama chongo ya sindano na hakiwezi kujifunza jambo lolote kutokana na wakubwa wake, ni kusema, vipepeo wakubwa zaidi, kinafanya safari ndefu ya kuhama kutoka kontinenti moja mupaka kontinenti nyingine.” Fox anasema tena kwamba kidudu hicho “kiliwaziwa wakati fulani kuwa kinapeperushwa tu na upepo huku na huku mupaka wakati kilikufa katika kipindi cha baridi ya Uingereza bila tumaini lolote kwamba hali itakuwa nzuri kwa wazao wake.” Lakini uchunguzi huo “umeonyesha kuwa Vipepeo Wenye Rangi Nyingi ni wasafiri wa hali ya juu.”