Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Je, Kuna Kiumbe Fulani Anayesababisha Uovu?

Je, Kuna Kiumbe Fulani Anayesababisha Uovu?

Je, Kuna Kiumbe Fulani Anayesababisha Uovu?

“NILIKUTANA uso kwa uso na Ibilisi.” Hivyo ndivyo kamanda wa majeshi ya Umoja wa Mataifa nchini Rwanda alivyosema akionyesha kushindwa kwa majeshi hayo kuchukua hatua yoyote ya kukomesha mauaji ya jamii nzima-nzima nchini humo mwaka wa 1994. Akizungumza kuhusu ukatili usio wa kawaida ambao ulifanywa wakati huo, mtu mwingine alisema: “Ikiwa kuna mtu anayetilia shaka kama kuna Shetani, basi tukutane kwenye kaburi la ujumla nchini Rwanda.” Je, ukatili kama huo ni kazi ya Ibilisi?

Watu wengi hawafikiri kwamba jeuri na ukatili wa aina hiyo ni kazi ya kiumbe mwovu wa roho asiyeonekana. Wengi wanafikiri kwamba mambo kama hayo yanasababishwa na uovu tuliozaliwa nao na kwamba chanzo kikuu cha uovu ni mtazamo wetu wa ubinafsi. Watu wengine wanafikiri kwamba kundi fulani la watu matajiri na wenye nguvu, ambao wanafanyiza mtandao wa siri wa ulimwenguni pote, wamekuwa wakidanganya watu kwa miaka mingi ili waitawale dunia. Kisha, kuna wale wanaozilaumu serikali na watawala wa nchi zao kwa ukosefu wa haki na mateso wanayoona.

Wewe una maoni gani? Kwa nini uovu, ukatili, jeuri, na kuteseka kumeenea sana ulimwenguni leo ingawa kuna jitihada za kukomesha mambo hayo? Kwa nini wanadamu wanakimbilia kufanya mambo maovu, huku wakipuuza maonyo yanayotolewa? Je, kuna kiumbe anayesababisha mambo yote hayo? Ni nani hasa anayeutawala ulimwengu? Huenda majibu ya maswali hayo yakakushangaza.