Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 119

Yesu​—Ni Njia, Kweli, na Uzima

Yesu​—Ni Njia, Kweli, na Uzima

YOHANA 14:1-31

  • YESU ANAENDA KUTAYARISHA NAFASI

  • ANAAHIDI WANAFUNZI WAKE KWAMBA WATAPATA MUSAIDIZI

  • BABA NI MUKUBWA KULIKO YESU

Yesu angali katika chumba cha juu pamoja na wanafunzi wake kisha chakula cha ukumbusho, anawaambia hivi: “Mioyo yenu isivurugike. Mukuwe na imani katika Mungu; mukuwe na imani katika mimi pia.”—Yohana 13:36; 14:1.

Yesu anaelezea mitume wake waaminifu kuwa hawapaswe kutaabika ao kuhangaika kwa sababu anaenda. Anasema hivi: “Katika nyumba ya Baba yangu kuko makao mengi. . . . Kama ninaenda na kuwatayarishia ninyi nafasi, nitakuja tena na nitawapokea ninyi katika nyumba yangu mwenyewe, ili kwenye niko, ninyi pia mukuwe pale.” Lakini, mitume hawaelewe kuwa anazungumuzia juu ya kuenda mbinguni. Tomasi anauliza hivi: “Bwana, sisi hatujue kwenye unaenda. Namna gani tunaweza kujua njia?”—Yohana 14:2-5.

Yesu anajibia hivi: “Mimi ndiye njia na kweli na uzima.” Wale wenye kumukubali na kusikiliza mafundisho yake na kufuata mufano wake, ndio tu wanaweza kuingia katika nyumba ya Baba yake, ni kusema, mbinguni. Yesu anasema hivi: “Hakuna mwenye anakuja kwa Baba isipokuwa kupitia mimi.”—Yohana 14:6.

Filipo mwenye anasikiliza kwa uangalifu, anamuomba hivi: “Bwana, utuonyeshe Baba, na hilo linatutosha.” Pengine Filipo anapenda Mungu afanye mambo fulani ili kujionyesha kama vile alifanya katika maono yenye Musa, Eliya, na Isaya waliona. Lakini, mitume wako na jambo la muzuri zaidi kuliko maono hayo. Yesu anaonyesha jambo hilo, anajibia hivi: “Je, hata kisha mimi kuwa pamoja na ninyi kwa wakati murefu vile, Filipo, bado haujanijua? Kila mutu mwenye ameniona mimi amemuona Baba pia.” Yesu anaonyesha kwa ukamilifu utu ao sifa za Baba yake; kwa hiyo, kuishi na Yesu na kumutazama kwa uangalifu ni kama vile kumuona Baba. Kwa kweli, Baba ni mukubwa kuliko Mwana, kwa sababu Yesu anasema hivi: “Mambo yenye ninawaambia ninyi, siyaseme kwa kujitungia mwenyewe.” (Yohana 14:8-10) Kwa hiyo, mitume wanaona kuwa Yesu anamupatia Baba yake utukufu kwa ajili ya mafundisho yake.

Mitume wa Yesu wameona namna anafanya miujiza na wamesikia namna anatangaza habari njema juu ya Ufalme wa Mungu. Sasa anawaambia hivi: “Kwa kweli kabisa ninawaambia ninyi, kila mutu mwenye ananiamini atafanya pia kazi zenye mimi ninafanya; na atafanya kazi kubwa kuliko hizi.” (Yohana 14:12) Yesu hapendi kusema kuwa watafanya miujiza mikubwa kuliko yenye alifanya. Lakini, watafanya kazi ya kuhubiri kwa muda murefu zaidi, katika eneo kubwa zaidi, na watahubiria watu wengi zaidi.

Hawatabakia peke yao wakati Yesu ataenda, kwa sababu anawapatia ahadi hii: “Mukiomba jambo lolote katika jina langu, nitalifanya.” Pia, anasema hivi: “Nitamuomba Baba, na atawapatia ninyi musaidizi mwingine akuwe pamoja na ninyi milele, roho ya ile kweli.” (Yohana 14:14, 16, 17) Anawahakikishia kuwa watapata roho takatifu, ambayo ni musaidizi mwingine. Jambo hilo linatokea siku ya Pentekoste.

Yesu anasema hivi: “Kisha tu wakati kidogo ulimwengu hautaniona tena, lakini ninyi mutaniona, kwa sababu ninaishi na ninyi mutaishi.” (Yohana 14:19) Kisha kufufuliwa kwake, Yesu atawatokea akiwa na mwili wa kibinadamu, lakini pia kisha wakati fulani, atawafufua na kuwa pamoja nao mbinguni wakiwa viumbe wa roho.

Sasa Yesu anasema kweli hii yenye kuwa mwepesi: “Kila mutu mwenye kuwa na amri zangu na kuzishika, huyo ndiye mwenye ananipenda. Na kila mutu mwenye ananipenda atapendwa na Baba yangu, na mimi nitamupenda na nitajionyesha waziwazi kwake.” Juu ya jambo hilo mutume Yuda, mwenye anaitwa pia Tadayo, anauliza hivi: “Bwana, kumetokea nini ili ukusudie kujionyesha waziwazi kwetu lakini hapana kwa ulimwengu?” Yesu anajibu hivi: “Kama mutu yeyote ananipenda, atashika neno langu, na Baba yangu atamupenda . . . Kila mutu mwenye hanipendi hashike maneno yangu.” (Yohana 14:21-24) Tofauti na mitume wake, ulimwengu haumuone Yesu kuwa njia, kweli, na uzima.

Yesu iko karibu kuenda, sasa namna gani wanafunzi wake wataweza kukumbuka mambo yote yenye aliwafundisha? Yesu anaeleza hivi: “Lakini musaidizi, roho takatifu yenye Baba atatuma katika jina langu, huyo atawafundisha mambo yote na kuwakumbusha mambo yote yenye niliwaambia.” Mitume wameona nguvu ya roho takatifu wakati inatenda, kwa hiyo, maneno hayo yanawatia moyo sana. Yesu anaongeza hivi: “Ninawaachia ninyi amani; ninawapatia amani yangu. . . . Mioyo yenu isivurugike wala kuregea kwa woga.” (Yohana 14:26, 27) Kwa sababu Yehova atawaongoza na kuwalinda, wanafunzi wa Yesu hawana sababu ya kuhangaika.

Hivi karibuni wataona ushuhuda wenye kuonyesha kuwa Mungu atawalinda. Yesu anasema hivi: “Mutawala wa ulimwengu anakuja, na hana uwezo juu yangu.” (Yohana 14:30) Shetani aliweza kuingia katika Yuda na kumuchochea. Lakini Yesu hana uzaifu wowote wa zambi wenye Shetani anaweza kutumia ili kumuchochea aache kumutii Mungu. Na Shetani hataweza kumufanya abakie katika kifo. Sababu gani? Yesu anasema hivi: “Ninafanya kama vile Baba aliniamuru.” Iko hakika kuwa Baba yake atamufufua.—Yohana 14:31.