Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 111

Mitume Wanaomba Alama

Mitume Wanaomba Alama

MATAYO 24:3-51 MARKO 13:3-37 LUKA 21:7-38

  • WANAFUNZI INE WANAOMBA ALAMA

  • KUTIMIZWA KWA ALAMA KATIKA SIKU ZA MITUME NA KUENDELEA

  • TUNAPASWA KUENDELEA KUWA MACHO

Ni Siku ya Pili kisha muchana, na siku ya Nisani 11 inaanza kumalizika. Tena utumishi mukubwa wa Yesu duniani unakaribia kufika mwisho. Muchana amekuwa akifundisha katika hekalu, na usiku amekuwa akienda kulala inje ya muji. Watu wamependezwa sana na mafundisho yake. Walikuwa “wanakuja asubui sana katika hekalu ili wamusikilize.” (Luka 21:37, 38) Yesu amekaa sasa kwenye Mulima wa Mizeituni pamoja na mitume wake ine: Petro, Andrea, Yakobo, na Yohana.

Mitume hao ine wamekuja kwake kwa siri. Wanaogopa kwa ajili ya hekalu kwa sababu Yesu ametoka tu kutabiri kwamba hakuna jiwe lenye litaachwa juu ya jiwe. Kuko mambo mengi yenye yangali yanawahangaisha. Hapo mbele Yesu aliwaambia hivi: “Muendelee kuwa tayari, kwa sababu Mwana wa binadamu atakuja katika saa yenye hamutazamie.” (Luka 12:40) Alizungumuzia pia “siku yenye Mwana wa binadamu atafunuliwa.” (Luka 17:30) Je, maelezo hayo yanapatana kwa njia fulani na mambo yenye alitoka tu kuzungumuzia kuhusu hekalu? Mitume wanapenda kujua zaidi. Wanamuuliza: “Tuambie mambo haya yatakuwa wakati gani, na ni nini itakuwa alama ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mupangilio wa mambo?”—Matayo 24:3.

Pengine wanawaza kwamba hawataona tena hekalu sababu litaharibiwa. Tena, wanauliza kuhusu kuwapo kwa Mwana wa binadamu. Pengine wanakumbuka kwamba Yesu alitoa mufano kuhusu “mutu fulani wa familia ya kifalme” mwenye “alisafiri kuenda inchi ya mbali ili afanywe kuwa mufalme na kisha arudie.” (Luka 19:11, 12) Na mwishowe, wanajiuliza ni nini itatokea wakati wa “umalizio wa mupangilio wa mambo.”

Katika jibu lake lenye mambo mengi, Yesu anatoa alama yenye kuonyesha ni wakati gani mupangilio wa mambo wa Wayahudi na hekalu lake vitafikia mwisho. Lakini anatoa maelezo mengi zaidi. Wakati wenye kuja, alama hii itasaidia Wakristo watambue kwamba wanaishi katika kipindi cha “kuwapo” kwake na kwamba wanakaribia mwisho wa mupangilio wote wa mambo wa dunia.

Kadiri miaka inaendelea, mitume wanaona utimizo wa unabii wa Yesu. Wanaanza kujionea mambo mengi yenye alitabiri. Kwa hiyo, Wakristo wenye kuwa macho wenye wanaishi miaka 37 kisha, katika mwaka wa 70 kisha kuzaliwa kwa Yesu, wako tayari kwa ajili ya uharibifu wenye kukaribia wa mupangilio wa Wayahudi na hekalu lao. Lakini, haiko mambo yote yenye Yesu anatabiri ndiyo yanatimia katika kipindi chenye kuongoza kwenye mwaka wa 70 kisha kuzaliwa kwa Yesu. Kwa hiyo, ni alama gani itaonyesha kama Yesu amekuwa Mufalme? Yesu anafunulia mitume wake jibu.

Yesu anatabiri kama kutakuwa “vita na habari za vita” na kama “taifa litasimama kupigana na taifa na ufalme kupigana na ufalme.” (Matayo 24:6, 7) Anasema tena kama “kutakuwa matetemeko makubwa ya inchi na mahali pamoja kisha pengine kutakuwa upungufu wa chakula na magonjwa hatari.” (Luka 21:11) Yesu anaonya wanafunzi wake hivi: “Watu watawakamata ninyi na kuwatesa.” (Luka 21:12) Manabii wa uongo watatokea na kupoteza watu wengi. Uvunjaji wa sheria utaongezeka, na upendo wa watu wengi utapoa. Tena, anasema kama “habari njema ya Ufalme itahubiriwa katika dunia yote yenye kukaliwa na watu ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote, na kisha ule mwisho utakuja.”—Matayo 24:14.

Hata kama unabii wa Yesu unatimizwa kwa kiasi fulani kupitia matukio fulani yenye yanatokea mbele na wakati Waroma wanaharibu Yerusalemu, ingewezekana unabii huo ufikie kutimia kwa njia kubwa zaidi? Unaona ushuhuda wenye kuonyesha kwamba unabii huo wa maana unaendelea kutimia kwa njia kubwa katika wakati wetu?

Jambo moja lenye Yesu alitia katika alama ya kuwapo kwake ni kutokea kwa “lile chukizo lenye linaleta uharibifu.” (Matayo 24:15) Katika mwaka wa 66 kisha kuzaliwa kwa Yesu, chukizo hilo lilikuwa “majeshi yenye kupiga kambi” ya Waroma, pamoja na bendera zao za ibada. Waroma wanazunguka Yerusalemu na kuharibu kuta zake fulani. (Luka 21:20) Hivyo, “lile chukizo” linasimama kwenye halingepaswa kusimama, nafasi kwenye Wayahudi waliona kuwa “mahali patakatifu.”

Yesu anatabiri tena hivi: “Kutakuwa taabu kubwa yenye haijatokea tangu mwanzo wa ulimwengu mupaka sasa, hapana, na haitatokea tena.” Katika mwaka wa 70 kisha kuzaliwa kwa Yesu, Waroma wanaharibu Yerusalemu. Shambulio hilo la “muji mutakatifu” wa Wayahudi, kutia ndani hekalu lake, linaonekana kuwa taabu kubwa, na maelfu ya watu wanaharibiwa. (Matayo 4:5; 24:21) Huo ulikuwa uharibifu mukubwa wa muji wenye Wayahudi walikuwa hawajapata kuona, na ulimaliza namna ya ibada yenye Wayahudi walikuwa wemefuata kwa mamia ya miaka. Vilevile, hivi karibuni utimizo mukubwa wa maneno ya Yesu, bila shaka utakuwa wenye kuogopesha.

KUWA NA UHAKIKA KATIKA SIKU ZA MWISHO

Mazungumuzo ya Yesu pamoja na mitume wake kuhusu alama ya kuwapo kwake katika Ufalme na mwisho wa umalizio wa mupangilio wa mambo yangali yanaendelea. Sasa anawaonya kuhusu hatari ya kufuata “Makristo wa uongo na manabii wa uongo.” Anawaambia kama Makristo hao watajaribu “kupotosha, ikiwezekana, hata wale wenye kuchaguliwa.” (Matayo 24:24) Lakini wachaguliwa hawa hawatadanganywa. Makristo wa uongo wangeonekana tu kwa inje. Lakini kuwapo kwa Yesu hakutaonekana.

Wakati anazungumuzia taabu kubwa yenye itatokea mwisho wa umalizio wa mupangilio huu wa mambo, Yesu anasema hivi: “Jua litatiwa giza, na mwezi hautatoa mwangaza wake, na nyota zitaanguka kutoka mbinguni, na nguvu za mbingu zitatikiswa.” (Matayo 24:29) Wakati mitume wanasikia maelezo hayo hawajue kabisa jambo lenye litatokea, lakini bila shaka, litaogopesha sana.

Mambo hayo yenye kuogopesha yatakuwa na matokeo gani juu ya wanadamu? Yesu anasema: “Watu watazimia kwa woga na kwa sababu ya kungojea mambo yenye yatakuja juu ya dunia yenye kukaliwa, kwa maana nguvu za mbingu zitatikiswa.” (Luka 21:26) Kwa kweli, Yesu anaeleza kwamba kipindi hicho kitakuwa kibaya zaidi katika historia ya mwanadamu.

Yesu anahakikishia mitume wake waziwazi kwamba haiko wote ndio wataomboleza wakati ‘Mwana wa binadamu anakuja na nguvu na utukufu mwingi.’ (Matayo 24:30) Amekwisha kuonyesha kama Mungu atatenda “kwa sababu ya wale wenye kuchaguliwa.” (Matayo 24:22) Kwa hiyo, wanafunzi waaminifu wa Yesu wanapaswa kutenda namna gani wakati mambo hayo ya kuogopesha yenye Yesu alizungumuzia yatatokea? Yesu anatia wanafunzi wake moyo hivi: “Lakini wakati mambo haya yataanza kutokea, musimame wima na kuinua vichwa vyenu, kwa sababu ukombozi wenu unakaribia.”—Luka 21:28.

Namna gani wanafunzi wa Yesu wenye kuishi wakati huo watajua kama mwisho unakuwa karibu? Yesu anatoa mufano kuhusu muti wa tini: “Wakati tu matawi yake machanga yanakuwa teketeke na kutoa majani, munajua kwamba kipindi cha joto kinakaribia. Vilevile ninyi pia, wakati mutaona mambo yote hayo, mujue kama iko karibu kwenye milango. Kwa kweli ninawaambia ninyi kwamba kizazi hiki hakitapita hata kidogo mupaka mambo haya yote yatokee.”—Matayo 24:32-34.

Kwa hiyo, wakati wanafunzi wake wenye kuishi katika kipindi hicho wataona mambo mbalimbali ya alama yakitimizwa, wataelewa kama mwisho unakuwa karibu. Kwa wale wanafunzi wake wenye watakuwa wazima wakati wa kipindi hicho cha maana, Yesu anawatolea onyo hili:

“Kuhusu siku ile na saa ile, hakuna mutu mwenye anajua, ikuwe malaika wa mbinguni ao Mwana, lakini Baba tu. Kwa maana kama vile siku za Noa zilikuwa, ni vile kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakuwa. Kwa maana kama vile walikuwa katika siku hizo mbele ya Garika, walikuwa wanakula na kunywa, wanaume walikuwa wanaoa na wanamuke walikuwa wanaolewa, mupaka siku Noa aliingia ndani ya safina, na hawakuhangaika mupaka Garika ikakuja na kuwaharibu wote, ni vile kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakuwa.” (Matayo 24:36-39) Yesu analinganisha tukio hilo na Garika ya siku ya Noa. Jambo hilo lilitokea katika dunia yote.

Mitume wenye wanasikiliza Yesu kwenye Mulima wa Mizeituni wanaelewa bila shaka kama wanapaswa kuendelea kuwa macho. Yesu anasema: “Mujiangalie ninyi wenyewe ili mioyo yenu isilemewe hata kidogo na kula kupita kiasi na kunywa sana na mahangaiko ya maisha, na kwa kushitukia siku ile ikuje juu yenu mara moja kama mutego. Kwa maana itakuja juu ya wale wote wenye kuishi katika dunia yote. Basi, muendelee kukesha, mukimulilia Mungu kila wakati ili muweze kuponyoka mambo haya yote yenye yanapaswa kutokea na kusimama mbele ya Mwana wa binadamu.”—Luka 21:34-36.

Hapa, Yesu anaonyesha tena kama mambo yenye anatabiri yatakuwa katika dunia yote. Matukio yenye anatabiri hayatagusa Yerusalemu tu na taifa la Wayahudi kwa miaka 30 ao 40 tu. Lakini yatakuja “juu ya wale wote wenye kuishi katika dunia yote.”

Anasema kama wanafunzi wake wanapaswa kuendelea kuwa macho, wenye kukesha, na kuwa tayari. Anakazia wazo hilo kupitia mufano huu mwengine: “Mujue jambo hili: Kama mwenye nyumba angejua ni wakati gani usiku mwizi atakuja, angekaa macho na hangeruhusu nyumba yake ivunjwe. Kwa hiyo ninyi pia mukuwe tayari, kwa sababu Mwana wa binadamu atakuja katika saa yenye hamuwazie.”—Matayo 24:43, 44.

Yesu anatolea wanafunzi wake sababu ingine ya kutazamia mambo ya muzuri. Anawahakikishia kwamba wakati unabii wake unaendelea kutimia, kutakuwa “mutumwa” mwenye kuwa macho na mwenye kutenda. Yesu anazungumuzia hali fulani yenye mitume wanaweza kuwazia haraka: “Ni nani kwa kweli mutumwa mwaminifu na mwenye busara mwenye bwana wake ameweka juu ya watumishi wake wa nyumbani, ili kuwapatia chakula chao kwa wakati wenye kufaa? Mwenye furaha ni mutumwa huyo Kama bwana wake wakati atakuja atamukuta akifanya vile! Kwa kweli ninawaambia ninyi, atamuweka juu ya mali zake zote.” Lakini kama ule “mutumwa” anakuwa na nia mbaya na kutesa “wenzake,” bwana “atamupatia azabu kwa ukali mukubwa zaidi.”—Matayo 24:45-51; linganisha na Luka 12:45, 46.

Lakini, Yesu haseme kama kikundi cha wafuasi wake watakuwa na nia ya mubaya. Kwa hiyo, ni somo gani lenye Yesu anapenda kufundisha wanafunzi wake? Anapenda wakae macho na wenye kutenda, kama vile atafasiria hilo waziwazi katika mufano mwengine.